Friday, October 16, 2015

Lowassa atuma salamu za rambirambi kifo cha Filikunjombe

 Lowassa atuma salamu za rambirambi kifo cha Filikunjombe
Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA), Edward Lowassa ametuma salamu za rambirambi kwa chama cha Mapinduzi(CCM) na familia ya aliyekuwa mbunge/mgombea wa jimbo la Ludewa Deo Filikunjombe aliyefariki pamoja na watu wengine watatu katika ajali ya Helikopta iliyotokea jana jioni maeneo ya mbuga ya Selous mkoani Morogoro.
Helikopta hiyo iliyokuwa inaongozwa na Kapt.William Silaa(marehemu) ilidaiwa kupata hitilafu na baadae kupoteza mawasiliano jana jioni ilipokuwa safarini kutoka Dar es salaam kuelekea Njombe.
Helikopta hiyo ilianguka kwenye mbuga ya Selous na kupelekea vifo vya watu wote wanne waliokuwemo.
“Filikonjombe alikuwa Mbunge mahiri aliyesimama imara kutetea maslahi ya wananchi wa jimbo lake la Ludewa na watanzania kwa ujumla,” amesema Lowassa.
“Alikuwa mwiba kwa serikali ya Chama chake CCM kutetea maslahi ya nchi, mfano ni katika kashfa ya Escrow ambapo alikuwa Makamu Mwenyekiti wa kamati iliyochunguza kashfa hiyo.”
“Mwenyezimungu awape moyo wa subira, familia, jamaa, marafiki na wananchi wa Ludewa, katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na mpendwa wao,” amesema Lowassa.
Ni pigo lingine kubwa ambalo katika kipindi kifupi Taifa limepata, huku bado likiwa na kidonda cha kuondokewa na wanasiasa wengine mahiri,Mchungaji Christopher Mtikila, Celina Kombani, Dr Abdallah Kigoda na Dr Emanuel Makaidi aliyefariki jana
Kwa mujibu wa Zitto Kabwe, ambaye ndiye msimamizi wa mazishi ya Filikunjombe, amesema miili ya marehemu wote wanne imehifadhiwa katika Hospitali ya jeshi Lugalo kwa ajili ya kufanyiwa utambuzi na madaktari kutokana na miili hiyo kuwa katika hali mbaya ya kuungua.
Baada ya utambuzi huo, taratibu za mazishi zitaendelea.

Deo Filikunjombe afariki dunia kwenye ajali ya Chopa

 Tanzia : Deo Filikunjombe afariki dunia kwenye ajali ya Chopa
Aliyekuwa mbunge wa jimbo la Ludewa, Deo Filikunjombe ambaye alikuwa anatetea nafasi hiyo kupitia chama cha Mapinduzi(CCM), amefariki kwenye ajali ya helikopta iliyotokea jana usiku ndani ya Pori la Akiba la Selous lililopo eneo la Kilombero mkoani Morogoro. Filikunjombe ni mmoja wa abiria wanne waliokuwa ndani ya chopa hiyo ambao wamethibitishwa kupoteza maisha. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Jerry Silaa,Meya wa Manispaa ya Ilala anayemaliza muda wake, Capt.William Silaa baba mzazi wa Jerry ndiye aliyekuwa rubani wa chopa hiyo ambaye naye amepoteza maisha. “Kwa masikitiko makubwa nimepokea taarifa rasmi kutoka kwa timu ya uokoaji imefanikiwa kufika eneo la ajali na kukuta abiria wote na rubani wamepoteza maisha,” ilisomeka sehemu ya taarifa ya Jerry Silaa. “Nimepoteza Baba na rubani mzuri wa nchi yetu Capt.William Silaa,nimepoteza rafiki na kiongozi wangu Mhe.Deo Filikunjombe. Nawapa pole wote waliopoteza ndugu zao. Nawaombea marehemu mapumziko ya Amani.” “Nawashukuru wote walioshirikiana na familia kusaidia uokozi,” . “Namshukuru Mhe.Rais Jakaya M Kikwete, Dr.John Pombe Magufuli, IGP Ernest Mangu, Katibu Mkuu MU Dr.Meru, Kampuni ya Everest Aviation ,Wabunge, MaDC, Maafisa wa TCAA na wote walioshiriki kuwatafuta wahanga wa tukio hili,” ilimaliza sehemu ya Taarifa ya Silaa Wakati Taifa bado likiwa limeshikwa na butwaa kutokana na vifo vya aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara Dr Abdallah Kigoda, aliyezikwa jana na siku hiyohiyo kutokea kifo cha Dr Emanuel Makaidi, Mwenyekiti wa NLD na mgombea ubunge jimbo la Masasi, leo tena Taifa linaamka na kushuhudia kumpoteza kijana shupavu aliyekuwa miongozi mwa wabunge mahiri kuwahi kutokea ndani ya chama cha Mapinduzi, Deo Filikunjombe. Ni misiba..misiba..misiba, hakika uchaguzi wa mwaka huu unatengeneza historia ya aina yake na ya kuhuzunisha. Filikunjombe anakuwa mgombea ubunge wa sita kufariki ndani ya kipindi kisichozidi majuma sita. Mungu ailaze roho yake mahali pema, AMEN

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR