Tuesday, October 20, 2015

BI. ANNA MGWIRA: MGOMBEA URAIS TANZANIA KUPITIA CHAMA CHA ACT-WAZALENDO


Julius  S. Mtatiro's photo. Bi. Anna Mghwira ni mwenyekiti wa kitaifa wa chama kipya cha siasa, ACT – Wazalendo. Alizaliwa tarehe 23 Januari 1959 katika hospitali ya mkoa wa Singida, Kata ya Mungumaji, Kitongoji cha Irao manispaa ya Singida Mjini. (Mwezi Januari mwaka huu ametimiza miaka 56).
Baba mzazi wa Anna alikuwa diwani na kiongozi wa TANU kabla ya CCM hadi mwaka 1985, mama yake alijishughulisha na kilimo na ufugaji na wazazi hawa kwa ujumla walijipatia watoto tisa, akiwemo Bi. Anna.
Bi. Anna Mgwira alianza safari ya kielimu katika shule ya msingi “Nyerere Road” mwaka 1968 – 1974 akaendelea na elimu ya sekondari kwenye Shule ya Ufundi Ihanja kati ya mwaka 1975 – 1978 kabla ya kuhitimisha masomo ya juu ya Sekondari (Kidato cha V na VI) Lutheran Junior Seminary kati ya mwaka 1979 – 1981.
Anna aliendelea na masomo ya Chuo Kikuu mwaka 1982 baada ya kujiunga Chuo Kikuu cha Thiolojia (Chuo Kikuu cha Tumaini) na kuhitimu shahada ya Thiolojia mwaka 1986.
Mwaka huohuo 1986 alijiunga Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam akitafuta shahada ya Sheria na akaimaliza na kutunukiwa mwaka 1986.
Kati ya mwaka 1987 – 1998, Bi Anna aliendelea na shughuli za ujenzi wa Taifa, akifanya kazi ndani na nje ya nchi na kupata uzoefu mkubwa sana.
Safari ya Elimu ya Bi. Anna ilikamilikia Chuo Kikuu cha Essex nchini Uingereza ambako alianza shahada ya uzamili ya sheria (LLM) mwaka 1999 na kutunukiwa mwaka 2000.
Licha ya kuwa mwanasheria na mtheologia aliyebobea, pia amefanya kazi za maendeleo kwa muda mrefu na ana uzoefu katika uendeshaji wa serikali za mitaa, uzoefu wa utumishi katika mashirka ya kimataifa, kitaifa na mashirika ya dini ambamo amejihusisha na masuala ya wanawake, watoto, wakimbizi, utawala na haki za binadamu.
Anna ana historia ya kupenda siasa, masuala ya jamii na michakato ya maendeleo kama inavyojidhihirisha katika maandiko yake mbalimbali katika majarida na magazeti ya hapa ndani ya nchi.
Alianza siasa tangu wakati wa TANU akiwa ni mwanachama wa Umoja wa Vijana wa Tanu (Tanu Youth League) na aliwahi kushinda tuzo mbalimbali kutokana na ushiriki wa juu katika TANU lakini baadaye ilipoanzishwa CCM alipunguza ushiriki wake ili ajipe muda katika masomo na baadaye ndoa na malezi ya watoto.
Kwa kipindi kirefu hakuwa anajihusisha na siasa hadi alivyoamua kujiunga na CHADEMA mwaka 2009 ambako alishika nafasi mbili tu za Uenyekiti wa baraza la wanawake ngazi ya wilaya na Katibu wa Baraza la wanawake Mkoa.
Mwezi Machi 2015 alijiunga rasmi na chama cha ACT – Wazalendo na katika Mkutano Mkuu wa kwanza wa chama hicho, yeye ndiye akachaguliwa kuwa mwenyekiti wa kwanza wa ACT.
Bi. Anna aliolewa na Shedrack Maghwiya tangu mwaka 1982 na walibahatika kupata watoto 3 wa kiume: Fadhili, Peter na Elisha. Hata hivyo kwa bahati mbaya, mume wake hivi sasa ni marehemu.
MBIO ZA UBUNGE
Bi. Anna Mghwira alijitosa katika mbio za ubunge kwa mara ya kwanza mwezi Januari 2012 baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kutangaza uchaguzi mdogo katika jimbo la Arumeru Mashariki baada ya kifo cha Solomon Sumari.
Anna alishiriki kura ya maoni ndani ya CHADEMA akihitaji kupewa ridhaa, hata hivyo chama hicho kilimpitisha Joshua Nassari (Josh) na Bi. Anna alikuwa na kazi ya kuendelea kumuunga mkono hadi ushindi ulipotangazwa kwa chama hicho.
Pia, amewahi kugombea ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki, kupitia CHADEMA japokuwa hakuchaguliwa kushikilia wadhifa huo.
MBIO ZA URAIS
Bi. Anna Mghwira hajatangaza kuwa atagombea urais. Ila, tafiti kadhaa na maoni ya watanzania zinaonesha kuwa yeye ni miongoni mwa viongozi wa kisiasa ambao wamejipambanua hivi karibuni na kuonesha uwezo mkubwa katika uwanja wa kisiasa na hivyo anapewa nafasi kubwa kuwa anaweza kupewa majukumu makubwa na anaweza kuyahimili.
NGUVU YAKE
Jambo la kwanza linalompa nguvu mwanamama huyu ni Umahiri katika elimu. Yeye nimsomi nguli wa masuala ya sheria lakini ana shahada tatu za vyuo vikuu. Nchi yoyote ingependa pamoja na sifa zingine, iongozwe na Rais ambaye elimu si kikwazo kwake. Kwa nchi kama Tanzania ambayo “mfumo dume” umewakandamiza wanawake kwa kipindi kirefu, Anna anakuwa mmoja wa wanawake wachache wenye uwezo mkubwa sana.
Kwa sababu Bi, Anna ni Mwanamke imara na anayepambana kwa muda mrefu sasa. Kitendo tu cha yeye kuwa mwanamke ni baraka tosha kwa siasa za kisasa ambazo zinaanza kuchangamkia, kukubali na kutafuta mchango wa wanawake katika Nyanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa. Jinsia yake inampa fursa ya kuendelea kuaminiwa zaidi katika jamii ambayo inazidi kupoteza imani na uaminifu wa wanaume kama Tanzania.
Lakini nguvu ya tatu ya Bi. Anna ni uthubutu. Ameniambia kuwa hata alipoingia katika ndoa bado alithubutu kujiendeleza kielimu bila kuchoka. Alipambana na changamoto za ndoa na shule. Wanawake wengi huchagua kufanya jambo moja na kuacha mengine, yeye alikwenda nayo yote na kuyakamilisha salama. Uwezo na uthubutu huu vinamfanya kuwa mwanamama imara anayeweza kukabidhiwa uongozi wa taasisi kubwa.
Anna ni mtu wa kuhoji kila jambo, si mwanamama “Ndiyo Mzee”. Wakati natafuta maoni ya watu waliowahi kufanya naye kazi katika Kituo cha Haki za Binadamu, mtendaji mmoja aliniambia kuwa ukimpa Anna kazi ya harakati iliyo kwenye maandishi, hataondoka kwako hadi umpe taarifa za kina za kila jambo na atakuhoji hadi utachoka.
Hata mtaalam mshauri wa chama hicho Prof. Kitila Mkumbo, ameniambia kuwa wakati wanafanya marekebisho ya katiba ya chama cha ACT walikabidhi kazi hiyo kwa jopo maalum la wataalam akiwemo Bi. Anna. Kitila ananiambia kuwa, kwa kiasi kikubwa katika timu yeye ndiye aliyehoji na kutoa mapendekezo ya masuala mengi kuliko hata wataalamu wengine wa sheria ambao walikuwa wanaume.
Mimi binafsi nilipojaribu kumfikia Bi. Anna kwa ajili ya kupata taarifa zake za kina na maisha binafsi, nilijikuta nashushiwa maswali matano mfululizo kiasi kwamba nilirudi kujipanga na kumtafuta tena. Huyu ni mwanasiasa wa kisasa ambaye anahoji kila jambo lililoko mbele yake, sifa hii wanaikosa wakuu wengi sana wa nchi.
Pamoja na kuwa na elimu kubwa, uzoefu wa kutosha wa kukaa nje ya nchi na kufanya kazi na taasisi za kitaifa na kimataifa, Bi. Mghwira ni Mwanamama wa kawaida sana. Watu wa karibu naye wanamtaja hivyo. Si mtu wa kupoteza muda na mambo yasiyo na tija, anapenda kuandika makala zakuelimisha jamii, kufanya kazi na jamii na kujitolea na kujichanganya na wananchi wasio na uwezo na wenye kuhitaji msaada. Sifa zote hizi ni nguvu muhimu kwa binadamu yeyote ambaye anahitaji uongozi mkubwa wa nchi.
UDHAIFU WAKE
Udhaifu mkubwa nilioubaini na hata kujulishwa na watu wa karibu na Bi.Anna Mghwira, yeye ni mwanasiasa mpole sana. Nimeambiwa kuwa ni mpole kupita kiasi na mara nyingi huwa anakuwa msikilizaji mzuri kabla hajaanza kuhoji mambo mfululizo. Moja ya sifa muhimu za Rais ajaye ni uwezo wa kuwa mpole na mkali kutegemeana na mazingira.
Kiwango cha upole cha mwanamama huyu kinazidi kiwango cha ukali alionao na naliona kama ni jambo linalopaswa kufanyiwa kazi kwa sababu taifa letu lilipofikishwa, mara kadhaa nimesisitiza kuwa tunahitaji kiongozi anayeweza kumudu hali zote mbili.
Lakini udhaifu wa pili mkubwa wa Bi. Anna Mghwira ni kutojijenga kisiasa ndani ya nchi. Katika siasa bado namuona kama mchanga, hajakomaa na kuwa na uwezo mkubwa kisiasa kiasi cha kujipa jina kubwa kwa jamii.
Mchango wake katika jamii ni mkubwa kwa sababu amewahi kusimamia masuala mengi ya kijamii na kisheria yanayoonekana, lakini nachokisema hapa ni kuwa, chama chochote kila kina jukumu la kusimamisha kiongozi ambaye anajulikana sana katika tasnia za siasa. Kutojijenga na kuwa juu tokea alipokuwa CHADEMA n.k. nakuchukulia kama udhaifu ambao anahitaji kuufanyia kazi.
NINI KINAWEZA KUMFANYA APITISHWE
Kama ACT Wazalendo itampitisha mwanamama huyu kuwa mgombea urais wa chama hicho katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, Sababu ya kwanza ya kufanya hivyo inaweza kuwa ni ile dhana ya kumpa mwanamke nafasi.
Chama anachotoka ndicho peke yake kimeweza kumpa mwanamke nafasi ya juu ya uongozi wa chama, nadhani pia bado chama hicho kinaweza kumpa jukumu kubwa zaidi ya hilo kwa sababu tayari kimeshajijengea misingi ya kuwajenga kina mama.
Lakini ikiwa Anna Mghwira atapitishwa, Uzoefu wake kimataifa na katika masuala ya haki za binadamu na kushughulika na masuala ya kijamii kunaweza kuwa moja ya sababu.
Mwanamama huyu amefanya kazi mbalimbali za kitaaluma na kijamii hapa Tanzania, nchini Sweden, Marekani, uingereza na nchi nyingine za Afrika. Amekuwa mwalimu wa Vyuo Vikuu hapa Tanzania na msimamizi wa miradi mbalimbali ya kitaifa ya mashirika ya ndani na nje ya nchi. Uwezo na uelewa wake vinampa fursa ya juu ya kuteuliwa kugombea urais na kuonesha kuwa kina mama wanaweza ikiwa wanapewa fursa sawa na wanaume.
NINI KINAWEZA KUMWANGUSHA KWENYE MCHUJO?
Dhana ileile ya kijinsia inayombeba, pia ndiyo inaweza kumuangusha. Ikiwa ACT itadhani kuwa vyama vingine washindani vitasimamisha wagombea wanaume imara ambao wanaungwa mkono na mfumo dume uliotawala nchi hii, chama hicho kinaweza kumuweka nje Bi. Mgwira na kutafuta mwanachama mwingine “mwanaume” ambaye atakuwa na fursa ya kupambana na wanaume wengine kutoka vyama vingine na kuangaliwa na jamii “ambayo kwa kiasi kikubwa bado inatawaliwa na wanaume”.
Lakini jambo la pili linaloweza kumwangusha ni ugeni wake katika masuala ya kisiasa. Kama nilivyoeleza, Anna Mghwira hana uzoefu wa uongozi wa juu wa kisiasa katika vyama, nadhani nafasi aliyonayo ndani ya chama cha ACT Wazalendo ndiyo inayompa uzoefu wa kwanza wa siasa za kitaifa.
Lakini uzoefu wa jumla unaonesha kuwa vyama mbalimbali hapa Tanzania huteua wagombea urais wake miongoni mwa wanachama wazoefu au wale waliowahi kushika madaraka muhimu katika chama kwa muda mrefu. ACT ikipiga hesabu hizi inaweza kabisa kumuweka nje mwanamama huyu.
MIPANGO MINGINE IWAPO HATACHAGULIWA NA CHAMA CHAKE (PLAN B)
Ikiwa Bi. Anna Mgwira hatapewa fursa ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama chake, anaweza kuwa na mipango mitatu mezani:
Mpango wa kwanza ni Kugombea ubunge katika jimbo mojawapo Tanzania. Bahati nzuri nimejulishwa kuwa moja ya majimbo anayojipanga kugombea ni pale Singida. Ikiwa ndivyo basi, mpango huu unaweza kumfaa kwa maana ya kuzidi kujifunza na kupata uzoefu wa siasa za Tanzania kwa upana.
Lakini mpango wa pili ni kuendelea kufundisha vijana katika Vyuo Vikuu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kutoa ushauri nasaha kwa wanafunzi na ushauri wa kisheria katika jamii. Masuala haya Bi. Anna ana uzoefu nayo, itakuwa tu ni kiasi cha kuendelea pale alipoishia, huwenda mara hii kwa kasi kubwa zaidi.
Nadhani mpango wa tatu ni kuendelea kuongoza chama cha ACT Wazalendo. Nimeambiwa kuwa uongozi (Uenyekiti wake) unapaswa kuisha mwaka 2020 mwezi Februari. Ikiwa ndivyo nadhani ana fursa njema ya kuendelea kufanya uongozi.
HITIMISHO
Bi. Anna Mgwira ni mwanasiasa na kiongozi wa chama kipya ambacho kimeanzishwa na wanachama wengi waliotoka CHADEMA. Safari yake kisiasa na hata ugombeaji wa nafasi zingine kubwa za nchi kwa namna moja ama nyingine lazima utaathiriwa na ustawi au uzorotaji wa CHADEMA.
Ikiwa CHADEMA itazidi kukubalika kwa watanzania na kuwa chama kinachoimarika zaidi kuishinda ACT, ndiyo kusema kuwa yeye na wenzake watakuwa kwenye wakati mgumu sana kujipambanua kisiasa, na hivi ndivyo siasa za Afrika hutizamwa.
Pamoja na “sintofahamu” hizo, namuona Bi. Anna Mgwira kama mmoja wanasiasa watulivu sana na wenye maono mapana katika taifa hili. Kwa maneno yake yeye mwenyewe amenieleza kuwa “…Natamani siku moja nchi hii iongozwe kwa misingi ya udugu na kusaidiana, kwa misingi ya malezi ya maadili bora kama alivyofanya Mwalimu Nyerere – Mimi nimekulia kwenye familia kubwa sana lakini wazazi wetu walitulea sote kama ndugu, na tuliishi kwa furaha kubwa, nina ndoto kuwa Tanzania ijayo ipite katika njia hiyo…”
Nachoweza kusema kwa sasa ni kumwombea mama huyu na mwanamama nguli wa upinzani, na kumtakia safari njema katika nia zake za kisiasa ikiwa hii ambayo ametajwa sana, kwamba ana sifa za kuongoza Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mchambuzi wa Safu hii ni Julius Mtatiro, Adv Cert in Ling, B.A, M.A, L LB (Continuing): juliusmtatiro@yahoo.com, +255787536759.

FAHMI DOVUTWA: MGOMBEA URAIS WA TANZANIA KUPITIA CHAMA CHA UPDP.


Fahmi Nasoro Dovutwa ni Mwenyekiti wa Kitaifa wa Chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP). Alizaliwa tarehe 27 Februari 1957 huko Kisarawe mkoani Pwani(Amefikisha miaka 58 mwezi Februari mwaka huu).
Dovutwa alianza elimu yake ya Msingi mwaka 1967 katika shule ya msingi Zanaki hadi alipohitimu mwaka 1974 alipoendelea na masomo ya Sekondari katika shule ya sekondari Azania ambako alihitimu mwaka 1977.
Rekodi za elimu za Dovutwa zimekuwa “kizungumkuti” kupatikana. Hata taarifa zake binafsi alizotoa kwa ajili ya rekodi za Bunge Maalum la Katiba zinasisitiza kuwa ameishia kidato cha nne.
Juhudi za kumpata yeye mwenyewe ili akamilishe rekodi zake hazikufua dafu na ni yeye peke yake tangu nianze kufanya uchambuzi wa watu wanaotajwa kuwania urais, ambaye hakutoa ushirikiano kabisa ili kunifanya nipate rekodi zake sahihi.
Watu wa karibu yake wamenijulisha kuwa kwa muda mrefu amekuwa akijishughulisha na kazi za ujasiriamali katika soko la Magereza jijini Dar Es Salaam hadi baadaye alipochaguliwa kuongoza chama cha UPDP ambacho yeye ni mwenyekiti hadi sasa.
Mwaka 2014 yeye alikuwa ni miongoni mwa watanzania waliopata fursa ya kuteuliwa na Rais wa Tanzania kupitia kundi la vyama vya siasa, na kuwa mjumbe wa bunge maalum la katiba lililofanya kazi yake mjini Dodoma na kukamilisha katiba inayopendekezwa ambayo hata hivyo imeligawa taifa katika vipande viwili.
Dovutwa ameoa na ana watoto.
MBIO ZA UBUNGE
Katika historia ya kisiasa ya Dovutwa, hakutoa pia rekodi zinazoonesha kama aliwahi kugombea ubunge katika jimbo lolote na hata nilipozitafuta sikufanikiwa kuzipata.
MBIO ZA URAIS
Kiongozi huyu alijitosa katika mbio za urais mwaka 2010 akitumia tiketi ya chama chake cha UPDP. Katika uchaguzi ule ambao Jakaya Mrisho Kikwete aliongoza kwa ushindi wa asilimia 62.83, akifuatiwa na Willibroad Slaa aliyekuwa na ushindi wa asilimia 27.5, na Prof. Ibrahim Lipumba wa CUF akiwa na asilimia 8.28, Dovutwa aliibuka katika nafasi ya mwisho akiwa na asilimia 0.16 ya kura zote kwa kupitwa na Peter Mziray wa APPT (asilimia 1.15), Hashim Rungwe wa NCCR (asilimia 0.31), na Mutamwega Bhatt wa TLP aliyekuwa na asilimia 0.21 ya kura zote.
Katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu, Dovutwa hajatangaza popote kuwa atagombea tena nafasi ya Urais lakini duru za kisiasa ndani ya chama hicho ikiwemo kutoka kwa baadhi ya viongozi waandamizi, zimenieleza kuwa anapewa nafasi kubwa ya kugombea tena.
NGUVU YAKE
Jambo la kwanza nalolitizama kama nguvu ya Dovutwa ni “Umaarufu”. Nathubutu kusema kuwa huyu ni mmoja wa viongozi maarufu wa wa vyama visivyo na wabunge. Mikogo yake ya kuvutia katika kampeni za mwaka 2010.
Uvaaji wake kuanzia chini hadi “kofia nyekundu”, vilimtofautisha na mgombea yeyote yule kwenye uchaguzi ule. Mimi binafsi nilijikuta navutiwa sana na staili za kiongozi huyu hata kama sikuwa najua sera za chama chake kwa mwaka 2010. Nguvu hii ya kuvutia macho nayo ni muhimu sana kwa mwanasiasa yeyote, hata kama ukiwa na elimu kubwa, mipango mingi n.k. suala la unavaaje, unavutiaje na ukoje (mtazamo wa nje), halikwepeki katika siasa.
Lakini pia, Dovutwa ni Mjasiriamali mzoefu na sifa hii pia inamuongezea nguvu mtu yeyote yule ambaye anataka uongozi wa juu wan chi. Tena nimeambiwa kuwa amekuwa mjasiriamali mdogo kwa kipindi kirefu na hasa akifanya kazi na vijana wa chini. Natambua kuwa fursa hiyo ilimpa nafasi kubwa ya kuendela kuyaishi maisha ya vijana wa chini na hata kujua masuluhisho ya haraka, ya muda mfupi na muda mrefu, kwa sababu pia ukishaingia ikulu kazi yako kubwa ni kutafuta majawabu ya masuala ya watu. Majawabu ya muda mrefu na muda mfupi.
UDHAIFU WAKE
Udhaifu wa kwanza wa Dovutwa uko katika elimu (hadi hapo atakapowajulisha watanzania elimu yake rasmi tofauti na iliyoko kwenye vyanzo sahihi vya taarifa kama tovuti ya Bunge Maalum la Katiba), udhaifu huu unasimama kama ulivyo kwa sababu taifa letu linakwenda mbele hivi sasa na elimu ni jambo la msingi katika uongozi, hata kama siyo kila kitu.
Kukosekana kwa taarifa za elimu yake tofauti na ilivyo kwa viongozi wengi wa vyama vya siasa ni jambo linaloleta mashaka juu ya weledi wa kiongozi huyu. Kwa karne ya sasa na hapa Tanzania kulikojaa wasomi, ni nadra sana ikatokea kwamba mtanzania mwenye elimu ya Kidato cha nne tu “akawa na ndoto za kuingia ikulu na jambo hilo likatekelezeka”.
Lakini jambo la pili, Dovutwa mara nyingi amekuwa ni mtu wa Kukosa Ajenda na matokeo yake hupenda kurukia ajenda za masuala ambayo hayana tija. Mara kadhaa ameonekana katika vyombo kadhaa vya habari akivishambulia sana vyama vya upinzani lakini akiwa hafanyi hivyo kwa CCM. Hali hii inamuweka katika sahani ya wanasiasa ambao wanashangaza kidogo na nadhani huu ni udhaifu mkubwa sana kama kweli bado ana ndoto za kugombea urais, achilia mbali kuingia ikulu.
Uhusiano wenye mashaka baina yake na CCM ni suala lingine linalosisitiza juu ya udhaifu wake. Dovutwa, akiwa mgombea urais kwenye uchaguzi wa Oktoba mwaka 2010, aliwashangaza watanzania katikati ya kampeni huku Chama Cha Mapinduzi kikionekana kuzidiwa sana na upinzani, hususani CHADEMA na CUF, Dovutwa alijitokeza hadharani (akiwa mgombea) na kutangaza kuwa chama chake na vyama vingine kadhaa visivyo na wabunge na mitandao mikubwa “ati” vinamuunga mkono mgombea wa CCM, Jakaya Mrisho Kikwete.
Hata hivyo Tume ya Taifa ya Uchaguzi haikukubaliana na kujitoa huko kwa baadhi ya vyama na kusisitiza kuwa kisheria muda wa kujitoa umekwisha. Tamko na msimamo ule ambao sina uhakika kama kweli ulitokana na vikao vya chama chake, vina maana kuwa huwenda anafanya “kazi maalum” katika siasa za ndani ya nchi. Kwa sababu, katika mantiki ya kawaida, si jambo rahisi chama cha upinzani kufanya maamuzi ya kuunga mkono chama kinachoongoza, katika nchi inayosaka demokrasia kama yetu.
Katika Bunge Maalum la Katiba, Dovutwa ni mmoja wa viongozi ambao pia walishangaza sana watanzania. Yeye ni mmoja wa wabunge wa bunge lile ambao walisimama hadharani mara kadhaa na “kuponda” msimamo wa vyama vya UKAWA lakini bila kueleza kuwa anaunga mkono upande upi.
Ni jambo la hatari sana chama cha siasa au viongozi wa vyama vya siasa wanapokwenda katika kazi kubwa ya kitaifa bila kuwa na ajenda ya msingi ya kuisimamia. Ndiyo maana kulikuwa na sintofahamu hiyo ambayo iliegemea upande mmoja bila kutafakari kuwa vyama vilivyoondoka katika mchakato ule navyo vilikuwa na hoja zao. Viongozi kama Dovutwa walipaswa kufanya kazi ya kujenga hoja kuliko kuendelea “kuponda” UKAWA, jambo lililowapotezea muda na kushindwa hata kujenga taswira za vyama vyao.
Lakini udhaifu mwingine wa Dovutwa ni Kushindwa kukihuisha chama chake. Chama cha UPDP hakijapata ushindi wa kujivunia katika Uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika mwezi Disemba 2014. Chama hiki kilizidiwa na vyama vipya kama ACT na ADC ambavyo viliambulia viti kadhaa katika maeneo mbalimbali ya nchi. Kama Dovutwa ameshindwa kukihuisha chama chake kisimamie ajenda muhimu za kitaifa hapa nchini lakini pia kufanya vibaya sana hata katika uwakilishi chini wa wananchi, hizo siyo dalili nzuri kwa kiongozi ambaye anatarajia kuwa kiongozi wa nchi.
Baadhi ya viongozi waandamizi wa UPDP walioongea name, wameniambia kuwa chama chao kimekuwa na matatizo makubwa sana katika kufanya uchaguzi wa kikatiba wa kila baada ya awamu. Baadhi yao wameeleza kuwa baadhi ya viongozi wa juu wa chama hicho mara kadhaa wamekuwa na uoga kuwa chaguzi zikifanyika kwa uwazi na haki, huwenda wakaangushwa.
Tuhuma hizi pia zinamgusa Dovutwa mwenyewe ambaye amewahi pia kuonekana kwenye kipindi kimoja che televisheni akijitetea kuwa chama chake kitajitahidi kukamilisha chaguzi zake za ndani. Kama Dovutwa anashindwa kusimamia chaguzi za chama chake kwa uhakika na kwa wakati hadi anasuasua sana, ni dalili tosha kuwa kazi ya urais wa nchi inaweza kumuwia ngumu kupita kiasi.
NINI KINAWEZA KUMFANYA APITISHWE
Jambo moja ambalo naona linaweza kumvusha Dovutwa katika harakati za ndani ya chama chake za kupewa ridhaa ya kugombea urais ni Uongozi wake ndani Chama. Dovutwa ndiye kiongozi mkuu wa UPDP na jambo hilo kwa siasa za Afrika lina maana kuwa mara nyingi yeye ndiye mwenye nafasi kubwa ya kupewa ridhaa muhimu kama hizi, mara zinapotokea. Sitashangaa kuona chama chake kikimpitisha kwa sababu yeye ni mwenyekiti wa chama.
Lakini jambo la pili linaloweza kumfanya apitishwe ni kwa sababu aligombea urais mwaka 2010. Mipango na mbinu alizotumia mwaka 2010 pamoja na kwamba zilimpa nafasi ya mwisho lakini tunakubali kuwa kuna baadhi ya watanzania walimpigia kura. Ndiyo kusema kuwa UPDP kama inahitaji kura zaidi katika uchaguzi wa mwaka huu huwenda yeye Dovutwa akapaswa kutumia uzoefu wake wa mwaka 2010 ili kufanikisha jambo hilo.
NINI KINAWEZA KUMWANGUSHA KWENYE MCHUJO?
Jambo la kwanza linaloweza kukifanya chama chake (UPDP) kisimpitishe kugombea urais, nadhani ni itakapotokea kuwa chama hicho kina mgombea urais mwingine mwenye sifa na uwezo mkubwa kumshinda. Kama nilivyoeleza awali, elimu tu ya Dovutwa haieleweki na inawezekana kabisa kuwa hata yeye mwenyewe hapendi kuiweka wazi. Ikiwa chama chake mathalani kikapata mtu mwingine mwenye elimu kubwa sana na uwezo kumshinda, nadhani Dovutwa anaweza kupumzishwa katika nafasi hiyo.
Lakini jambo la pili linaloweza kumfanya asipitishwe ni ikiwa Hoja ya mwaka 2010 ya kumuunga mkono Kikwete itatiliwa mashaka katika vikao vya maamuzi vya chama chake. Baddhi ya viongozi waandamizi wa UPDP waliokubali kuongea nami wamesisitiza kuwa hatua ile ya Dovutwa ya mwaka 2010 haikupita katika vikao vya maamuzi. Ikiwa atatiliwa mashaka kuwa anaweza tena kufanya yale ya mwaka 2010, huwenda sababu hii pia ikamuweka nje ya mbio hizi.
MIPANGO MINGINE IWAPO HATACHAGULIWA NA CHAMA CHAKE (PLAN B)
Ikiwa Dovutwa hatapitishwa kugombea urais wa Tanzania, huwenda akawa na mipango kama mitatu mezani:
Mpango wa kwanza unaweza kuwa kutafuta jimbo na kugombea nafasi hiyo.Lakini nadhani kwa nguvu dhaifu ya chama chake ni vigumu pia kushinda jimbo lolote, maana kama chama hakina wenyeviti wa serikali za mitaa wa kutosha, madiwani n.k ni vigumu kudhani kuwa kitapata “mbunge” kutoka mbinguni.
Mpango wa pili unaweza kuwa ni kuendelea na uongozi wa ndani ya chama chake. Mpango huu ndio anaendelea nao hadi sasa na nimeambiwa kuwa kunaweza kufanyika uchaguzi mwingine katika chama hicho na kwamba bado atatetea nafasi yake ya uenyekiti, jambo ambalo halina shida kidemokrasia.
Na mpango wa tatu unaweza kuwa kuunganisha nguvu za vyama vya upinzani visivyo na wabunge ili kuunda umoja wao. Tayari nina taarifa za kina kuwa baadhi ya vyama visivyo na wabunge vinaendelea na vikao vya chini kwa chini ili vione kama na vyenyewe vinaweza kuunda “UKAWA” yao. Mpango huu utakuwa unamhusu sana Dovutwa kwa sababu natambua ushawishi alionao juu ya vyama visivyo na wabunge.
HITIMISHO
Dovutwa ana changamoto kubwa sana katika siasa za Tanzania. Ukiachilia mbali kwamba yuko katika chama kisicho hata na diwani lakini nisisitize kuwa taswira kadhaa za chama hicho zinamsababishia yeye na wenzake hukumu ambazo wakati mwingine zingeepukika kama zingefanyiwa kazi.
Kama nilivyoeleza pale juu, huyu ni mmoja wa viongozi wa vyama visivyo na wabunge ambaye ana mvuto wa pekee unaotokana na staili zake za kufanya mambo na ubunifu wa mavazi n.k. Hayo peke yake hayatoshi. Ana jukumu kubwa sana la kusimamia uhuishaji wa chama chake na kufuta makosa ya nyuma kuliko kusonga mbele.
Nafasi ya Dovutwa kisiasa ndani ya nchi natumaini kuwa itaendelea kuwa palepale (bila kukua) kwa sababu watanzania wa sasa wanazidi kupata weledi mkubwa unaowasaidia katika ufanyaji wa maamuzi mbalimbali.
Siasa za sasa zinataka viongozi wepesi sana ambao sioni kama Dovutwa ni mmoja wao. Ikiwa mwenyekiti wa chama cha siasa kilichosajiliwa unaombwa wasifu wako na hauutoi kwa wiki kadhaa ina maana kuwa hata wanaokupigia chapuo kuwa una uwezo wa kugombea nafasi fulani ya juu wanakuwa wanakosea sana.
Pamoja na mapungufu lukuki ambayo nimeyabainisha kutokana na hali halisi inayomkabili kiongozi huyu, namtakia kila lililo jema katika mipango yake ya mbele kisiasa huku nikimpa nafasi finyu ya kuwa mgombea mwenye mafanikio ikiwa atafanya hivyo Oktoba mwaka huu

MJUE HAMAD RASHID MGOMBEA URAIS ZANZIBAR KUPITIA ADC.

HAMAD RASHID: NANI NI NANI URAIS UPINZANI?
HISTORIA YAKE
Hamad Rashid Mohamed ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwakilisha wananchi wa jimbo la Wawi, Pemba. Alizaliwa tarehe 01 Machi 1950 huko Zanzibar na kusoma katika shule ya msingi ya Wavulana ya Chake kati ya mwaka 1958 hadi 1967. Amesoma Sekondari (kidato cha kwanza hadi cha nne) kati ya mwaka 1968 – 1970 katika Shule ya Sekondari Chanjamjawiri huko huko Zanzibar (Mzunguko wa Kwanza).
Hamad Rashid alisoma kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari Fidel Castro kati ya mwaka 1970 – 1971. Na wakati huohuo kati ya mwaka 1974 – 1976, alipata mafunzo ya muda mrefu ya masuala ya Kibenki katika Chuo cha Mafunzo cha Benki ya NBC.
Baadaye mwaka 1980 Hamad Rashid alijiunga katika chuo cha Itikadi cha Zanzibar na kupata stashahada kati ya mwaka 1981 na mwaka 1981 alienda kusoma katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Francis Xavier kilichoko huko Antigonish katika mji wa Nova Scotia nchini Canada, na kuhitimu stashahada ya Maendeleo ya Jamii mwaka 1982.
Kwa upande wa ajira, Kwa miaka mitano (1972 – 1977), Hamad Rashid aliajiriwa na Benki ya watu (People’s Bank) kama karani na mwaka 1979 hadi 1982 akateuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Ushirika Tanzania.
Kisiasa Hamad Rashid amekuwa mwanachama wa ASP na baadaye CCM, kabla hajahamia Chama Cha Wananchi CUF baada ya kufukuzwa CCM mwaka 1988. Amekuwa Katibu wa Vijana wa ASP kati ya mwaka 1970 – 1972, amefanya kazi na benki ya ASP kati ya mwaka 1972 hadi 1977, amekuwa mwakilishi wa CCM katika Chama Cha Ushirika kati ya mwaka 1978 – 1988 na amewahi kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM kuanzia mwaka 1982 – 1988.
Uanachama wa Hamad Rashid na wenzake kadhaa ndani ya CCM ulikoma mwaka 1988 baada ya chama hicho kuwavua nyadhifa zao zote za uongozi wa kichama na kiserikali kwa sababu ya tuhuma kadha wa kadha ambazo ni vigumu kuzithibitisha hadi leo. Yeye mwenyewe na wenzake mara kadhaa wamesisitiza kuwa walifukuzwa kwa kuonewa na kw sababu tu walionekana wanatetea misimamo thabiti ambayo CCM haikuipenda kwa woga usio na maana.
Mwaka 1992 Hamad Rashid alikuwa mmoja wa waasisi na waanzilishi wa Chama Cha Wananchi CUF ambako ametumikia nyadhifa kadhaa za ndani ya chama ikiwemo ukurugenzi wa chama katika vipindi kadhaa, ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya Taifa, Ujumbe wa Baraza Kuu la Uongozi la taifa n.k.
Hamad Rashid akiwa CUF alikuwa mmoja wa viongozi waliofanya kazi kubwa katika kusimamia mazungumzo ya kutafuta muafaka kati ya CUF na CCM (akiiwakilisha CUF).
Hamad Rashi ameoa na ana watoto.
MBIO ZA UBUNGE
Akiwa ndani ya CCM, Hamad Rashid ni mmoja wa wanasiasa walioanza kuwa wabunge takribani miongo zaidi ya mitatu iliyopita. Amekuwa mbunge kwa mara ya kwanza mwaka 1978 - 1988 na wakati huo pia akiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania kati ya mwaka 1980 – 1982 na Naibu Waziri wa Madini, Fedha na Uchumi wa Tanzania kati ya mwaka 1982 – 1988.
Lakini hata katika uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi uliofanyika mwaka 1995, Hamad Rashid alichaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar na kutumikia nafasi hiyo hadi mwaka 2000.
Kuanzia mwaka 2000 - 2005 Hamad Rashid aliteuliwa na Rais wa Tanzania wakati huo, Benjamin Mkapa, kuwa Mbunge katika Bunge la Tanzania. Mwaka 2005 alijitosa katika jimbo la Wawi akiomba kuchaguliwa kuwa mbunge na aliungwa mkono na asilimia 75 ya wapiga kura kwenye masanduku. Kuchaguliwa kwake kulimfanya achaguliwe pia na wabunge wa kambi rasmi ya upinzani bungeni, kuwa kiongozi mkuu wa kambi hiyo, wadhifa ambao aliutumikia hadi mwaka 2010.
Kwenye uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 alitupa karata zake kwa mara nyingine pale Wawi na kufanikiwa kuchaguliwa tena lakini mara hii hakuweza tena kuendelea na wadhifa wa kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni kwa sababu CUF haikuwa na wabunge wengi ili kufikia vigezo vya kuongoza kambi hiyo.
Hadi niandikapo kumhusu, yeye ni mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania japokuwa Chama Chake (CUF) kilikwishamvua uanachama mwaka 2012 kutokana na tofauti kati yake na viongozi wenzake. Alipovuliwa uanachama moja kwa moja ilikuwa na maana ya kupoteza nafasi ya ubunge kwa mujibu wa katiba, lakini alikwenda kutafuta haki katika Mahakama Kuu ya Tanzania ambako liliwekwa zuio la muda la kutekeleza wa uamuzi wa vikao vya CUF hadi mahakama itakapoamua juu ya shauri alilolipeleka. Hadi mwaka huu wa uchaguzi bado mahakama haijaamua shauri ambalo Hamad Rashid alilifungua dhidi ya chama chake na ndiyo kusema kuwa atamaliza kipindi chake cha ubunge mwezi Julai na hivyo mvutano ulioko mahakamani kuisha kwa mtindo huo.
MBIO ZA URAIS
Hamad Rashid hajatangaza kugombea Urais wa Jamhri ya Muungano wa Tanzania lakini nilipofanya utafiti na kuwauliza baadhi ya viongozi na wanachama wa ADC walimtaja kama mmoja wa watu muhimu ndani ya chama hicho wenye sifa, uwezo vigezo na ari ya kuweza kugombea urais, kuleta ushindani na hata kushinda wakitokea vyama vya upinzani. Hiyo ndiyo sababu iliyomfanya aingie kwenye orodha hii.
NGUVU YAKE
Mambo makubwa matatu nayatizama kama karata zinazompa Hamad Rashid nguvu na ubavu wa kugombea kiti cha Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania:
Kwanza, kiongozi huyu ni mzoefu sana katika masuala ya ndani na nje ya serikali. Hamad Rashid amekuwa serikalini kwa miaka zaidi ya 30, amesimamia masuala mengi ndani ya serikali na ni watanzania wachache sana wenye rekodi kama yake. Kwa sababu Rais bora pia huhitaji kuwa na ufahamu wa kutosha kuhusu masuala ya kiserikali, Hamad Rashid ameshavuka kigezo hiki na kinampa nguvu thabiti.
Lakini jambo la pili ni uelewa mkubwa. Kati ya viongozi ambao ukipishana nao unaona kabisa ngazi kubwa ya uelewa wao ni pamoja na Hamad Rashid, yeye si msomi sana, si Daktari wala Profesa na si mtu mwenye shahada nyingi lakini akianza kujenga hoja au kushauri njia za utatuzi wa masuala ya wananchi unaweza kuona uwezo wa baadhi ya maprofesa na madaktari wakiwa chini yake, yeye ni mmoja wa wanasiasa ambao hunifanya niamini kuwa elimu si kila kitu katika uongozi, inahitaji kuambatana na masuala mengine mengi ndiyo inakuwa na manufaa kwa jamii. Uelewa wa Hamad Rashid kwa maana ya mambo ya Tanzania na ya kimataifa unamvusha katika chujio la watu ambao wanaweza kutiliwa mashaka kiuwezo katika uongozi wa juu wa nchi.
Lakini jambo la mwisho linalozidisha nguvu yake ni ile rekodi ya kuweza kufanya kazi na baadhi ya viongozi wakuu waliowahi kuongoza taifa hili pamoja na wale wa upinzani. Tangu enzi za Nyerere, Hamad Rashid hakukosa japo kuteuliwa kuongoza wizara nyeti, na hata wakati wa Mwinyi vivyo hivyo. Ulipokuja mfumo wa vyama vingi na baada ya yeye na wenzake kufukuzwa CCM alianza kufanya kazi na viongozi wenye majina makubwa katika vyama vya upinzani. Rekodi hii nayo inamuweka juu sana, kwamba katika kipindi chote hicho ameweza kuchota uzoefu wa kutosha wa masula ya uongozi wa nchi na hapo huwezi kumtilia shaka.
UDHAIFU WAKE
Jambo moja ambalo nalichukulia kama udhaifu mkubwa sana wa Hamad Rashid ni ile hali ya kutovumilia kukaa bila kuwa kiongozi hata kama mazingira ya wakati husika hayaruhusu nia yake kutekelezeka. Watu waliofanya kazi na kiongozi huyu kwa muda mrefu kutoka ndani ya CUF wamenifahamisha kuwa yeye huhitaji kuwa kiongozi mahali popote pale alipo, na jambo hilo lisipotokea huweza kuchukua hatua zozote ambazo atadhani zinafaa kwa wakati husika.
Watu wenye tabia kama yake hupata matatizo makubwa sana katika siasa za Afrika ambako masuala ya uongozi si ya kupokezana vijiti na hata katika siasa za Tanzania ambako viongozi katika vyama wanakaa muda mrefu ili kutekeleza dhana nyingine ya kuvihuisha vyama walivyomo. Kwa mtu ambaye si mvumilivu, siasa za Afrika ni ngumu sana kwenye eneo hili na inaonekana Hamad Rashid hajakubaliana na jambo hilo, matokeo yake atapata matatizo ya kisiasa katika majukwaa mengi atakayopitia na jambo hili limewaponza wanasiasa wengi wa Afrika.
Lakini jambo la pili, Hamad Rashid ni mtu mwenye mipango mingi isiyotekelezeka. Baadhi ya wanachama waliojiunga katika chama cha ADC na baadaye kujiondoa wamenieleza kuwa walishawishika sana baada ya kusikia viongozi wakiwaeleza masuala mengi ambayo yeye alikuwa pia akiyataja kama mipango ya muda mfupi na muda mrefu ya chama hicho. Lakini hadi leo wananieleza kuwa masuala muhimu ambayo walitarajia angeyafanyia kazi hakuyakamilisha. Lakini pia baadhi ya viongozi waliofanya naye kazi ndani ya CUF wanamtaja sana kwa sifa hii ambayo kiuongozi naichukulia kama udhaifu uliopitiliza.
Na mwisho, Hamad Rashid wakati mwingine haelewi mahali gani aongee jambo gani, hasa anapokuwa na machungu yanayosumbua akili yake. Akiwa katika Bunge Maalum la katiba aliwashangaza watu wengi pale alipotumia sehemu kubwa ya hotuba yake kumshambulia hasimu wake kisiasa, Maalim Seif Sharif Hamad, Katibu Mkuu wa CUF na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.
Kwa mtizamo wangu, Hamad Rashid alihamishia ugomvi wake na wa viongozi wake au na chama chake cha zamani kwenda katika bunge la kitaifa linalotunga katiba. Alipoteza muda mwingi sana kufanya mashambulizi kwa mtu ambaye hayumo bungeni na hawezi kumjibu. Watu wengi ambao tumekuwa tukimfahamu kiongozi huyu kwa busara na utulivu mkubwa, tuligutushwa sana na hali ile na inaweza kupelekea ikahitimishwa kuwa si mfano bora wa uongozi au wa mtu anayetajwa kuwa na sifa na vigezo vya kuweza kuwa Rais wa nchi.
NINI KINAWEZA KUMFANYA APITISHWE
Kama ADC itafikiria na hata kumpitisha Hamad Rashid kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sababu moja kubwa itakuwa ni kuhuisha ujenzi wa chama hicho kichanga. Ikumbukwe kuwa ADC ni chama kipya, hakina hata miaka minne katika ulingo wa kisiasa, kwa vyovyote vile kinahitaji mtu mwenye uelewa, uzoefu na uwezo kama wake.
Lakini jambo la pili linaweza kufanya apitishwe ni kwa sababu ya umaarufu. Pamoja na kwamba ni Mzanzibari, lakini Hamad Rashid ni kiongozi anayefahamika sana ndani ya Tanzania Bara na visiwani. Viongozi wengi wa Zanzibar hufanikiwa kuwa maarufu katika visiwa hivyo tu. Yeye ni mmoja wa wale waliovuka mipaka na nadhani chama hicho kipya kinahitaji kuwa na mgombea wa aina hii ili kiwavute wapiga kura.
Lakini jambo la tatu linaloweza kumvusha pia ni kwa sababu yeye ni mmoja wa watu waliotoa mchango mkubwa katika uanzishaji wa chama hicho. Na katika siasa za Afrika, watu wa aina hii hupewa uzito mkubwa pale ambapo hutokea wanataka nafasi ya uongozi.
Na mwisho, uzoefu wa kufanya kazi Tanzania Bara na Zanzibar kwa pamoja vinampa Hamad Rashid nafasi ya kipekee ya kuwa mgombea wa Urais wa chama hicho. Kwamba yeye ni Mzanzibari ambaye amefanya kazi Zanzibar muda mrefu lakini pia akifanya upande wa Bara. Ni mmoja wa viongozi wanaotoka Zanzibar huku wakifahamu vizuri sana masula ya Bara na hii ni faida muhimu kwa ADC.
NINI KINAWEZA KUMWANGUSHA KWENYE MCHUJO?
Moja ya masuala yatakayoweza kumkwamisha kwenye mchujo wa nafasi hii ni ikiwa chama chake (ADC) kitaamua kuweka mgombea kutoka Tanzania Bara ili aweze kupambana vilivyo na hata kuwa na uwezo wa kulinda kura nyingi zitakazopigwa kwa mkumbo wa U-bara na U-Zanzibari.
Tukumbuke kuwa wapiga kura walioko Tanzania Bara ni kwa mamilioni na chama chochote kile cha siasa kingependa kuvutia waliko wapiga kura wengi kwa sababu siasa zile za umoja wa kitaifa zimeanza kupotea na wazanzibari wameanza kupoteza uwezo na nguvu za kupata nafasi ya Urais wa Jamnhuri ya Muungano wa Tanzania, labda hadi siku “Nyerere mwingine” atakapozaliwa.
MIPANGO MINGINE IWAPO HATACHAGULIWA NA CHAMA CHAKE (PLAN B)
Kama Hamad Rashid hatapaendekezwa na chama chake kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, naamini moja kwa moja atakuwa mmoja wa wgombea Urais wa Zanzibar. Tayari natambua kuwa mwaka huu akiwa bungeni Dodoma (Bunge la Bajeti), aliutangazia umma kuwa ana mpango wa kugombea Urais wa Zanzibar na nadhani huu ni mpango wa kwanza kwake, wakati anastaafu siasa za Ubunge.
Lakini mpango wa pili unaoweza kuwa mezani kwa kiongozi huyu ni kuendelea na biashara. Hamad Rashid ni mfanyabiasha wa kadri na amekuwa hivyo katika kipindi kirefu sana. Kama hatogombea Urais wa Tanzania naona akijikita katika biashara na kufanikiwa sana.
HITIMISHO
Kwa sababu Hamad Rashid ni Mtanzania mwenye asili ya Zanzibar na anayetokea upande wa Zanzibar, tena kisiwani Pemba. Sioni akiwa na nafasi kubwa sana katika siasa za kitaifa ndani ya miaka mitano ijayo.
Shida ya siasa za Zanzibar ni kwamba kama wewe hauko CUF au CCM ni kama vile huna mahali pa kufanyia siasa, na nadhani hili ndilo linalomkuta. Wanasiasa wengi wakubwa wanaotoka Pemba au Unguja na waliohama CCM walifanikiwa ikiwa walikwenda CUF, na waliohama CUF walifanikiwa ikiwa walikwenda CCM, ni vigumu kabisa kufanya siasa Zanzibar nje ya CUF na CCM na jambo hili linamgusa moja kwa moja Hamad Rashid.
Anaweza kuamua kuja kufanya shughuli za siasa Tanzania Bara ambako nako navyoona hali ya mambo, ndani ya miaka michache ijayo Wazanzibari watakuwa na nafasi ndogo sana ya upenyo wa kisiasa maana hali ya “usisi” na “umimi” imeshakuwa kubwa mno na kila upande (Bara na Zanzibar) umeanza kumuona mwenzie kwa jicho kali.
Lakini, kwa sababu Hamad Rashid ni mwanasiasa wa siku nyingi na anajua njia nyingi za kupita, nawajibika kuweka akiba ya maneno na kumtakia kila la heri katika safari yake ngumu kisiasa, kiongozi huyu ambaye amewavutia vijana wengi sana wa Zanzibar na Tanzania bara, kujiunga katika siasa za kitaifa.

VYUO VIKUU 20 BORA AFRIKA - ORODHA YA MWAKA 2015

VYUO VIKUU 20 BORA AFRIKA - ORODHA YA MWAKA 2015
1 University of Cape Town - South Africa
2 University of Pretoria - South Africa
3 Universiteit Stellenbosch - South Africa
4 University of the Witwatersrand - South Africa
5 University of South Africa - South Africa
6 The American University in Cairo - Egypt
7 Cairo University - Egypt
8 Mansoura University - Egypt
9 Alexandria University - Egypt
10 UNIVERSITY OF DAR ES SALAAM - TANZANIA
11 University of KwaZulu-Natal - South Africa
12 Rhodes University - South Africa
13 Ain Shams University - Egypt
14 Assiut University - Egypt
15 University of the Western Cape - South Africa
16 Universit̩ Mohammed V РAgdal - Morocco
17 University of Johannesburg - South Africa
18 Université de Ouagadougou - Burkina Faso
19 UNIVERSITY OF NAIROBI - KENYA
20 University of Lagos - Nigeria

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR