Sunday, January 10, 2016

TAARIFA YA SERIKALI KUHUSU ZOEZI LA KUHAMISHA WAKAZI WA MABONDENI KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM


Utangulizi
Nchi yetu ina kingo za mito na mabonde na maeneo mengi hatarishi ambamo watu wanaishi kinyume cha sheria, huku wakiharibu mazingira na kuhatarisha maisha yao.  Kutokana na uhaba wa makazi, hali ni mbaya zaidi katika mabonde ya Jiji la Dar es Salaam, hasa bonde la Mto Msimbazi.
 
Serikali za awamu zote, zimekuwa zikifanya jitihada za kuwaondoa wakazi wa maeneo ya mabondeni wanaoishi katika maeneo hayo kinyume cha sheria lakini mafanikio yamekuwa si ya kuridhisha.

Serikali ya Awamu ya Tano, ambayo moja ya misingi yake mikuu ni utii wa sheria za nchi, imeanza jitihada za kuwaondoa wakazi hawa. 
Tuliamua kuanza na Bonde la Mto Msimbazi kwasababu ndiko kwenye watu wengi na athari kubwa.Sababu zetu kuu za kufanya zoezi hili ni kusafisha mabonde na mito katika jiji la Dar es Salaam na mazingira yanayozunguka ni:-

Kunusuru maisha ya wananchi wanaoishi katika mazingira hatarishi. Eneo la Bonde la Mto Msimbazi lilitangazwa kuwa ni eneo hatarishi kuishi binadamu tangu mwaka 1949 na baadaye 1979.

Kupanua uwezo wa mito ya Dar es Salaam ili kupitisha maji ya mvua kwa kasi kubwa, hivyo kupunguza uwezekano wa kutokea mafuriko na maafa wakati wa mvua nyingi;Kuzuia milipuko ya magonjwa, hasa ya kipindupindu, hasa wakati wa mvua;

Kuzuia eneo hilo kuendelea kutumika kama maficho ya wahalifu na uhalifu;

Kutoa nafasi kwa Serikali kuandaa na kuendeleza eneo hilo kwa mujibu wa sheria za nchi na mipango miji;

Utaratibu wa Zoezi
Kabla ya nyumba kubomolewa, taasisi hizi zinashirikiana kuhakiki iwapo nyumba anayokaa mkazi ina nyaraka za umiliki na vibali vya ujenzi na iwapo nyaraka hizo zina uhalali wowote. 
 
Nyumba ambazo zimethibitika kuwepo katika maeneo yasiyostahili ndio zinawekwa alama X kuashiria kwamba wakazi wanapaswa kuhama au kubomoa. Baada ya hapo, mkazi hupewa muda wa kubomoa na kuhama mwenyewe.

Kutokana na utaratibu huu, sehemu kubwa ya nyumba zinazobomolewa ni zile ambazo watu wamekwishaamua kubomoa wenyewe. 
 
Baada ya hapo, alama huwekwa kuonyesha mpaka wa bonde. Katika zoezi hili, imebainika kwamba sehemu kubwa ya wakazi wa maeneo ya mabondeni ni wapangaji huku wamiliki wakikaa sehemu nyingine salama.
 Serikali pia imeweka Dawati la Malalamiko katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Tathmini ya Zoezi
Jana, terehe 7 Januari 2016, Mawaziri watatu (Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI; na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais; pamoja na Naibu Waziri wa  Maliasili na Utalii), walifanya mkutano wa kutathmini zoezi la kuhamisha wakazi wa mabondeni katika Jiji la Dar es Salaam. 

Mkutano huo ulipokea ripoti ya timu ya wataalam wa Wizara mbalimbali, inayoongozwa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira, ambayo, pamoja na mambo mengine ilibainisha kwamba sehemu kubwa ya kubaini makazi yaliyojengwa kinyume cha Sheria katika Bonde la Mto Msimbazi imekamilika. 
Ripoti ilieleza kwamba, hadi sasa, wananchi katika nyumba 774  wamehama na nyumba hizo kubomolewa. Ilielezwa pia kwamba kabla ya mkazi kuombwa  kuhama, uhakiki kuhusu uhalali wa makazi anayoishi hufanywa. 
Kutokana na uhakiki huo, jumla ya wakazi 20 walikuwa na hati halali za makazi na wakazi 119 walikuwa na leseni za makazi za muda mfupi. 
Hawa watu hawakuhamishwa. Mawaziri walipokea maelezo kuhusu changamoto mbalimbali zilizojitokeza katika zoezi hilo.  
Baada ya tafakuri na mjadala, Mawaziri hao walitoka na msimamo ufuatao, kama uamuzi wa Serikali: -

1.Zoezi la kuwaondoa wananchi waishio katika bonde la Mto Msimbazi (eneo hatarishi) litaendelea kwa utaratibu ambao hautaleta mateso na usumbufu kwa wananchi;

2.Katika awamu hii, zoezi litajikita katika Bonde la Mto Msimbazi tu.

3.Kwa wakati huu, watakaohitajika kuhama ni wale tu ambao makazi yao yamo NDANI kabisa ya bonde, kwenye miteremko ya kuingia bondeni na kwenye KINGO za mto;

4.Wale watakaokuwa na nyaraka halali walizopewa na mamlaka za umma, zilizowamilikisha na kuwaruhusu kujenga katika bonde hilo, hawatahamishwa bila kupewa sehemu nyingine za kujenga. Na watumishi wa umma waliowamilikisha maeneo hayo watachukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria;

5.Serikali, ndani ya siku tatu zijazo, itaanza zoezi la kuzoa kifusi na kusafisha maeneo ambapo ubomoaji umefanyika.

6.Serikali itaheshimu amri za mahakama kuhusu mapingamizi yaliyowekwa na baadhi ya wakazi wa mabondeni lakini pia itafuatilia kesi hizi ziishe haraka ili taratibu zinazofuatia zifanyike;

7.Serikali itawachukulia hatua za kinidhamu watumishi wake wanaoendesha zoezi hili kinyume na misingi ya sheria zinazotekelezwa, na kinyume na misingi ya haki na uwazi, ikiwemo wanaoweka alama za X zaidi ya mita zilizowekwa kisheria. Limeanzishwa dawati la malalamiko katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa ajili ya kupokea malalamiko au maswali kuhusu zoezi hili.

8.Nyumba na majengo ya miaka mingi, yaliyokuwepo miaka mingi kabla ya kutungwa kwa Sheria zinazotekelezwa kwa zoezi hili, hayatabomolewa isipokuwa tu pale maisha ya wakazi yapo hatarini. Wanaoishi katika makazi hayo watapewa miongozo ya hatua za kuhifadhi mazingira na kujiokoa na maafa;

9.Serikali haina dhamira ya kubomoa mahoteli makubwa ya siku nyingi yaliyo karibu na fukwe katika maeneo ya Masaki. Wamiliki wa mahoteli haya watapewa masharti na miongozo ya kuhifadhi mazingira kwa mujibu wa Sheria.

10.Serikali inaweka uratibu wa karibu zaidi miongoni mwa taasisi zake ili hatua za utekelezaji wa sheria za nchi zisiwe chanzo cha taharuki katika jamii.

11.Serikali haina dhamira ya kuwatesa wananchi wake kwa kuwalazimisha kuhama katika makazi yao bila sababu za msingi. Lakini pia Serikali haiwezi kuruhusu wananchi waendelee kukaa katika maeneo ambayo ikinyesha mvua kubwa maisha yao yapo hatarini.
 Itakumbukwa kwamba katika mafuriko ya mwaka 2011, wananchi 49 waishio mabondeni walipoteza maisha. Kwa mujibu wa taarifa ya Kurugenzi ya Hali ya Hewa, mwaka huu zinatarajiwa kunyesha mvua kubwa kuliko zilizowahi kutokea katika miaka ya hivi karibuni.

12.  Serikali inafuatilia kwa karibu kwa mamlaka za Serikali za Mitaa juu ya taarifa za wananchi wanaohitaji msaada maalum wa kibinadamu.

Suala la Mchungaji Getrude Rwakatare
Mkutano ulipokea taarifa kuhusu suala linaloongelewa sana la nyumba ya Mchungaji Rwakatare.  Ilielezwa kwamba Mchungaji Rwakatare amejenga nyumba yake pahali ambapo amezuia mtiririko wa mto kwa kujaza kifusi ili kupata eneo zaidi katika eneo la miti ya mikoko, kinyume kabisa na Sheria tatu muhimu.  
Pia ilielezwa kwamba tangu wakati ujenzi unaanza jitihada za kumsimamisha zilifanyika na mamlaka za Serikali za Mitaa lakini ikashindikana kutokana na sababu mbalimbali. Pale Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira lilipoingilia kati na kutaka kuibomoa nyumba hiyo, Baraza lilishtakiwa mahakamani. 
Wakati kesi inataka kuanza kusikilizwa, mwanasheria mdogo wa Baraza, yeye mwenyewe bila kuagizwa wala kuwaarifu wakubwa zake, mnamo tarehe 11 Mei 2015, aliingia makubaliano na mawakili wa Mchungaji Rwakatare kwa niaba ya Baraza ya kuondoa kesi hiyo mahakamani na kukubali, kwa niaba ya Baraza, kutombughudhi kabisa Mchungaji Rwakatare.  
Makubaliano hayo yalisajiliwa na Mahakama kama hukumu tarehe 13 Mei 2015. Mwanasheria huyo alificha makubaliano hayo kwa miezi mitano hadi Oktoba 2015, yalipogundulika na mtumishi mwingine wa Baraza. Mkutano ulielezwa kwamba Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, kwa kufuata taratibu zote, alishaagiza kufukuzwa kazi, kukamatwa na kufunguliwa mashtaka kwa mwanasheria huyo. 
Mwanasheria huyo alifukuzwa kazi siku ya juzi tarehe 6 Januari 2016 na taarifa zake zimekwishafikishwa TAKUKURU. 
Vilevile, Ofisi ya Makamu wa Rais, iliiagiza Baraza kufungua shauri mahakamani la kuomba “makubaliano” kati yake na Mchungaji Rwakatare yawekwe pembeni kwasababu yalipatikana na njia ya udanganyifu. Shauri hilo lilifunguliwa tarehe 29 Disemba 2015.

Kuhusu Karakana ya Mradi wa Mabasi Yaendayo kwa Kasi (DART)
Mkutano pia ulijulishwa kuhusu hoja inayozungumzwa kwamba wananchi wanaondolewa katika maeneo ya kuishi mabondeni lakini mradi wa DART umeachwa.
 Mkutano ulielezwa kwamba Sheria ya Mazingira (kifungu 57 (2)) inatoa nafasi ya kutolewa ruhusa kwa miradi/shughuli zenye maslahi ya taifa kufanyika katika maeneo ya mabondeni, na kwamba Waziri mwenye dhamana ya mazingira anaruhusiwa kutoa miongozo ya namna ya shughuli hizo zinavyoweza kufanyika bila kuathiri mazingira.
 Mradi wa DART ulipata kibali hicho na una mkataba na Baraza la Mazingira kuhusu hatua za hifadhi ya mazingira zinazopaswa kutekelezwa katika mradi huo.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA MAKAMU WA RAIS
08.01.2016

check na hii siku yako iwe nzuri Justin Bieber - Sorry (Lyric Video)

Chamwino Dodoma wananchi Wala Viwavi Jeshi Kuikabili Njaa inayowakabili

Wakazi wa Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma wanakula wadudu jamii ya viwavi jeshi, wanaojulikana kwa jina la fumbili kutokana na njaa kali iliyoikumba wilaya hiyo.


Hata hivyo, chakula hicho huenda kikapotea wakati wowote kutokana na mvua kutonyesha hivyo wadudu hao, ambao huishi kwa kutegemea majani, nao kupotea kwa kukosa chakula.
Mbali na fumbili, chakula kingine ambacho kilikuwa mkombozi kwa wakazi wengi, hususan Tarafa ya Chilonwa, ni matunda ya zambarau ambayo nayo yatakwisha wakati wowote kwani msimu wake umekwisha.
Chamwino ni wilaya iliyoko takriban kilomita 30 kutoka mjini Dodoma, ikikadiriwa kuwa na watu 349,714 na mazao ya chakula yanayolimwa kwenye wilaya hiyo ni mtama, uwele, mpunga, mahindi, mihogo, viazi vitamu, kunde, nyonyo, mbogamboga na choroko.
Juzi, Mbunge wa Chilonwa, Joel Mwaka aliitisha kikao cha dharura cha madiwani wote wa jimbo hilo lenye kata 14 kujadili suala hilo na kila diwani aliyechangia mjadala huo, alionyesha kujuta kugombea kwa kuwa wananchi wanamlilia.
Madiwani hao waliweka azimio la kusafiri kwenda Ikulu, Dar es Salaam kuwasilisha kilio cha wananchi wao.
Akizunguma kwenye kikao hicho, Mwaka alisema hali ya wakazi wa Chilonwa ni mbaya kiasi hakuna matumaini hata ya kupata mlo mmoja na badala yake wengi wanaishi kwa uji na matunda pori na fumbili.
Mbunge huyo alilaani mpango wa Serikali wa kuwapa vibali wafanyabiashara kwenda kuchukua mahindi katika ghala la chakula la Songea kwani bei zinakuwa kubwa.
“Ndiyo maana wanyabiashara wengi walikataa kwa kuwa bei inakuwa ni kubwa ambayo haiwezi kurudisha hata gharama zao, kitendo hicho kimefanya wafanyabiashara wa kawaida kuendelea kuwaumiza wananchi, lakini hakuna mwenye uwezo kipindi hiki, nasema walete mahindi ya bure siyo ya kununua tena,” alisema Mwaka.
Mbunge huyo alihoji ni kwa nini Serikali isiruhusu ghala la mahindi la Kizota, Dodoma kutoa mahindi kwa wafanyabiashara ili bei isiwe kubwa kama ilivyo sasa. Alisema bei ya sasa ya Sh15,000 kwa debe la kilo 20 ni kubwa na wachache ndiyo wanaoweza kuimudu.
Diwani wa Majeleko, Mussa Omari alifika kwenye kikao hicho akiwa na fumbili wengi akisema aliwakamata wakati akishirikiana na wapigakura wake kupata kitoweo.
Hata hivyo, hakuna diwani aliyeonyesha mshangao kwani kila mmoja alisema hata kwake wanakula wadudu hao na ni jambo la kawaida.
Mussa alisema hali ni mbaya zaidi kwenye kata yake na tayari baadhi ya watu wameanza kuvimba miguu kwa kukosa chakula, huku kukiwa na taarifa za vifo vinavyosadikiwa kuwa vimetokana na watu kukosa lishe.
Diwani wa Zajilwa, Farida Maulidi alisema katika eneo lake, kuna kaya 10 ambazo zimeelemewa zaidi na tayari kuna taarifa za vifo viwili. “Kwangu hali ni mbaya sana yaani naomba tuandamane kwenda hata kwa mkuu wa mkoa au niungane na wenzangu twendeni Ikulu tukamuone Rais. 

Mbona, pamoja na kusema hakuna mtu atakayekufa kwa njaa, huku watu wanateketea na sisi tupo? Kila siku nafanya kazi ya kutafuta uji kunusuru maisha ya watu wangu,” alisema Maulid.
Ofisa kilimo wa wilaya hiyo, Godfrey Mnyamale alikiri kuwa hali ni mbaya wilayani Chamwino na kusema kama juhudi za makusudi hazitachukulia ndani ya wiki moja, kutakuwa na madhara makubwa.
Mnyamale alisema tatizo kubwa lililoikumba Chamwino ni mvua kidogo zilizonyesha msimu wa mwaka jana iliyosababisha watu wasivune chakula cha kutosha.
Alisema ili kukabiliana na njaa iliyoanza wilayani humo tangu Aprili mwaka jana, jumla ya tani 14,377 za mahindi zinatakiwa kwenye vijiji 107, lakini hadi sasa Serikali imepeleka tani 150 tu ambazo ziligawiwa katika vijiji 10 tena kwa idadi ndogo.
Akizungumzia hali hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Chiku Galawa alisema Serikali haijalala katika kuwaza namna ya kuwasaidia.
Galawa alisema katika kipindi kilichopita, Chamwino ilipewa msaada wa chakula lakini kilikuwa hakitoshi na ndiyo sababu hakikupelekwa maeneo yote.
“Hata hivyo, lazima watu wajue kuwa huwezi kuomba chakula leo na ukapewa leo. Leo kamati ya mkoa imeshapeleka maombi taifa na juzi niliongea na mhusika kwamba wanalifanyia kazi,” alisema Galawa.
Kuhusu wafanyabiashara kulazimishwa kununua mahindi Songea badala ya Dodoma, alisema jambo hilo liko nje ya uwezo wake kwa kuwa wenye kuwapangia ni mamlaka ya chakula.
Aliwataka wanasiasa kuacha kukuza mambo kuwa kuna watu wamekufa kwa njaa, badala yake watumie muda huo kuwahamasisha wafugaji kuuza mifugo na kununua chakula.

Thursday, January 7, 2016

IKULU LEO AFIKA RAIS MSTAAFU BENJAMINI MKAPA NA JAJI MSTAAFU WARIOBA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimpokea Rais Mstaafu wa Awamu ya tatu, Benjamini William Mkapa Ikulu jijini Dar es Salaam January 7,2016.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 07 Januari, 2016 amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Mstaafu wa awamu ya tatu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa na Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba Ikulu Jijini Dar es salaam.

Akizungumza mara baada ya Mazungumzo hayo Rais Mstaafu Mkapa amesema lengo la kukutana na Rais Magufuli ni kumpongeza kwa dhamana aliyopewa na watanzania kuiongoza nchi, kuunda serikali na kumtakia heri ya Mwaka Mpya.


Rais Mstaafu Mkapa pia amemhakikishia Rais Magufuli kuwa yupo tayari kutoa ushirikiano wakati wote ama kufanya kazi yoyote endapo atahitajika kufanya hivyo.

Kwa upande wake Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba pamoja na kumtakia heri ya Mwaka Mpya, amempongeza Rais Magufuli kwa jinsi alivyoanza kazi vizuri hususani katika kusimamia ukusanyaji wa mapato, kubana matumizi na kuelekeza matumizi kwenye maeneo muhimu ambayo yanawahusu wananchi yakiwemo afya na maji.


Jaji Warioba ameongeza kuwa Watanzania wote wanapaswa kumuunga mkono Rais Magufuli kwa kazi kubwa anazofanya, ambazo ni kukomesha rushwa, ufisadi, matumizi mabaya ya madaraka na wizi wa mali ya umma.

"Lazima kila mmoja amuunge mkono Rais, tusije tukamuachie, pale ulipo kama ni mambo ya rushwa uanzie hapo hapo, kama ni mambo ya matumizi mabaya ya madaraka anzia hapohapo, tusije tukamuachia Rais pekee yake, yeye awe kiongozi wetu, lakini watanzania wote tushughulike na matatizo hayo" alisisitiza Jaji Warioba.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es salaam
07 Januari, 2016


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimpokea Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba Ikulu jijini Dar es Salaam January 7,2016


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba Ikulu jijini Dar es Salaam alipomtembelea January 7,2016




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya kufanya mazungumzo January 7,2016


HEKALU LA DK. LWAKATARE LASHINDIKANA TENA KUBOMOLEWA

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjx7hKNyj6kogEU4YKMrs3_WNqiA7tSU_dYjwI5xi9vxCSYcBTmSddO_eYfY5pxYtWbPcQIrQ25fKg6cAisuWEvYzihJddO4MEcA7tXEDYLzLqobHPaeqV0YbEBp6BrBfE7mkZGO32EiOLm/s1600/3.jpgMAHAKAMA Kuu Kitengo cha Ardhi imezuia nyumba anayoishi Mchungaji wa Kanisa  la  Assemblies of God Mikocheni, Dk. Getrude Lwakatare kubomolewa.
 
Uamuzi huo wa mahakama ulitolewa juzi na Jaji John Mgeta, baada ya Wakili wa Lwakatare, Emmanuel Muga kuwasilisha maombi ya kupinga ubomoaji huo chini ya hati ya dharura.
 
Jaji Mgeta alizuia ubomoaji wa jengo hilo ama kuchukua hatua yoyote kuhusu jengo hilo lililopo Kawe Beach.
 
Muga aliwasilisha maombi akimwakilisha mdai ambaye ni mtoto wa Mchungaji Lwakatare, Robert Brighton dhidi ya wadaiwa NEMC, Manispaa ya Kinondoni na wadau wengine wote.
 
“Mheshimiwa jaji, nawasilisha maombi ya zuio la kubomoa nyumba ya mteja wangu chini ya kifungu namba 95 cha Sheria ya Mwenendo wa Madai na kifungu namba 2(3) cha JALA vinavyotoa mamlaka kwa mahakama kutoa nafuu stahili pale kunapokuwa na ukiukwaji wa kuvunja haki ya wazi,” alidai.
 
Akitoa uamuzi huo alisema tayari pande husika zilikuwa na kesi namba 70 ya mwaka 2012 na ikamalizika kwa kutoa hukumu na kukazia hukumu iliyompa haki ya ushindi mdai.
 
“Mahakama ilimpa haki mdai, lakini chakushangaza mdaiwa anakiuka matakwa ya hukumu na kutaka kubomoa nyumba, kwa hali isiyokuwa ya kawaida mdai anahitaji ulinzi wa mahakama hii ya haki,”alisema Jaji Mgeta.
 
Alisema nyumba hiyo ipo katika kiwanja namba 2019 na 2020 ambapo hati yake ilitolewa mwaka 1979.
 
Inadaiwa mwaka 2011 NEMC ilitoa notisi ya kuvunja nyumba hiyo baada ya kushinikizwa na wakazi wa eneo hilo wakidai ujenzi wake unaziba Mto Ndumbwi na uko jirani na mikoko.
 
Wakili Muga aliwasilisha maombi ya kuzuia nyumba  ya mteja wake kubomolewa  baada ya Wizara  ya  Maliasili  na  Utalii kupitia  wakala  wa  misitu  Tanzania (TFS ), kuweka alama  ya X wakidai imo katika hifadhi  ya  bahari.

ANZA KURUDISHA MKOPO WAKO WA ELIMU YA JUU (CAG ATETA

Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), imeanza kukagua taasisi za umma kuhusu utekelezaji wa sheria inayozitaka kuwatambua waajiriwa walionufaika na mikopo ya elimu ya juu.
 
Hadi Mei mwaka jana, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) ilikuwa imekusanya Sh65.2 bilioni kati ya Sh123.8 bilioni zilizopaswa kuwa zimerejeshwa.
 
Bodi hiyo iliwakopesha wanafunzi Sh1.8 trilioni tangu mwaka wa masomo 1994/95 hadi Juni 2014 kati ya fedha hizo, Sh51 bilioni zilitolewa na iliyokuwa Wizara ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia.
 
Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, George Nyatega alisema ili kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mikopo iliyoiva, CAG ameanza kutekeleza matakwa ya kisheria ya ukaguzi kwenye taasisi za umma ili kuwabaini wanafunzi waliopaswa kuanza kurejesha mikopo yao.
 
“Ni imani ya HESLB kuwa waajiri katika utumishi wa umma watatoa ushirikiano kwa ofisi ya CAG ili kuondokana na matatizo ya kisheria,” alisema.
 
Nyatenga alisema sheria iliyoanzisha HESLB inazitaka taasisi zote za umma kuijulisha kwa maandishi kuhusu waajiriwa wapya ndani ya siku 28 na bodi kuthibitisha kama waajiriwa hao ni wanufaika wa mikopo au la.
 
Mkurugenzi huyo alisema baada ya bodi kupokea taarifa na kuthibitisha kuwa waajiriwa ni wanufaika wa mikopo, mwajiri atapaswa kuijulisha HELSB na kuanza kukata sehemu ya mshahara wa mwajiriwa ndani ya siku 30. 

SUMATRA WAKARIBISHA MAONI YA WANANCHI JUU YA NAULI ZA MABASI YAENDAYO KASI



MAMLAKA ya Udhibiti,Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), inatarajia kukusanya maoni ya wananchi juu ya viwango vya nauli za mabasi yatakayotoa huduma ya usafiri wa haraka Jijini Dar es Salaam.

Taarifa hiyo imetolewa na Ofisi ya Mkurugenzi wa SUMATRA kwa vyombo vya habari kwenda kwa wananchi  ambapo ofisi hiyo itawaalika wadau wote wa usafiri hususani wananchi kuchangia maoni kwenye mkutano utakao fanyika januari 5 kwenye ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam kuanzia saa 3 na nusu asubuhi.

Mamlaka  pia inapokea maoni ya wananchi kupitia anuani ya ofisi ya Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo ambayo ni S.L.P 3093 au kwa barua pepe ambayo info@sumatra.go.tz ambapo kabla ya kufikia uamuzi wadau wanatakiwa kutoa maoni ya kuridhia viwango vya nauli  kwa mujibu wa sheria ya Sumatra.

Maoni ya maandisi yatapokelewa kwenye ofisi ya Mkuregenzi Mkuu iliyopo Jengo la Mawasiliano House Makutano ya barabara ya Ali Hassani Mwinyi na Nkumo kuanzia Saa 4 asubuhi hadi saa 9 alasiri mwisho wa kupokelewa maoni hayo ni Januari 13 mwaka huu.

Mamlaka hiyo imepokea maombi ya nauli kutoka kampuni ya UDA-RT inayolenga kutoa huduma ya mpito ya usafirishaji jijini Dar es Salaam katika kutekeleza awamu ya kwanza ya mradi wa Dart.

Maombi yaliyowasilishwa na kampuni hiyo ni Safari kwenye njia za pembeni (feeder route) shilingi 700 ,safari kwenye njia kuu (trunk route) shilingi 1200 na njia zote mbili ni 1400 ambapo wanafunzi watalipa nusu nauli anayotoa mtu mzima.

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR