Showing posts with label NDOA. Show all posts
Showing posts with label NDOA. Show all posts

Sunday, September 21, 2014

KWANINI UFUNGE NDOA

“Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—MHUBIRI 4:12.
JE, UNAPENDA kwenda kwenye harusi? Wengi wanapenda, kwa sababu mara nyingi hizo huwa pindi zenye kufurahisha sana. Bwana na bibi-arusi wanavalia mavazi yenye kupendeza kwelikweli. Zaidi ya hilo, nyuso zao zinaonyesha kwamba wana shangwe nyingi! Siku hiyo, wana furaha nyingi na inaonekana wana matazamio mengi mazuri ya wakati ujao.
2 Hata hivyo, ukweli ni kwamba ndoa nyingi leo ziko mashakani. Ingawa tunawatakia mema wenzi wapya wa ndoa, nyakati nyingine tunajiuliza: ‘Je, ndoa hii itakuwa na furaha? Itadumu?’ Majibu ya maswali hayo yanategemea ikiwa mume na mke wanaamini na kutumia shauri la Mungu kuhusu ndoa. (Methali 3:5, 6) Wanahitaji kufanya hivyo ili waendelee kukaa katika upendo wa Mungu. Acheni tuchunguze majibu ya Biblia kwa maswali haya manne: Kwa nini ufunge ndoa? Ikiwa utafunga ndoa, utachagua mwenzi wa aina gani? Unaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya ndoa? Na ni nini kinachoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa waendelee kuwa na furaha?
KWA NINI UFUNGE NDOA?
3 Watu fulani wanaamini kwamba siri ya kuwa na furaha ni kufunga ndoa na kwamba huwezi kamwe kutosheka au kuwa na furaha maishani ikiwa huna mwenzi wa ndoa. Hilo si kweli hata kidogo! Yesu, ambaye alikuwa mseja, alisema useja ni zawadi, naye aliwahimiza wale wanaoweza waupe nafasi. (Mathayo 19:11, 12) Mtume Paulo pia alizungumzia faida za useja. (1 Wakorintho 7:32-38) Hata hivyo, Yesu na Paulo hawakuweka sheria kuhusu jambo hilo; na ‘kukataza kufunga ndoa’ ni ‘fundisho la roho waovu.’ (1 Timotheo 4:1-3) Lakini wale wanaotaka kumtumikia Yehova bila kukengeushwa wanaweza kufaidika kwa kuendelea kuwa waseja. Basi, si jambo la hekima kufunga ndoa kwa sababu ndogo-ndogo, kama vile kufunga ndoa kwa sababu tu wenzako wamefunga ndoa au kwamba wanakutia moyo ufanye hivyo.
4 Kwa upande mwingine, je, kuna sababu nzuri za kufunga ndoa? Ndiyo. Ndoa pia ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, inatimiza mambo fulani mazuri na inaweza kuleta furaha. Kwa mfano, ndoa nzuri ndio msingi bora wa maisha ya familia. Watoto wanahitaji kulelewa katika mazingira yanayofaa wakiwa na wazazi wanaowapenda, wanaowatia nidhamu, na kuwapa mwongozo. (Zaburi 127:3; Waefeso 6:1-4) Hata hivyo, kusudi la ndoa si kupata na kulea watoto tu.
5 Fikiria andiko la msingi la sura hii pamoja na mistari inayotangulia: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake. Lakini itakuwaje kwa yule aliye peke yake akianguka wakati ambapo hakuna mwingine wa kumwinua? Tena, wawili wakilala pamoja, watapata joto; lakini aliye peke yake anawezaje kupata joto? Na mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—Mhubiri 4:9-12.
6 Andiko hilo linazungumzia hasa faida ya urafiki. Bila shaka, ndoa ni muungano wa marafiki wa karibu zaidi. Kama andiko hilo linavyoonyesha, katika muungano huo wenzi wa ndoa wanaweza kupata msaada, faraja, na ulinzi. Ili kifungo cha ndoa kiwe imara zaidi, mengi zaidi yanahitajika. Kamba yenye nyuzi mbili, kama mstari huo unavyodokeza, inaweza kukatika. Lakini kamba yenye nyuzi tatu zilizosokotwa au kufumwa pamoja haikatiki kwa urahisi. Lengo kuu la mume na mke linapokuwa kumpendeza Yehova, ndoa yao ni kama kamba yenye nyuzi tatu. Kwa kuwa Yehova anahusishwa kabisa, ndoa hiyo inakuwa muungano imara sana.
7 Pia, katika ndoa ndipo tu tamaa za ngono zinaweza kutoshelezwa inavyofaa. Ni katika kifungo hicho tu ambapo mahusiano ya kingono huonwa kwa kufaa kuwa chanzo cha shangwe. (Methali 5:18) Hata baada ya mtu kupita kipindi ambacho Biblia inakiita “upeo wa ujana”—wakati ambapo tamaa za ngono huanza kuwaka—huenda bado akahitaji kuzuia tamaa hizo. Zisipozuiliwa, tamaa hizo zinaweza kumwingiza katika mwenendo mchafu au usiofaa. Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuwapa watu ambao hawajafunga ndoa shauri hili: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.”—1 Wakorintho 7:9, 36; Yakobo 1:15.
8 Hata kuwe na sababu gani za kufunga ndoa, mtu anapaswa kuona mambo kihalisi. Kama Paulo alivyosema, wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Watu waliofunga ndoa hupata matatizo fulani ambayo waseja hawapati. Hata hivyo, ukiamua kufunga ndoa, unaweza kufanya nini ili upunguze matatizo na kuwa na furaha zaidi? Njia moja ni kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima. Etaendelea

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR