Showing posts with label Pope Francis. Show all posts
Showing posts with label Pope Francis. Show all posts

Tuesday, June 24, 2014

Papa: anayehukumu wengine ni mnafiki, na hujiweka katika katika nafasi ya Mungu

Baba Mtakatifu Francisko ameonya dhidi ya tabia ya kupenda kuhukumu wengine bila kutafakari hali zetu wenyewe. Kupenda kujiona sisi tu safi na yule ni mdhambi. Lakini tukumbuke kipimo kilekile tunacho tumia kuhukumu wengine, ni hichohicho kitakacho tumika kutuhukumu... Anayehukumu ndugu yake, naye atahukumiwa kwa njia hiyo hiyo. Mungu ndiye pekee "hakimu". Na mshutumiwa anaweza daima hutetewa na Yesu. Yesu, Wakili Mkuu wa Kwanza, na Wakili wa pili ni Roho Mtakatifu. Papa Francisko amesema katika hotuba yake ya wakati wa Ibada ya Misa, asubuhi Jumatatu , katika Kanisa dogo la Mtakatifu Martha, ndani ya Vatican.

Papa Francisko ameonya dhidi ya kuwa watu wa kupenda kuhukumu wengine katika nafasi mbalimbali, kimaisha,au katika uwajibikaji au mamlaka akieleza kwamba jambo kuhukumu ni hatari kwa sababu licha ya kuuumiza wengine, pia, humgeukia mwenyewe na kuishia kuwa mwathirika wa ukosefu wa huruma kwa wengine. Hiki ndicho hutokea katika kuwahukumu wengine.
Papa Francisko alitoa onyo hili, mara baada ya kusoma kifungu cha Injili kuhusu kibanzi na boriti iliyoko katika jicho, akibainisha kwamba , ni wazi inaonyesha mtu anayependa kuhukumu wenzake kuwa anafanya makosa , na huonyesha udhaifu wa mtu wa kushindwa, maana binadamu hana haki ya kumhukumu mtu mwingine kiroho, hakimu ni Mungu peke yake . Kuhukumu wengine ni "unafiki", kama Yesu alivyowaambia kwa mara kadhaa walimu wa sheria, wakati wa matukio kadhaa kwa wakati ule. Na pia ni kwa sababu Papa alieleza, binadamu hutoa hukumu yake harakaharaka, wakati hukumu ya Mungu huchukua muda.


Na hivyo , kutokana na hili , kuhukumu wengine ni makosa , kwa maneno mepesi ni kwa sababu ni kuchukua nafasi isiyokuwa yako. Na si tu ni makosa lakini pia ni kumchanganya mtu. Ni kupagawa na nia kali za kutaka kujitakatifusha, kuonekana kama safi na wengine ni wakosaji , nia zinazowasha moto wa ndani ambazo haziachi nafasi ya utulivu, wa kujitafakari wenyewe. Lakini tunaambiwa kwanza toa boriti katika jicho laki ndipo utoe kibazi kilicho ndani ya ndugu yako.

Homilia ya Papa imesisitiza , mwenye uwezo wa kutoa hukumu ni Mungu peke, na kuongeza, kile kinacho onyesha tabia ya kumtegemea Yesu,ni mfano wake wa kuto hukumu wengne.
Yesu mbele ya Baba, kamwe hakuwatuhumu wengine.Kinyume aliwatetea! Anakuwa Mtetezi wa kwanza. Kisha anampeleka mtetezi wa pili, ambaye ni Roho Mtakatifu. . Yeye ni Wakili mbele ya Baba dhidi ya mashtaka, Papa ameeleza na kuhoji Na ni nani basi mshitaki? Na kutoa jibu la Biblia,kwamba Mshitaki anaitwa Ibilisi , shetani. Na hivyo Mwisho wa Dunia, Yesu atahukumu lakini wakati huo huo ni mwombezi na mtetezi ..

Hatimaye, Papa Francisko , alisema, anayehukumu, humwinga Mkuu wa ulimwengu huu,ibilisi ambaye daima ni nyuma ya watu, akitaka kuwashtaki kwa Baba. Lakini Bwana, atatupa neema ya kumwiga Yesu, wakili na mwanasheria wetu. Na si kuwaiga wengine, ambayo mwisho wao ni huangamiza

Papa ameasa, iwapo tunataka kutembea katika njia ya Yesu, tunapaswa kuwa mawakali watetezi wale wanaotuhumiwa mbele ya Baba. Kwa namna gani tunaweza kuwa watetezi wa wengine wanaoshutumiwa, je ni kuingilia kati mara ? Hapana ni kukaa kimya na kwenda kusali na kumtetea mbele ya Bwana kama Yesu alivyofanya msalabani. Kusali kwa ajili yake na si kuhukumu. Ni vibaya kuhukumu kwa sababu, pia utahukumiwa

Papa aliwataka wote waliokuwa wakimsikiliza kukumbuka hilo siku zote , pale inapokuja hamu ya kutaka kuhukumu wengine , na kusema mabaya ya wengine, kuyashihnda majaribu hayo kwa kusali na kuomba neema ya kusamehe wengine..

Wednesday, November 6, 2013

Mnaalikwa kwenye Karamu ya Bwana! Wakristo msiridhike kuwa katika orodha ya wageni waalikwa! Mnatakiwa kufanya makubwa zaidi!




Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, Jumanne, tarehe 5 Novemba 2013 anawaalika waamini kuhakikisha kwamba, wanasherehekea kikamilifu Karamu ya Bwana. Wakristo watambue kwamba, wanaalikwa na Mwenyezi Mungu kushiriki karamu hii wakiwa na dhamiri safi na nyofu.

Karamu ya Bwana ni sherehe inayobubujika furaha, matumaini na mapendo kutoka kwa Kristo; sherehe ambayo inawakumbatia wote pasi na ubaguzi kwani wao ni sehemu ya viungo vya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa, kila mtu ana wajibu na dhamana ya kutekeleza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa. Wakristo wajitambue kwamba, wao ni sehemu muhimu sana ya Kanisa la Kristo! Karamu hii ni mwaliko wa kujenga na kudumisha umoja miongoni mwa Wakristo, kila mwamini akijitahidi kujitakatifuza kwa nyenzo mbali mbali zinazotolewa na Mama Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, Kanisa linawakumbatia watakatifu na wadhambi; na kwamba, kila mmoja wao ana karama na zawadi ambayo amekirimiwa na Roho Mtakatifu; zawadi ambayo anapaswa kuifanyia kazi barabara kwa ajili ya mafao ya Kanisa. Kanisa linapaswa kuwakumbatia wote kwa kuanzia na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Inasikitisha kuona kwamba, kuna baadhi ya Wakristo wamepewa mwaliko na wako kwenye orodha ya waalikwa, lakini bado wanagoma kuhudhuria Sherehe ya Mwanakondoo wa Mungu kwa visingizio kibao! Wanashindwa kutambua kwamba, kuingia ndani ya Kanisa ni mwaliko na neema inayowataka waamini kujenga na kuimarisha Jumuiya ya Kikristo, kila mtu akitumia kikamilifu karama na vipaji vyake kwa ajili ya Kanisa na Jirani zake. Kristo anaendelea kuwaalika waamini kufanya hija inayowapeleka kwenye maisha ya uzima wa milele na kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye kiongozi mkuu wa safari hii ya maisha ya kiroho.

Baba Mtakatifu anasema, Yesu ni mwingi wa huruma na mapendo, hata kwa wale wanaoonesha shingo ngumu kwa mwaliko wake. Anaendelea kuwasubiri kwa saburi na mapendo makuu. Yesu anawapenda watu ambao ni wanyofu na wa kweli katika maisha yao: kwa maneno na matendo.

Inapendeza ikiwa kama Wakristo wote wataweza kushiriki katika Karamu ya Bwana, ili kuonja furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na wala wakristo wasiridhike kwamba, majina yao yameandikwa kwenye orodha ya waalikwa kwenye Karamu ya Bwana, bali wanatakiwa kushiriki bila kutoa visingizio!

Friday, November 1, 2013

Maadhimisho ya Siku ya Watakatifu wote na siku ya Marehemu wote

Papa afafanua kiini cha Maadhimisho ya Siku ya Watakatifu wote na siku ya Marehemu wote.



BabaMatakatifu Francisko akiendelea kutoa tafakari juu ya sala ya Nasadiki, kwa Jumatano hii, alilenga zaidi katika usharika na Watakatifu, kama Kateksimu ya Kanisa Katoliki inavyotukumbusha sisi kwamba, usharika huu ni kwa Mambo Matakatifu na kati ya watu Watakatifu (No. 948 ).

Papa alizama zaidi katika sehemu ya Pili ya kuw ana usharika na Marehemu Watakatifu , ukweli unaohitaji ufafanuzi zaidi katika imani yetu, akieleza pia kwamba, hutukumbusha pia kwamba, hatuko pweke, lakini kuna uwepo wa usharika wa maisha kwa wale wanaokuwa wa Kristu. Usharika mmoja unaoundwa na imani , katika ukweli wake, neno hili Watakatifu hurejea wale wanao mwamini Yesu Kristu kuwa ndiye Bwana wa Maisha na hivyo humwilishwa kwake Yeye ndani ya kanisa kupitia ubatizo. Na kwa namna hiyo , Wakristu wa kwanza waliitwa pia Watakatifu.

Papa aliendelea kufundisha , Usharika wa Watakatifu ni kina halisi cha maana ya Kanisa kwa sababu kama wakristu kupitia Ubatizo , tunafanywa kuwa washiriki wa maisha ya usharika mmoja na upendo wa Utatu Mtakatifu. Na hivyo sote tunaunganishwa mmoja kwa mwingine na kiungo cha ubatizo katika Mwili wa Kanisa. Na kupitia usharika huu wa kidugu, tunawekwa karibu zaidi na Mungu, na tukitakiwa kusaiidiana mmoja kwa mwingine kiroho.

Papa alieleza na kuirejea Injili Yohana ambayo inasema kwamba , kabla ya mateso yake, Yesu aliomba kwa Baba kwa ajili ya umoja kwa wanafunzi wake kwa maneno haya : “Naomba ili wote wawe kitu kimoja kama wewe, Baba , ulivyo ndani yangu , nami ndani yako. Naomba wawe kitu kimoja kusudi ulimwengu upate kuamini kwamba wewe ndiye uliyenituma "( 17:21). Kanisa , katika kweli yake kamili , ni usharika na Mungu , usharika wa upendo na Kristo na Baba katika Roho Mtakatifu shina la usharika huo. . Uhusiano huu baina ya Yesu na Baba ni dhamana kati ya Wakristo, iwapo pia sisi tumo ndani yake katika umoja huu, na tanuru la moto huu wa upendo katika Utatu Mtakatifu, basi tunaweza kweli kuwa na moyo na roho moja kati yetu kwa sababu upendo wa Mungu unauguza ubinafsi wetu , chuki zetu, utengano na miganyiko yetu ya ndani na nje.

Papa Francisko amesema, iwapo ushariki huu chanzo chake ni mzizi wa upendo ambao ni Mungu, basi pia kuna sababu za kufanya hima kutoa jibu landiyo katika muungano huu na Mungu, maisha ya ushirika wa udugu unaoongoza katika kuwa msharika na Mungu.

Hii ni sehemu ya pili ya usharika, ambayo Papa alitoa msisitizo zaidi, kuwataka watu wa Mungu,kupta uelewa mpana kwamba, imani yetu inahitaji msaada wa wengine , hasa katika nyakati ngumu. Alisema, tazama pia jinsi ilinavyokuwa vizuri kutoa msaada kwa mwingine katika maajabu haya ya imani! Papa alieleza kukemea mwelekea kukubatia tabia ya kutaka kujifungia binafsi, hata katika mazingira ya kidini, kiasi kwamba, inakuwa hata vigumu kwa wengine, hata kuomba msaada wa kiroho, kwa wale wenye uzoefu katika maisha haya ya Kikristu.

Papa alihimiza katika nyakati hizi ngumu ni muhimu kuwa imani kwa Mungu kupitia sala, na wakati huo huo, ni muhimu kupata ujasiri na unyenyekevu kuwa wazi kwa wengine. Papa amekumbusha ushirika wa watakatifu ni familia kubwa, ambapo vipengele vyote ni kusaidia na kusaidiwa yaani kusaidiana mmoja kwa mwingine. Kushirkiana na wengine katika parokia zetu, katika vyama , jumuiya, harakati na vikundi, kama sehemu ya maisha katika safari yetu ya imani, ni kutochoka kuomba msaada wa maombezi na faraja ya kiroho. Ni wakati wetu wa kusikiliza na kuwasaidia wale ambao hawaja jiunga nasi katika safari hii.

Papa alikamilisha Katekesi yake kwa kuchambua kipengele kingine cha usharika wa watakatifu, akisema kwamba, ushariki wa wakatifu huenda zaidi ya maisha ya dunia, inakwenda zaidi ya kifo kwa kuwa huduma milele. Usharika wa kiroho tunaopokea wakati wa Ubatizo hauvunjwi na kifo , lakini umeinuliwa na ufufuko wake Kristu, unao ipeleka roho katika mapito ya utimilifu wa maisha ya milele.

Papa aliendelea kubaini kwmba, kuna dhamana ya kina na isiyokuwa na mwisho kati ya wale ambao bado mahujaji katika dunia hii na wale ambao wamevuka kizingiti cha kifo na kuingia katika umilele. Wote hao huuundwa wakati wa ubatizo hapa duniani,na nafsi hutakatifushwa toharani na kufanywa wenye heri, kuingia katika makazi ya mbinguni ambako ni makazi ya familia moja kubwa. Ushirika huu kati ya nchi na mbinguni ni barabara ya maombezi , ambayo ni aina ya juu ya mshikamano, na pia ni msingi wa maadhimisho ya kiliturujia ya Watakatifu wote na Maadhimisho ya Marehemu wote kama itakavyokuwa siku chache zijazo.

Papa alimalizia kwa kumtaka kila mmoja alifurahie fumbo hili , na kumwomba Bwana neema zake , ili tuweze kuwa karibu zaidi naye na katika usharika na waamini wote, wake kwa waume ndani ya kanisa.
Wito wa Kuombea Iraki
Baada ya Katekesi, Papa akisalimia makundi mbalimbali, pia alilitaja kundi la mahujaji kutoa Iraki ambao walikuwa wakiwakilisha makundi mbalimbali ya kidini, toka yanayojionyesha kama ni utajiri wa Ukristu katika taifa la Iraki . Kundi hili liliongozwa na Kardinali Tauran Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya majadiliano na dini zingine. Papa alitoa wito kwa watu wote kukumbuka kuliombea taifa la Iraki ambalo kila kukicha hukumbana na majanga ya fujo na ghasi za kusitisha zinazofaywa na makundi mabalimbali. Tusali ili Iraki ipate kurejea katika njia ya majadiliano, maridhianao , amani, umoja na utulivu wa kudumu kitaifa.

Monday, October 28, 2013

Sala ya Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya Familia



Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa ajili ya Familia limekuwa ni tukio la imani kwani kabla ya Misa Takatifu, waamini wengi walipata nafasi ya kuungama ili kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani zao kwa kutambua umuhimu wa Sakramenti ya Upatanisho.

Mara baada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili, tarehe 27 Oktoba, 2013, Baba Mtakatifu Francisko amesali mbele ye Sanamu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, akiiendea kwa imani thabiti ili kutafakari umoja na upendo wa dhati, ili hatimaye, aweze kuzikabidhi Familia zote za Kikrito ambazo zinapaswa kuonja neema.

Familia Takatifu ni shule makini ya Neno la Mungu, Fadhila, hekima na nidhamu ya maisha ya kiroho. Baba Mtakatifu anaomba ili waamini waweze kuwa na jicho la kuona kazi ya Mungu katika uhalisia wa maisha yao ya kila siku. Familia Takatifu ni hifadhi aminifu ya Fumbo la Ukombozi.

Baba Mtakatifu anaomba fadhila ya ukimya, moyo wa sala katika familia ili ziweze kuwa kweli ni Kanisa dogo la nyumbani; daima wanafamilia watamani utakatifu pamoja na kuwasaidia kukabiliana na changamoto za maisha, kwa kusikilizana, kuelewana na kusameheana.

Familia Takatifu iwasaidie walimwengu kutambua na kuthamini utakatifu wa maisha na kwamba, Familia ni hazina ambayo haina mbadala. Kila familia ijitahidi kupokea na kuenzi amani kwa ajili ya watoto na wazee; wagonjwa na wapweke; maskini na wote wanaosukimizwa pembezoni mwa Jamii.

Saturday, August 3, 2013

Ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa Waislam wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Id El Fitri




Kwa Waislam wote duniani.
Ninayo furaha kubwa kuchukua fursa hii kuwasalimia wakati huu mnapoadhimisha Siku kuu ya Id El Fitri, inayofunga Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, uliotengwa kwa ajili ya kufunga, swala na sadaka.
Ni mapokeo ya siku nyingi kwamba, katika Siku kuu hii, Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini linawatumia ujumbe wa matashi mema, ukiambatana na mada kwa ajili ya tafakari ya pamoja. Mwaka huu, ambao ni mwaka wangu wa kwanza kama Papa, nimeamua kutia sahihi mimi mwenyewe na kuwatumieni, ndugu zangu wapendwa, kama alama ya heshima na urafiki kwa Waislam wote, lakini kwa namna ya pekee viongozi wa kidini.
Kama wengi wenu mnavyofahamu, Makardinali waliponichagua mimi kama Askofu wa Roma na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki, nilichagua jina la “Francisko” Mtakatifu maarufu aliyempenda Mungu na watu wote, kiasi hata cha kuwaita ndugu zake. Alipenda, akasaidia na kuwahudumia wahitaji, wagonjwa na maskini; ni mtu aliyetunza sana mazingira.
Ninafahamu kwamba, familia na mwelekeo wa kijamii unapata nafasi ya pekee kwa Waislam katika kipindi hiki, ni vyema kutambua kwamba, kuna uwiano wa mambo haya hata katika imani ya Kikristo na utekelezaji wake.
Mwaka huu, mada ambayo ninapenda kutafakari pamoja nanyi bila kuwasahau wote watakaobahatika kuusoma ujumbe huu ni ile inayowahusu Waislam na Wakristo: Kuhamasisha hali ya kuheshimiana kwa njia ya elimu.
Mada ya mwaka huu inapania kufafanua umuhimu wa elimu kadiri tunavyofahamiana, ili kujenga msingi wa kuheshimiana. “Kuheshimiana” maana yake ni mwelekeo wa upendo kwa watu tunaowathamini na kuwajali. Huu ni mchakato wa “pande mbili za shilingi” unaozihusisha pande zote.
Tunachoalikwa kuheshimu kwa kila mtu kwanza kabisa ni maisha yake, mwili wake mzima, utu na haki ambatanishi zinazotokana na utu huo, heshima, mali yake, kabila, utambulisho wake wa kitamaduni, mawazo na msimamo wake wa kisiasa. Tunaalikwa kufikiri, kuzungumza na kuandika kwakuwaheshimu wengine, si tu wakati wanapokuwepo, bali ni kwa daima na kwa wakati wote, kwa kuachana na shutuma au kuwachafulia wengine sifa yao njema. Familia, shule na mafundisho ya dini pamoja na njia za mawasiliano ya kijamii zina dhamana ya kuhakikisha kwamba, lengo hili linafikiwa.
Nikiangalia dhana ya kuheshimiana katika uhusiano wa majadiliano ya kidini, hasa zaidi kati ya Waislam na Wakristo, tunaalikwa kuheshimu dini ya wengine, mafundisho yao, vielelezo vya imani na tunu msingi za maisha ya kiroho. Viongozi wa kidini waheshimiwe pamoja na nyumba za ibada. Inatia uchungu kuona viongozi au nyumba za ibada zinashambuliwa.
Ni wazi kwamba, tunapoheshimu dini ya jirani zetu au pale tunapowatakia wengine matashi mema katika Maadhimisho ya Siku kuu zao za kidini, tunapania kushiriki furaha yao, bila hata ya kufanya rejea kwenye maudhui ya imani yao.
Kuhusiana na elimu kwa vijana wa Kiislam na Kikristo, ni wajibu wetu kuwalea vijana ili waweze kufikiri na kuzungumza kwa heshima kuhusu dini na wafuasi wa dini nyingine, pamoja na kujizuia kuzibeza au kukashifu imani na ibada zao.
Tunafahamu kwamba, kuheshimiana ni msingi wa kila mahusiano, lakini zaidi miongoni mwa waamini wanaoungama imani zao. Kwa njia hii, ukweli na urafiki wa kudumu unaweza kukua.
Nilipokutana na Wanadiplomasia wanaowakilisha nchi zao mjini Vatican hapo tarehe 22 Machi 2013, nilisema, “Haiwezekani kuanzisha uhusiano mwema na Mwenyezi Mungu, wakati unawabeza watu wengine. Kwa hiyo ni jambo la muhimu kuzidisha majadiliano miongoni mwa dini mbali mbali, lakini zaidi na Waamini wa dini ya Kiislam. Katika Ibada ya Misa Takatifu, mwanzo wa utume wangu, nilifurahi kuona viongozi wa Serikali na wa Kidini kutoka katika Ulimwengu wa Waislam.”
Kwa maneno haya, ninapenda kusisitizia kwa mara nyingine tena umuhimu wa majadiliano na ushirikiano miongoni mwa waamini, lakini zaidi kati ya Wakristo na Waislam; jambo linalopaswa kuendelezwa.
Ni matumaini yangu kwamba Wakristo na Waislam watajitahidi kuwa ni vyombo vya kukuza hali ya kuheshimiana na urafiki, hasa kwa njia ya elimu.
Hatimaye, ninapenda kuwatumia sala na matashi mema, ili maisha yenu yaweze kumtukuza Mwenyezi Mungu pamoja na kuwakirimia furaha wale wanaowazunguka. Ninawatakieni Siku kuu Njema ninyi nyote!
Francisko.
Imetolewa Vatican,

Tuesday, June 18, 2013

Papa atoa wito: Semeni ndiyo kwa maisha na hapana kwa Kifo


Papa Fransisko ametoa wito kwa watu wote kuyatetea maisha na hapana kwa kifo. Kusema ndiyo kwa maisha na kukataa kila kitendo kinachotaka kukatisha uhai , kusema hapa kubwa kwa kifo. Papa alitoa wito huu wakati wa hotuba yake siku ya Jumapili asubuhi, ambamo Mama Kanisa aliadhimisha SIKu ya Injili ya Maisha “ Evangelium Vitae” .

Katika homili yake aliyoitoa mbele ya umati wa watu wapatao 200,000 waliofurika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro , kuhudhuria Ibada ya Misa iliyoongozwa na Papa, na pia kwa ajili ya sala Ya Malaika wa Bwana, ibada na sala zilizofanyika katika mtazamo wa maadhimisho Mwaka wa Imani, siku ililega zaidi majitoleo ya Injili ya Maisha.

Katika homilia yake , Papa Francis, alitafakari Maandiko Matakatifu yanavyotuambia mara kwa mara, jinsi Mungu Mmoja Hai, ndiye mwenye kutoa maisha.

Hata hivyo, alisema kwamba "mara nyingi, watu hawachagui maisha, hawaikubali Injili ya Maisha bali hujiachia wenyewe kuongozwa na itikadi na njia yapotofu katika kufikiri, zenye kuwekea maisha kibambaza, njia zisizo heshimu maisha, kwa sababu wamekubali kuongozwa na nguvu za ubinafsi katika utafutaji wa maslahi faida, mamlaka na kujijifurahisha , na si kwa ajili ya upendo kwa wengine , au kujali manufaa ya wengine.

Baba Mtakatifu aliendelea kusema kuwa, watu wana ndoto za kujenga upya "Mnara wa Babeli", mji wa mtu asiyekuwa na Mungu. Wanaamini kwamba kumkataa Mungu, kuukataa ujumbe wa Kristo na Injili ya Maisha, huwaongoza kwa namna fulani katika furaha, kuwa na uhuru kamili wa kutimiza malengo yao ya kibinadamu. Na kama Kama matokeo yake , Papa aliendelea, Mungu aliye hai huondolewa na badala yake huwekwa miungu mbadala mfululizo ya kibinadamu ambayo hulewesha mtu katika uhuru bandia , ambao mwisho wake hujenga aina mpya za mfumo wa utumwa na kifo.

Papa alimalizia homilia yake na wito kwa waamini, kuyaonamadhara hayo ni hivyo waseme Ndiyo kwa Mungu ambaye ni Upendo. Ndiyo kwa Maisha ya kushikamana na Mungu ndiye uhuru wa kweli na hamfadhaishi mtu.
Mara baada ya Ibada ya misa Takatifu, Papa aliongoza sala ya Malaika wa Bwana. Katika hotuba yake fupi, Papa alielekeza mawazo yake katika mifano ya watu walioyatetea maisha kikamilifu, akiangalisha katika tukio la Siku ya Jumamosi ambamo Mama Kanisa alimtagaza kuwa Mwenye Heri , baba wa watoto saba wa Capri Italy, aliyeuawa katika kambi za msongamano za Nazi mwaka 1944, ambaye aliyaokoa maisha mengi katika kambi hiyo , kabla ya kupoteza yake mwenyewe.

Papa pia aliitumia nafasi hiyo kusalimia washiriki wa Mkutano wa hadhara wa wanachama wa Harley-Davidson, kwa ajili ya kutumia kwa miaka 110, tangu kutengenezwa kwa pikipiki, yenye nembo hiyo ya Harley Davidson, ambayo inajulikana kuwa aina ya kipekee na mashuhuri Marekani. Kwa ajili ya sherehe hii zaidi ya wapanda pikipiki 100,000, walikusanyika mjini Roma mwishoni mwa wiki hii. Kati yao 1400 wakiwa na pikipiki zao , walibarikiwa na Papa wakati huo wa sala ya Malaika wa Bwana.




Tuesday, May 21, 2013

Papa azindua katika Smartphone-habari za Fides

Papa azindua katika Smartphone-habari za Fides



Shirika la habari za kimissionari la Fides, limetangaza kwamba, habari zake zitapatikana katika lugha nane, kupitia mpango wa smartphones, unayoitwa "Missio", ambao unaopatikana bil malipo yaani bure.
Huduma hii ilizinduliwa na Papa Fransisko wakati alipokutana na Wakurugenzi wa Mashirika ya Kipapa ya Kitume ya Kitaifa ya Missioni na pamoja na wafanyakazi wa Fides, Ijumaa iliyopita , Mei 17 mjini Vatican.
Papa Francesco ilizindua utoaji wa habari huo kwa kubofya juu ya iPad, kama alivyombwa na Padre Andrew Small, OMI, Mkurugenzi wa Kitaifa wa Mashirika ya Mashirika ya Kipapa ya Misioni nchini Marekani.
Ukurasa huu wa Utume wa uinjilishaji , utakuwa unatoa habari za Kanisa zilizotolewa kupitia tovuto ya habari za Vatican "news.va", pia kuna picha, sinema na homilia za Papa, habari ya Kanisa katika ulimwengu na zitakuwa zikitolewa katika lugha nane.
Padre Small katika uzinduzi huo alimwambia Baba Mtakatifu,kwamba wanalenga kuiweka Injili, ndani ya mfuko wa kila kijana ulimwenguni ,maneno yaliyomgusa Papa Fransisko wakati akibofya kifungo kilichoandikwa juu yake maneno “sisi ni wainjilishaji”.
Katika siku yake ya kwanza ya kuzinduliwa kwa ukurasa huu, jumla ya watu 1,140 wa kutoka nchi 27 tofauti, waliutembelea ukurasa huo. Padre Small anasema lengo letu ni kuwasaidia watu kuiona dunia kupitia macho ya imani". Ukurasa huu unapatikana katika iTunes App na Google Play , ambamo ujumbe wa uinjlishaji, unatolewa katika lugha nane: Kiingereza, Kihispania, Kiitaliano, Kijerumani, Kifaransa, Kireno, Kichina na Kiarabu.Karibuni nyote.

Imani katika sala, unyenyekevu, na moyo wa ushujaa hutenda miujiza

Imani katika sala, unyenyekevu, na moyo wa ushujaa hutenda miujiza



Sala ujasiri nyenyekevu na uthabiti, hufanikisha miujiza: Papa alieleza hili, mapema Jumatatu wakati akiongoza Ibada ya Misa, katika Kanisa dogo la Mtakatifu Marta la mjini Vatican. Ibada iliyohudhuriwa na wafanyakazi mbali mbali ilikuwa ni Homilia ya Papa kwa wafanyakazi hao, ilirejea Liturujia ya Neno la siku, kifungu cha Injili ambamo wafuasi wa Yesu walishindwa kumponya kijana mdogo mgonjwa, na Yesu aliwajibu kwamba wameshindwa kumponya kijana huyo kwa sababu wana imani haba. Baba wa Kijana huyo kwa imani thabiti, aliomba msaada kwa Yesu. Na Yesu anawaambia kila kitu kinawezekana kwa anayeamini.
Papa Francesco alieleza, mara nyingi wapo wanaopenda kuwa wafuasi wa Yesu, lakini hawapendi kuhatarisha mengine wanaoyoyaamini na hivyo imani yao kwa Kristu inakuwa ni imani nusunusu, hawana imani nae kikamilifu. Papa alieleza na kuhoji kwa nini hali hi ya kutosadiki kikamilifui? Na alitoa jibu kwamba, wao wana amini kwamba, ni moyo wenyewe usiotaka kujifunua wazi, moyo unabaki umefungwa , lakini katika ukweli wake moyo huo unaotamani kuwa na imani thabiti.

Hivyo basi, binadamu anaushinikiza moyo kutojifunua na wala kujiweka chini ya maongozi ya Yesu, kama ilivyokuwa wakati ule, wanafunzi wa Yesu walimwuliza kwa nini, hawakuweza kumponya kijana, na Bwana aliwajibu kwamba aina mapepo yaliyomshambulia kijana huyo, hayawezi kutolewa nje na jambo lolote , isipokuwa kwa sala tu.
Papa alieleza na kusema, ingawa tunamtolea sala Bwana,ndani mwetu tuna kigugumizi cha imani. Hatuna imani thabiti na yule tunayemtolea maombi yetu lakini twayatolea maombi hayo kama majaribio au mazoea ya kusali. Ili Bwana aweze kuyaitikia maombi yetu, twapaswa kusadiki kwamba kile tunachomwomba Bwana atakifanikisha. Na hii ni kuwa na imani thabiti katika nguvu ya sala, ni kusadiki kw unyenyekevu kwamba, Yesu ni nguvu na anaweza kufanya muujiza.
Kuomba muujiza wa uponyaji , au kuomba mabadiliko katika mahusiano ni lazima kuambatane na sala thabiti inayotuhusisha sisi sote. Papa Francisko alieeleza na kutolea mfano wa tukio hilo lilitokea huko Argentina, ambako : mtoto wa miaka 7 aliugua na madaktari kutoa masaa machache ya maisha. Baba yake, fundi umeme, mtu wa imani, akiwa kama amepagawa na habari hii ya maisha ya mtoto wake kufika ukingoni, alipanda basi na kwenda katiak madhabahu ya Mama Bikira Maria ya Lulijan, umbali wa 70 km mbali, ambako alisali na kumlilia Mungu ayaokoe maisha ya mwanae na Mungu alisikia sala yake na aliporejea nyumbani alimkuta mtoto wake akiwa amepona. :

Papa alihitimisha homilia yake akisema tunahitaji kuomba kwa moyo wa imani na ushujaa zaidi kwamba Mungu anaweza kila jambo. Hakuna anayeweza kusema ni peke yake ni jasiri wa maombi, bali kila mmoja ni jasiri, kinachotakiwa ni kuwa na Imani kwa Bwana. Papa alieleza na kuwataka wote watoleee sala zao kwa imani thabiti kwa ajili ya watu wengi ambao wanakabiliwa katika vita, wakimbizi wote na wote wnaokabiliwa na hali ngumu za maisha zilizo nje ya uwezo wao akisemam twapaswa kusema, Bwana, naamini na msaada wangu utatoka kwako leo hii. .

Friday, March 15, 2013

speech ya Pope

Wasifu wa Baba Mtakatifu Francis!



Baba Mtakatifu Francis ni Myesuiti wa kwanza kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni Papa wa kwanza katika historia ya Kanisa kutoka nje ya Bara la Ulaya na Papa wa kwanza katika historia ya Kanisa kutoka katika nchi za Amerika ya Kusini, nchi ambazo kwa sasa zina idadi kubwa ya waamini wa Kanisa Katoliki. Kwa mara ya kwanza Jina la Mtakatifu Francis linatumiwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Lakini ikumbukwe kwamba, kuna watakatifu wanne wenye majina ya Francis. Hawa ni akina Mtakatifu Francis wa Assisi, Msimamizi wa Italia; Mtakatifu Francis wa Sale, Mwalimu wa Kanisa na Msimamizi wa Waandishi wa Habari; Mtakatifu Francis Xsaveri, Myesuit na Msimamizi wa Wamissionari pamoja na Mtakatifu Francis wa Paulo, Mkaa pweke na mwanzilishi wa Shirika la Ndugu wadogo wa Calabria.

Kardinali Jorge Mario Bergoglio, SJ, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires, Argentina, alizaliwa tarehe 17 Desemba 1936 mjini Buenos Aires. Yeye ni mtoto wa Mzee Mario na Mama Regina Sivori, waliobahatika kupata watoto watano. Katika ujana wake, alisoma na kufuzu kama mtaalam wa kemia, baadaye akaacha kazi hii na kujiunga Seminarini huko Villa Devoto.

Tarehe 11 Machi 1958 alijiunga na malezi ya Kinovisi katika Shirika la Wayesuit akaendelea pia na masomo dunia nchini Cile na kunako mwaka 1963 alirejea tena Buenos Aires na kujipatia shahada ya uzamili kutoka katika Kitivo cha Falsafa, Chuo Kikuu cha San Josè huko San Miguel.

Kati ya mwaka 1964 na mwaka 1965 alikuwa ni Jaalim wa Fasihi Andishi na Saikolojia katika Chuo cha Bikira Maria wa Santa Fe. Kunako mwaka 1966 akafundisha masomo haya kwenye Chuo Kikuu cha Salvatore cha Buenos Aires. Kuanzia mwaka 1967 hadi mwaka 1970, alijiendeleza kwa masomo ya Taalimungu katika Chuo Kikuu cha San Josè kilichoko San Miguel na kujipatia shahada ya uzamili.

Tarehe 13 Desemba 1969 akapewa daraja takatifu la Upadre. Kati ya mwaka 1970 hadi mwaka 1971 alikamilisha hatua ya tatu ya majiundo yake kama Myesuit huko Hispania na tarehe 22 Aprili 1973 akaweka nadhiri za daima. Kati ya mwaka 1972 hadi mwaka 1973 alikuwa ni mlezi wa Wanovisi, Jaalim, Mshauri na Gombera wa Chuo cha Massimo. Tarehe 31 Julai 1973 akateuliwa kuwa Mkuu wa Jimbo la Argentina kwa upande wa Shirika, utume ambao aliutekeleza kwa muda wa miaka 6. Kati ya Mwaka 1980 hadi mwaka 1986, alikuwa ni Gombera wa Chuo cha Massimo na Paroko wa Parokia ya Patriaki San Josè, Jimboni San Miguel.

Kunako mwaka 1986 alikwenda nchini Ujerumani kumalizia masomo yake katika Shahada ya Uzamivu na wakuu wake wa Shirika wakampatia jukumu la kuwa mkuu wa malezi ya kiroho na muungamishi katika Chuo cha Salvatore.

Tarehe 20 Mei 1992 Papa Yohane Paulo II akamteuwa kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Buenos Aires, akawekwa wakfu kama Askofu tarehe 27 Juni 1992. Tarehe 3 Juni 1997 akateuliwa kuwa Askofu mwandamizi wa Jimbo kuu la Buenos Aires na tarehe 28 Februari 1998 akasimikwa kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires baada ya kifo cha Kardinali Antonio Quarracino na hivyo kuwa pia ni Mkuu wa Kanisa Katoliki Argentina.

Mwenyeheri Yohane Paulo II akamteuwa na kumsimika kuwa Kardinali kunako tarehe 21 februari 2001. Ameshiriki katika Sinodi ya Maaskofu iliyofanyika kunako mwaka 2001. Akashiriki pia kwenye mkutano wa Makardinali wakati wa uchaguzi wa Papa kati ya tarehe 18 na 19 Aprili 2005. Alikuwa ni mjumbe wa Halmashauri ya Sinodi ya kumi na moja ya Maaskofu kuanzia tarehe 2 hadi 23 Oktoba 2005.

Mjini Vatican alikuwa ni mjumbe wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa, Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri, Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Tume ya Kipapa ya Amerika ya Kusini, Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri na Mjumbe wa Sekretarieti ya Sinodi.

Nchini Argentina alikuwa ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Argentina.
Rais wa Tume ya Baraza la Maaskofu kwa ajili ya Chuo Kikuu cha Kipapa cha Argentina. Alikuwa ni mratibu mkuu wa Mahakama ya Kanisa; Mratibu wa Mahakama ya Jimbo kuu la Buonos Aires. Tangu mwaka 2005 hadi 2011 alikuwa ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina.
Ni mwandishi wa Vitabu vifuatavyo:
    1982: Meditaciones para religiosos
    1986: Reflexiones sobre la vida apostólica
    1992: Reflexiones de esperanza
    1998: Diálogos entre Juan Pablo II y Fidel Castro
    2003: Educar: exigencia y pasión
    2004: Ponerse la patria al hombro
    2005: La nación por construir
    2006: Corrupción y pecado
    2006: Sobre la acusación de sí mismo
    2007: El verdadero poder es el servicio

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR