Showing posts with label NDOA: MAHUSIANO KABLA YA NDOA. Show all posts
Showing posts with label NDOA: MAHUSIANO KABLA YA NDOA. Show all posts

Wednesday, September 17, 2014

MAHUSIANO KABLA YA NDOA

Katika ulimwengu, mahusiano ya karibu ya kimwili kabla na nje ya ndoa yanakubalika, na hata kushabikiwa. Vipindi vya uchumba vinahesabika kama nyakati za wahusika hao wawili kuona kama ‘wanafaana’. Hili mara nyingi linawapelekea katika kuwa na mahusiano ya karibu ya kimwili.
Inasikitisha kwamba katika makanisa mengi vijana wanauiga mtindo huu huu, na wale walio katika nafasi za mamlaka – uongozi wa kanisa, wazazi, nk., hawashughuliki na hili suala kwaumakiniunaohitajika.Vijanawanaachiwa kujiamulia wenyewe mipaka katika hili suala nyeti, badala ya kupewa miongozo ya Kibiblia iliyo wazi.
Hebu tuwe wazi tokea mwanzo ya kwamba Mungu hachanganyikani; Neno lake halijaficha jambo. Ndani mwake, tunaona maono na mpango wake vilivyo dhahiri, kwa watu wake na Kanisa lake. Ni wazi kwamba hataki tujichanganye na ulimwengu na njia zake. Na wala Mungu hataki sheria na kuhukumiana Kanisani mwake, ambavyo havina nguvu yoyote ya kumbadilisha mtu. Anachotaka ni Wakristo wote wahakikishwe na Roho Mtakatifu kuhusu dhambi kupitia Injili ya Yesu Kristo ambayo inaweka mpaka ulio wazi na kutuonyesha tunapaswa tusimame juu ya msingi upi. Hii ndiyo maana ninaamini tunapaswa kurejea kwenye msingi – Neno la Mungu – ili tuone anasemaje juu ya hili suala.
MIILI YETU NI VIUNGO VYA KRISTO
Hebu tuangalie Mungu anavyoiona ndoa na mahusiano nje ya ndoa, na tutaona ya kwamba uhusiano wowote wa kimwili nje ya ndoa, uwe wa aina yo yote ile, unahesabika kuwa ni dhambi machoni pa Mungu. Si suala la ‘Tuweke wapi mipaka?’ kwa sababu tukijaribu kuweka mipaka ya aina yoyote, tutaivuka tu. Ni kama lile tangazo la breki za magari lisemavyo, “Usianzishe jambo ambalo hutaweza kulizuilia!”

1 Wakorintho 6:15 inasema: “Je, hamjui ya kuwa miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo vya kahaba? Hasha!” Kwa hivyo, si roho zetu tu zilizounganika na Kristo; nafsi yetu yote ni mmoja naye. Mistari ya 16 – 17 inasema, “Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, ‘Wale wawili watakuwamwilimmoja.’Lakiniyeyealiyeungwa na Bwana ni roho moja naye.”
Paulo hapa anasema waziwazi ya kwamba ni lile tendo la ndoa linalowaunga watu kuwa mwili mmoja, na hili linapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Katu hatupaswi kusahau ya kuwa roho zetu, nafsi zetu na miili yetu imeungwa pamoja na Kristo. Siku hizi Wakristo wengi wanafanya wanavyopenda na miili yao, pasipo kutambua madhara ya rohoni yanayotokana na matendo yao. Kwenye kifungu hiki Paulo anaweka utofauti kati ya dhambi ya mwili na dhambi nyingine; katika zinaa unatenda dhambi dhidi ya mwili wako kwa sababu unafanyika kuwa mmoja na yule mnayeunganika naye kimwili. Uzinzi ni uhusiano wowote wa kimwili nje ya ndoa. Uongo, wizi, hasira, nk. ni tofauti; haya ni matunda ya tamaa zetu za kimwili.
Ikiwa Mungu aliamua kuweka utofauti kati ya dhambi katika miili yetu na dhambi nyingine, tunapaswa kuwa makini sana, na kuufahamu moyo wake katika hili suala. Msitari wa 18 unasema, “Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake; ila yeye afanyaye zinaa hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe.” Hatupaswi kusahau ya kuwa miili yetu pamoja na roho zetu vimeungwa na Kristo, na tunapotenda zinaa ni jambo zito sana machoni pa Mungu. Mistari ya 19-20 inatukumbusha ya kuwa mwili wetu ni hekalu la Roho Mtakatifu, na tunahimizwa, “mtukuzeni Mungu katika miili yenu.”
MWILI UNAPASWA KUSULUBIWA
Katika Wagalatia 5:24-25, Paulo anasema, “Na hao walio wa Kristo wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.” Kila Mkristo ana uelewa fulani wa maana ya haya Maandiko. Lakini kwa wale wanaotamani kutembea rohoni, na wako tayari kuoa au kuolewa, yana maana zaidi maishani mwao.

Tumeitwa kuisulubisha miili yetu na tamaa zake. Hii ndio maana tunahitajika kuusikia ujumbe wa Msalaba kila wakati kwa sababu unatukumbusha kujikana nafsi zetu na kuyapoteza maisha. Hakuna nafasi ya kudanganyana, wala kujaribisha mambo… Sisi ni watu waliochaguliwa ambao miili yetu ni mali ya Bwana Yesu Kristo.
Iweje, basi, tuwaze ya kuwa ni sahihi kwa watu wawili waliochumbiana rasmi au vinginevyo, kufanya mambo wanayoruhusiwa kufanya tu mume na mke, eti kwa kuwa wamefikia uamuzi wa kuwa wenza? Uamuzi wa watu wawili wa kuoana huko mbeleni unapaswa umaanishe ya kwamba wataheshiminiana kwa utimilifu mbele za Bwana. Hadi siku ya kuoana, Bwana anawataka waishi maisha safi na matakatifu.
Vijana, sikilizeni… isipokuwa una uhakika moyoni mwako ya kuwa uhusiano umeanzishwa na Mungu, usithubutu kuuingia. Ukitaka kuufahamu mpango wake, na mtu aliyekuandalia kuwa mwenzi wako, fahamu ya kuwa atakufunulia.
Mkishafahamu ya kuwa ni mpango wa Mungu muoane, na ikiwa mnafahamu maisha ya utakatifu mnayopaswa kuishi kabla ya harusi, hakuna hatari. Mnaweza mkachumbiana na kutiana moyo katika kuheshimiana, kwa sababu mmehakikishiwa mioyoni mwenu ya kuwa mnapaswa kuishi maisha matakatifu mbele za Bwana hadi mtakapooana. Utakuwa na kicho kitakatifu cha uwepo wa Mungu katika maisha ya mwenzi wako na kufanyika kielelezo kwa wengine.
Ndio maana unapaswa uthibitike katika kile Mungu anachosema, ili pasiwepo na kubahatisha. Je, kuna mahusiano ya aina yoyote ya kimwili kabla ya ndoa yanayokubalika? Hasha! Neno la Mungu liko wazi sana juu ya hili suala.
MANUKATO YA UHUSIANO SAFI NA MTAKATIFU
Labda tayari uko katika uhusiano wa kimwili nje au kabla ya ndoa, na Bwana anakunenea ya kwamba si sahihi. Ushauri wangu ni kwamba utubu na ufanye uamuzi imara wa kuacha mahusiano yote ya kimwili mara moja; na usigeuke nyuma. Si jambo ambalo linafanyika hatua kwa hatua, wala si jambo la kuchukulia kwa wepesi. Neema ya Mungu ipo kukusaidia. Na ikiwa ninyi wawili mnafahamu mioyoni mwenu ya kuwa mmeandaliwa kuoana, basi jitunzeni hadi siku hiyo, mheshimiane kama vile ndugu wa kiume anavyomheshimu ndugu wa kike kanisani, na katika kufanya hivyo muishi maisha matakatifu na safi. Injili ya Msalaba wa Yesu Kristo inaleta jawabu kwa, na kuchora msitari ulio wazi katika kila jambo tunalokabiliana nalo maishani mwetu. Inatusaidia kuenenda katika uhakikisho, na kwa maana hiyo tunatembea katika ushindi. Wakristo wa kila rika, walio kwenye ndoa na ambao wako bado, wanahitajika wasikilize kwa umakini kile Mungu anachosema katika Neno lake ili waweze kuishi maisha matakatifu na kufanyika vielelezo kwa wengine. Je! si ni jambo la utukufu moyo wako unapokushuhudia ya kuwa kuna hali ya usafi katika uhusiano wa ndugu wanaotaraji kufunga ndoa? Hili linaleta harufu nzuri ya manukato inayopendeza. Je, ni ushuhuda wa jinsi gani wa nguvu ya Injili watu wawili wanapooana juu ya huu msingi!

Ninaamini huu ndio mpango wa Mungu kwa Kanisa lake na kwa watoto wake. Hakuna haja ya kukata tamaa. Mungu yu hai; anaweza kuleta watu wawili pamoja. Anajua ya mbeleni. Anajua kila kitu kuhusu maisha yetu, na shauku yake ni sisi tuishi maisha safi na matakatifu. Ndio maana ni heri kusubiri, kuliko kujaribisha mambo. Fungua moyo wako; mwache Mungu azungumze na wewe na akushawishi. Kwa Yesu Kristo hakuna kuchelewa. Leo inaweza ikawa siku yako ya kumtangazia Bwana ya kuwa unaenda kuishi maisha yako ya Ukristo kabla ya ndoa kwa kulifuata Neno lake.

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR