Sunday, September 21, 2014

KWANINI UFUNGE NDOA

“Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—MHUBIRI 4:12.
JE, UNAPENDA kwenda kwenye harusi? Wengi wanapenda, kwa sababu mara nyingi hizo huwa pindi zenye kufurahisha sana. Bwana na bibi-arusi wanavalia mavazi yenye kupendeza kwelikweli. Zaidi ya hilo, nyuso zao zinaonyesha kwamba wana shangwe nyingi! Siku hiyo, wana furaha nyingi na inaonekana wana matazamio mengi mazuri ya wakati ujao.
2 Hata hivyo, ukweli ni kwamba ndoa nyingi leo ziko mashakani. Ingawa tunawatakia mema wenzi wapya wa ndoa, nyakati nyingine tunajiuliza: ‘Je, ndoa hii itakuwa na furaha? Itadumu?’ Majibu ya maswali hayo yanategemea ikiwa mume na mke wanaamini na kutumia shauri la Mungu kuhusu ndoa. (Methali 3:5, 6) Wanahitaji kufanya hivyo ili waendelee kukaa katika upendo wa Mungu. Acheni tuchunguze majibu ya Biblia kwa maswali haya manne: Kwa nini ufunge ndoa? Ikiwa utafunga ndoa, utachagua mwenzi wa aina gani? Unaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya ndoa? Na ni nini kinachoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa waendelee kuwa na furaha?
KWA NINI UFUNGE NDOA?
3 Watu fulani wanaamini kwamba siri ya kuwa na furaha ni kufunga ndoa na kwamba huwezi kamwe kutosheka au kuwa na furaha maishani ikiwa huna mwenzi wa ndoa. Hilo si kweli hata kidogo! Yesu, ambaye alikuwa mseja, alisema useja ni zawadi, naye aliwahimiza wale wanaoweza waupe nafasi. (Mathayo 19:11, 12) Mtume Paulo pia alizungumzia faida za useja. (1 Wakorintho 7:32-38) Hata hivyo, Yesu na Paulo hawakuweka sheria kuhusu jambo hilo; na ‘kukataza kufunga ndoa’ ni ‘fundisho la roho waovu.’ (1 Timotheo 4:1-3) Lakini wale wanaotaka kumtumikia Yehova bila kukengeushwa wanaweza kufaidika kwa kuendelea kuwa waseja. Basi, si jambo la hekima kufunga ndoa kwa sababu ndogo-ndogo, kama vile kufunga ndoa kwa sababu tu wenzako wamefunga ndoa au kwamba wanakutia moyo ufanye hivyo.
4 Kwa upande mwingine, je, kuna sababu nzuri za kufunga ndoa? Ndiyo. Ndoa pia ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, inatimiza mambo fulani mazuri na inaweza kuleta furaha. Kwa mfano, ndoa nzuri ndio msingi bora wa maisha ya familia. Watoto wanahitaji kulelewa katika mazingira yanayofaa wakiwa na wazazi wanaowapenda, wanaowatia nidhamu, na kuwapa mwongozo. (Zaburi 127:3; Waefeso 6:1-4) Hata hivyo, kusudi la ndoa si kupata na kulea watoto tu.
5 Fikiria andiko la msingi la sura hii pamoja na mistari inayotangulia: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake. Lakini itakuwaje kwa yule aliye peke yake akianguka wakati ambapo hakuna mwingine wa kumwinua? Tena, wawili wakilala pamoja, watapata joto; lakini aliye peke yake anawezaje kupata joto? Na mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—Mhubiri 4:9-12.
6 Andiko hilo linazungumzia hasa faida ya urafiki. Bila shaka, ndoa ni muungano wa marafiki wa karibu zaidi. Kama andiko hilo linavyoonyesha, katika muungano huo wenzi wa ndoa wanaweza kupata msaada, faraja, na ulinzi. Ili kifungo cha ndoa kiwe imara zaidi, mengi zaidi yanahitajika. Kamba yenye nyuzi mbili, kama mstari huo unavyodokeza, inaweza kukatika. Lakini kamba yenye nyuzi tatu zilizosokotwa au kufumwa pamoja haikatiki kwa urahisi. Lengo kuu la mume na mke linapokuwa kumpendeza Yehova, ndoa yao ni kama kamba yenye nyuzi tatu. Kwa kuwa Yehova anahusishwa kabisa, ndoa hiyo inakuwa muungano imara sana.
7 Pia, katika ndoa ndipo tu tamaa za ngono zinaweza kutoshelezwa inavyofaa. Ni katika kifungo hicho tu ambapo mahusiano ya kingono huonwa kwa kufaa kuwa chanzo cha shangwe. (Methali 5:18) Hata baada ya mtu kupita kipindi ambacho Biblia inakiita “upeo wa ujana”—wakati ambapo tamaa za ngono huanza kuwaka—huenda bado akahitaji kuzuia tamaa hizo. Zisipozuiliwa, tamaa hizo zinaweza kumwingiza katika mwenendo mchafu au usiofaa. Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuwapa watu ambao hawajafunga ndoa shauri hili: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.”—1 Wakorintho 7:9, 36; Yakobo 1:15.
8 Hata kuwe na sababu gani za kufunga ndoa, mtu anapaswa kuona mambo kihalisi. Kama Paulo alivyosema, wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Watu waliofunga ndoa hupata matatizo fulani ambayo waseja hawapati. Hata hivyo, ukiamua kufunga ndoa, unaweza kufanya nini ili upunguze matatizo na kuwa na furaha zaidi? Njia moja ni kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima. Etaendelea

Tafakari ya Neno la Mungu Domonika ya 25 ya Mwaka A,

Mpendwa, tunatafakari masomo ya Jumapili ya 25 ya mwaka wa A wa Kanisa, tukialikwa kuwa na matumaini daima katika kumtafuta Bwana na kutambua kuwa wema wa Mungu ni wa milele kwa watu wote na fikra zake ni tofauti na fikra za kibinadamu. Katika somo la kwanza Waisraeli wako utumwani Babeli kwa sababu hawakutii mausia ya Bwana na zaidi wanaona hawawezi kusamehewa dhambi zao, wamepoteza tumaini na wanaona kana kwamba Mungu amewatupa na kuwaacha kabisa. Zaidi ya hilo wanaongeza kosa jingine tena la kumwona Mungu anayefikiri kama wao, wanafikiri hawezi kuwasamehe tena.


Mpendwa, katika shida yao hiyo Mungu anamtuma Nabii Isaya awaambie kuwa fikra na njia za Mungu ni za juu mno ni tofauti na fikira za kibinadamu kiasi kwamba si rahisi kuzielewa. Zaidi ya hilo Isaya anawakumbusha kuacha njia zao mbaya na kumrudia Bwana. Kumrudia Bwana si tu kuacha dhambi, bali pia kubadili namna ya kumtazama Mungu, Mungu aliye haki na mkamilifu. Mawazo haya yatajitokeza waziwazi katika Injili ambapo tunaona Mungu anayewapenda wote wadhambi kwa wema.


Mtume Paulo akikoleza ujumbe wa nabii Isaya anawaambia Wafilipi, hata kama kuna shida katika maisha yao watambue kuwa kuishi kwao ni Kristu, ndiyo kusema la maana katika maisha yao ni Kristu mfufuka. Mara kadhaa watu wapatapo shida huanza manunguniko dhidi ya Mungu na kusahau kwamba yote waliyonayo yametoka kwake. Wanasahau kuwa, kwa njia ya msalaba yaani njia ya mateso, Kristu ametustahilisha kwenda mbinguni. Ndiyo kusema, hata sisi tuliodhaifu tunapaswa kupitia njia ya mateso ili kuweza kufika Mbinguni. Kwa hakika mtume Paulo anapoandika barua hii kwa Wafilipi yuko katika wakati mgumu yaani kuchagua kufa ili akae na Kristu au kuendelea kuhubiri Injili kwa mataifa, na mwisho anaona ahitimishe fikra zake akisema kuishi kwangu ni Kristu na kufa ni faida. Hapa tunaonja imani ya Paulo ilivyozama katika Mwana wa Mungu.

Tujiulize je kwetu sisi kuishi na kufa, twaweza kuvipokea kama alama ya ushindi katika imani kama Mtume Paulo? Mpendwa msikilizaji jitafiti na hivi unapokuwa umechoka, unapokuwa umefikia mwisho wa maisha yako uweze kusema nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza na imani nimeilinda sasa kufa kwangu ni faida na kuishi kwangu ni Kristu!


Mpendwa mwana wa Mungu tukiongozwa na mwinjili Mathayo, tunapata kuonja kuwa mawazo ya Mungu ni ya juu sana kuliko yetu. Jambo hili linajionesha wazi katika Injili ya leo pale ambapo Bwana wa shamba anawaajiri watu mbalimbali katika masaa tofauti na mwishoni anawalipa ujira sawa. Mpendwa katika hali ya kawaida, Bwana huyu angepaswa kuwalipa tofauti kwa maana muda wa kazi ulikuwa tofauti. Kuwalipa ujira sawa pia ni namna ya kusema kuwa uvivu uendelee katika ulimwengu, tuseme hakuna ile haki ya kawaida yaani common justice! Hii ni namna yetu ya kufikiri na hata namna ya watu wa wakati huo, lakini je Mwinjili anataka kutuambia nini? Je Bwana afikiri kama sisi?


Kwa hakika kuwalipa ujira sawa maana yake, wema wa Mungu ni kwa ajili ya wema na wabaya. Wale walioajiriwa kwanza ndio walisadikiwa kuwa wema na wale wa baadaye ndio kundi wakilishi la walio wabaya. Pamoja na hilo kuna jambo jingine jema, kwamba mwenye shamba anapenda kila mmoja afanye kazi, asiishi bila wajibu, ajisikie katikati ya jumuiya ya watu kwa maana kazi huleta heshima. Kwa jinsi hiyo kazi ya wokovu inaendelea na inawaletea heshima watu wote.
Mfano huu wa mwenye shamba unatufundisha kuwa Mungu si mhasibu wala meneja anayewalipa watu kulingana na jasho lao tu, bali kulingana na upendo wake aliokusudia tangu alipoumba ulimwengu. Hatuna uwezo wa kupata stahili yoyote toka kwa Mungu kwa nguvu zetu bali kwa uweza wake, huruma yake na mapendo yake ya milele. Kwa wazo hili tunarudi kwa nabii Isaya anayetuambia kuwa njia zake ni za juu mno na mawazo yake hatuwezi kuyafikia. Tunaalikwa kutambua kuwa wokovu si kwa maveterani peke yao bali hata vijana wanaokuja saa kumi na moja jioni! Hakutakuwa na upendeleo wowote katika wokovu cha msingi ni kumtafuta Bwana madamu anapatikana. Tumsifu Yesu Kristu.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya Cpps

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR