Monday, March 3, 2014

Mafungo ya Kwaresima Consolata Mission Centre - Bunju

Kituo cha Consolata mission center Bunju, kinawaalika Vijana wote katika Mafungo ya kwaresima, yatakayofanyika  siku ya jumamosi tarehe 08/03/2014 siku ya jumamosi

Mada ni: "INJILI YA FURAHA:EVANGELII GAUDIUM"

Ada ya ushiriki kwa kila Kijana ni TSHS 5000 kwa ajili ya chakula na chai .Fika bila kukosa na jitahidi ufike kabla ya saa Mbili asubuhi .......

MAANA YA KIPINDI CHA KWARESIMA

Hii ni Kwaresima

Nini maana ya Kwaresima?Kwa Kilatini na Kiitaliano neno Kwaresima lilimaanisha “40” yaani siku 40 za kufunga za wiki kati ya Jumatano ya Majivu hadi Jumamosi Kuu. Kwa Kijerumani Kwaresima maana yake “Kipindi cha kufunga.”

Kwaresima ilianzaje?
Kabla ya kuona Kwaresima jinsi ilivyoanza, ni vizuri kuongea kidogo kuhusu Sikukuu ya Pasaka ili tuweze kupata mwanga wa kuelewa mwanzo wa kipindi hiki muhimu cha Kwaresima.

Habari Njema yatuambia kwamba YESU KRISTO alifufuka “Siku ya kwanza ya juma.” “Hata sabato ilipokwisha, ikipambazuka siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi.” (Mt.28:1) Hii ni kwasababu Wakristo walianza kukutana pamoja kwa sikukuu ya ufufuko wa BWANA kila wiki sio Jumamosi kama Wayahudi, bali siku iliyo fuata. “Hata siku ya kwanza ya juma, tulipokuwa tumekutana ili kumega mkate, Paulo akawahutubu, akiazimu kusafiri siku ya pili yake, naye akafuliza -`maneno yake hata usiku wa manane.” (Mdo.20:7). “Siku ya Kwanza ya juma kila mtu kwenu na aweke akiba kwake, kwa kadiri ya kufanikiwa kwake: ili kwamba michango isifanyike hapo nitakapokuja.” (1Kor.16:2), siku ambayo Warumi waliita “Siku ya Jua”. Mara moja jina hilo lilibadilika na kuwa “Siku ya BWANA”

Kanisa la mwanzoni halikusherehekea sikukuu kama vile Noel, Sikukuu kwa heshima ya Mama Bikira Maria au sikukuu yeyote ile. Kulikuwepo na adhimisho la ufufuko wa BWANA kila wiki na hakuna zaidi.

Miaka mingi ikapita kanisa likiwa katika hali hii. Baadaye kulikuwepo na hitaji la kusherehekea tukio la kiini cha imani yetu kwa namna ya pekee. Wakristo waliona umuhimu wa kuwa na muda kwa sikukuu ya kwanza kati ya sikukuu zao yaani “Jumapili ya Pasaka”, ambayo ilifikiriwa kama “Mama wa Jumapili zote”, “Mama wa skikukuu zote”. Waliiona sikukuu hiyo kama “Malkia wa sikukuu zote, wa Jumapili zote, na kiujumla kama Malkia wa siku zote za mwaka. Tangu mwanzoni mwa karne ya pili, Jumuiya zote za Kikristo walikuwa wanasherehekea sikukuu hii ya Pasaka. Sherehe zilikuwa zinahitimishwa na kusanyiko la sala lililofanyika usiku na kumalizikia na Ekaristi. Ushiriki wa kwenye ibada hiyo, ulichukuliwa kama ni kitu muhimu sana kwa mkristo.



Kuanza kwa Kwaresima

Wote tunafahamu kwamba, ufanisi au mafanikio yoyote ya sikukuu au ya jambo lolote yanategemea sana maandalizi yake. Miaka miambili hivi baada ya KRISTO, Wakristo walitaka kuvuna matunda ya kiroho ya Paska kwa wingi. Ili kufanikisha hili, walianzisha utamaduni wa kuwa na siku tatu kabla ya Pasaka kwa sala, tafakari na kufunga kwa nia ya kuonyesha masikitiko yao juu ya kifo cha YESU KRISTO. Kutokana na ukubwa na umuhimu wa sikukuu hii, mbali ya kuona umuhimu wa maandalizi, walitafuta njia za kuongeza muda wa furaha na utajiri wa kiroho utokanao na Pasaka. Hivyo walianzisha “Wiki Saba,” yaani siku 50 za Pentekoste ambapo walisherehekea na kuzipitisha siku hizo kwa hali ya furaha. Askofu Mt. Ireneus alisema kuwa muda huo wa siku 50 ni kama Sikukuu ya Siku moja yenye umuhimu sawa na Jumapili. Katika kipindi cha siku za Pentekoste, sala zilikuwa zinasaliwa hali wamesimama, kufunga kulikatazwa na sakramenti ya ubatizo ilikuwa ikiadhimishwa. Ni kama vile sikukuu ya Pasaka ilidumu kwa kipindi chote cha siku 50. Miaka 150 ilipita na mwishoni mwa mwaka 350 B.K., Wakristo waliona kama siku tatu hazikutosha kwa maandalizi ya sikukuu kama hii. Hivyo waliongeza hadi kufikia siku 40. Hivi ndivyo Kwaresima ilivyoanza.

Kwa nini siku 40?
Tunaposema kuku wanne au kilo saba za mchele tuna maana kama ilivyo yaani kuku wanne na kilo saba za mchele. Si zaidi au pungufu.

Namba au tarakimu mbalimbali tunazokutana nazo katika Biblia zinaashiria lugha za picha na siyo kuchukulia katika thamani ya kuhesabu. Hivyio basi, tunapokutana na namba kama 40 huenda isimaanishe 40 kama tunavyo hesabu fedha. Kati ya maana nyingi zilizotolewa kwa namba 40, kuna moja yenye maana ya pekee, inamaana ya kipindi cha maandalizi cha kutosha kisichokuwa na muda maalum, kwa tukio kubwa. Kwa mfano , Gharika ilidumu kwa siku 40 usiku na mchana…na ilikuwa ni maandalizi ya ubinadamu mpya; Waisraeli walitumia muda wa miaka 40 jangwani…maandalizi ya kuingia nchi ya ahadi; watu wa Ninawi walifunga na kufanya kitubio siku 40…maandalizi ya kupokea msamaha wa MUNGU; Elia alitembea kwa siku 40 mchana na usiku…kama maandalizi ya kufika mlima wa MUNGU; Musa na YESU walifunga kwa siku 40 mchana na usiku… kama maandalizi kabla ya kuanza utume wao. “Kisha ROHO alimwongoza YESU mpaka jangwani ili ajaribiwe na ibilisi. Akafunga siku arobaini usiku na mchana, na mwishoe akaona njaa” (Mt.4: 1-4)

Natumaini hadi hapo tumeelewa nini maana ya namba 40. Je, ni siku ngapi ambazo zinahitajika kwa ajili ya maandalizi ya sikukuu kubwa kuliko zote za kikristo? Bila shaka ni 40. (Kuanzia Jumatano ya majivu hadi Jumamosi Kuu ukiondoa Jumapili zote) Siku 40 ni muda wa kutosha wa kufanikisha kitu fulani chema, kizuri na chenye thamani.

Lengo la Kwaresima ni nini?

Lengo kuu la Kwaresima ni kufanya upya maisha yetu ya kiroho na kutufanya kuwa watu ambao MUNGU anataka tuwe yaani ni kipindi chenye kutupatia utakatifu, tukikumbuka kuwa sote tumeitwa kuwa watakatifu kama BABA yetu wa mbinguni alivyo mtakatifu (Mt. 5:48). Ni kipindi cha kuuvua utu wetu wa kale na kuvaa utu mpya. Kwani tunasoma:- “Mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unao haribika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho na nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa na MUNGU katika haki na utakatifu wa kweli. Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake…Mwibaji asiibe tena…Neno lolote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema na kufaa…tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama MUNGU katika KRISTO alivyowasamehe ninyi.” (Efe.4:22-32.)

Kwaresima kwa hakika ni kipindi pia cha kuachana na matendo ya mwili. “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo;” (Gal.5:19 – 20)

Kwa ufupi Kwaresima ni kipindi cha kuachana na maisha ya dhambi na kurudi kwa MUNGU kwa kuishi maisha yanayompendeza MUNGU kwa njia ya kufanya toba ya kweli isiyo ya mazoea, na malipizi yasiyo ya nje tu, bali hasa mapinduzi ya kiroho. Katika kipindi hiki tunalazima ya kubadili hali yetu ya ndani. Badala ya kujitafuta wenyewe na kufuata mapenzi yetu, inatupasa sisi kumwelekea MUNGU na kuyatimiza mapenzi yake katika mawazo, maneno na matendo yetu.

Nguzo tatu kuu za Kwaresima ni:

i. Sala.Wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani. Usali mbele ya BABA yako aliye sirini; na BABA yako aonaye sirini atakujazi.” (Mt. 6:6)
Kupata muda wa sala pamoja na MUNGU. Sio tu kunena maneno ya sala fulani, lakini pia kumsikiliza MUNGU akizungumza mioyoni mwetu. Kumuomba MUNGU nguvu ya kubadilika, yaani uongofu wa kweli. Ndiyo maana tunaambiwa. “Tubuni na kuiamini Injili”. Hayo ndiyo MUNGU aombayo kwetu wakati wa Kwaresima. MUNGU anatuita kutoka kwa dhambi, na tuupokee ujumbe wake kwetu – Injili, na kuwa waamninfu kuishi kadiri ya Injili. Ni wakati pia wa kuhudhuria misa mara kwa mara kwa ibada na uchaji, kuhudhuria ibada mbalimbali, kama vile Baraka ya Sakramenti Kuu, Kuabudu Ekaristi Takatifu, kusoma Neno la MUNGU na kuliishi baada ya kuyatafakari maneno hayo ya MUNGU ambayo ndiyo sauti yake MUNGU na kutumia muda wetu kwa mambo ya ki-MUNGU yaliyo matakatifu.

ii. Kufunga. “Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso wako ili usionekane na watu ukifunga, ila na BABA yako aliye sirini; na BABA yako aonaye sirini atakutuza.” (Mt. 6:17-18). Kufunga sio tu kujinyima kutokunywa pombe, kutokula chakula, kutovuta sigara n.k. Kifupi ni kwamba kufunga kuondokana na ubinafsi wetu na kuwafikiria na kuwasaidia wenye shida. Uovu hauwezi kushindwa bila kujitoa nafsi na bila kutoa na kuwapa wahitaji vile tuvipendavyo. MUNGU hapendezwi na kufunga tu, bali upendo kwa wanaoteseka utusukume na kufunga tupendavyo kwa ajili ya kuwasaidia wahitaji. Hivyo kuna mahusiano makubwa sana kati ya kufunga na ukarimu. Kufunga lazima kuendane na ukarimu. Kufunga bila ukarimu huo ni mfungo tasa.

iii. Kutoa Sadaka.Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu kusudi mtazamwe nao. Bali wewe utoapo sadaka hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wa kuume; na BABA yako aonaye kwa siri atakujazi.” (Mt. 6:1) Hayo yanamaanisha kwamba usidai shukurani wala malipo kwa wema wowote uwatendeao jirani zako kwa sadaka yako. Malipo utakayopata uyatazamie tu kutoka kwa BABA yako wa mbinguni. Kutoa tunachojinyima kwa kumsaidia KRISTO anayeteseka kwa wenzetu. Kushirikiana na wengine tulivyo navyo kama vile fedha, nguo, chakula, ama kuwakaribisha wahitaji nyumbani.

Hivyo basi, Mazoezi tunayofanya katika kipindi cha Kwaresima kama kusali zaidi, kusikiliza au kusoma Neno la MUNGU, kutenda matendo ya huruma kwa wahitaji, kufunga chakula na kujihinisha kinywaji pamoja na kuzuia tamaa potovu za mwili wetu, yawe na kusudi la kuibadili hali yetu, kutufanya kuwa na upendo zaidi na huruma kwa wenzetu na kutufanya tuweze kuunganika zaidi na KRISTO MFUFUKA. Tumvue mtu wa zamani katika nafsi zetu na tumvae mtu mpya, yaani KRISTO Mfufuka.

Nini makusudi ya kufunga?YESU alifunga ili awape wanadamu mfano au kielelezo halisi na sahihi cha kuiga, na apate kuokoa roho zetu. Watu wawe na namna bora ya kufanya malipizi, kuuadibisha na kuutumikisha mwili na tamaa kwa kuwa anatenda dhambi.

Nani anapaswa kufunga?Inatubidi tujiangalie sana kwani miili yetu ni midhaifu na myepesi kwa kutenda dhambi na kuipeleka roho motoni. Tusiiendekeze miili yetu, bali tuitawale kwa kufuata maadili ya kimungu na kuinyima madai yake, ambayo ni kishawishi kinachotupeleka upotevuni. Tunapoamua kufuata njia hii, hakika, KRISTO atatuimarisha na kutuongoza kwenye uzima wa milele; na kutupa neema ya kupambanua mema na dhambi, huku tukielekea uzimani. Mdomo unao nena dhambi, na mwili unaotenda dhambi, sherti vyote vitende pia mema, siyo dhambi.

Mtu asiyetenda dhambi hana haja ya kufunga. Lakini hakuna mtu anyefikia utu uzima ambaye hatendi dhambi machoni pa MUNGU hata Wacha MUNGU wana dosari. Kwa hiyo, kila mtu afunge kufidia dhambi zake. Tusipofunga kuna hatari kubwa ya kuungua moto. Ni vizuri waamini wote wafunge ili kulipia fidia ya dhambi zinazotendwa. Tumwabudu KRISTO kwa unyofu na unyenyekevu, ili kwa huruma yake kuu atusamehe dhambi zetu na adhabu tunazostahili.

Ngazi tatu za kufunga chakula:

(a) Ngazi ya kwanza, ni kuacha chakula kimoja fulani, au kitu kingine unachopendelea. Kufunga huku ni rahisi hata kwa watoto. Kwa mfano, kuacha kula nyama au kunywa soda yoyote kwa kipindi kizima cha Kwaresima; au kula chakula bila chumvi, au kunywa chai bila sukari kwa kipindi kizima cha mfungo. Huu ni mfungo rahisi.

(b) Ngazi ya pili, ni kuacha kabisa kula siku nzima. Hii ni ngazi ya kawaida, yaani mfungo wa kawaida. Huku ni kula mlo mmoja tu kwa siku hadi utosheke. Yawezekana ikawa ukala mlo wa mchana au wa jioni tu. Asubuhi au jioni (au asubuhi na mchana) ule kidogo sana. Katikati ya hapo usile chochote tena wala kunywa chochote.

(c) Ngazi hii ya tatu ni ya wale wanaotaka kufanya malipizi makali zaidi. Huu ni Mfungo mkali. Katika ngazi hii ya kufunga watu wengi huaacha kabisa kula na kunywa siku nzima, wakawa na huo mlo mmoja tu. Wanaotaka malipizi makali zaidi siku ya kufunga chakula, asubuhi pokea Ekaristi Takatifu, na wala usiguse chakula au kinywaji chochote kingine. Mchana unaweza kula slesi moja (kipande) tu ya mkate na unywe glasi moja tu ya maji ya kawaida. Jioni pia ule slesi moja ya mkate na unywe glasi moja tu ya maji. Na endapo utaamua kutokula kabisa na kutokunywa kabisa hadi asubuhi kesho yake, itampendeza zaidi Mwenyezi MUNGU. Hii ndiyo toba ya kweli.

Tukumbuke kwamba kile tunachofunga kiwasaidie wasiojiweza. Si kufunga kwa nia ya kuweka akiba ili baada ya mfungo uweze kutumia wewe mwenyewe! La hasha. Huo si mfungo wenye kuleta faida kiroho, bali ni mfungo tasa.

Kuacha kula nyama Ijumaa Kuu na Ijumaa nyingine za mwaka.
Ufungapo au uachapo kula nyama, funga kweli na acha kweli kula nyama kwa dhati kwa toba ya dhambi. Vinginevyo utakuwa unajidanganya mwenyewe. Papo uutolee mfungo wako na kutokula nyama huku kwa Mwenyezi MUNGU, kwamba unafanya hivyo kwa kudhamiria. La sivyo utadhania unafunga na unaacha kula nyama kwa manufaa ya kiroho wakati unashinda tu na njaa ! Kuacha kula nyama maana yake ni kula vyakula vitokanavyo na ardhi tu; ndivyo vyakula vya mfungo. Acha kula kila aina ya nyama, na mafuta yanayotokana na wanyama. Usile nyama, mayai, mafuta ya wanyama, siagi na jibini, wala maziwa. Kula vitu vyovyote vitokanavyo na wanyama au ndege hurahishisha mfungo wako. Kumbuka pia kwamba siku za kufunga na kuacha kula nyama, uwe macho sana, maana shetani mshawishi atakuja kupima utashi wako. Shinda mwili (njaa na kiu) wako, mshinde shetani anyekuongoza dhambini. Jambo la muhimu hasa ni kwamba matendo hayo yote yatendeke kwa ajili ya BWANA. Tuyafanye kama alama ya kwamba tunataka kurudi kwake. Yawe ni matendo kati ya MUNGU na mimi. Kwa sababu hiyo lazima kulinda siri ya jambo lolote tutakalo tenda. “BABA yako aonaye sirini atakujazi.”

Nini thamani na maana ya kujinyima jambo fulani ambalo kimsingi ni zuri na inafaa kwa ajili ya afya ya mwili?

Thamani na maana ya kufunga tunaiona na kupata mfano kwa YESU. Ni vema tukumbuke kwamba Kwaresima inatukumbusha siku 40 za mfungo wa BWANA wetu jangwani, alivyofanya kabla ya kuanza Utume wake hadharani, (Mt. 4:1-2). Pia, kama Musa alivyofunga kwa siku 40 usiku na mchana kabla ya kupokea zile Mbao za Sheria (Kut. 34:28). Eliya naye alifunga kabla ya kukutana na BWANA katika Mlima Horeb (1 Wafal. 19:8), YESU vile vile kwa njia ya sala na kufunga, akijitayarisha kwa ajili ya majukumu yaliyokuwa mbele yake, alituonesha tangu mwanzo mapambano makali dhidi ya Shetani.

Hivyo basi, Maandiko Matakatifu na mafundisho yote ya desturi za ukristo yanafundisha kuwa mfungo ni msaada mkubwa katika kukwepa dhambi na vishawishi vinavyoweza kutupeleka katika dhambi yenyewe. Kwa kuwa kila mmoja wetu anaelemewa na dhambi na mafuatano yake, kufunga kumependekezwa kwetu kama njia ya kurudisha urafiki wetu na MUNGU. Hivi ndivyo alivyofanya Ezra (8:21), walivyofanya watu wa Ninawi (Yona 3:9).

Je, unajua mfungo wa kweli ni upi?
Mfungo wa kweli kama YESU alivyorudia mahali pengi, ni kufanya mapenzi ya Baba aliye Mbinguni, “na BABA yako aonaye sirini, na atakujazi” (Mt. 6:18). Mfungo wa kweli unaelekezwa katika kula chakula cha kweli; yaani “kufanya mapenzi ya MUNGU” (Yn. 4:34).

Hivyo basi, kama katika Kwaresima hii UMEAMUA kweli kusali, basi funga; kama unafunga, onesha huruma; kama unataka maombi yako yasikiwe, sikiliza maombi ya wengine. Endapo hufungi masikio yako kwa wengine, unafungua masikio ya MUNGU kwa ajili yako.

Kwa hakika mfungo unaleta faida za kimwili, lakini kwa Mkristo mfungo upo kwa ajili ya “Tiba” ya kuponya yale yote yanayouzuia mwili kutekeleza utashi wa MUNGU. Pia kufunga ni njia ya kuonesha “huzuni” (1 Sam 31:13; 1 Fal 21:27; Neh1:4); toba (1 Sam 7:6; Yoe 2:12; Dan 9:3-4) au hali ya “unyofu katika maombi” (2 Nya 20:3-4; Ezra 8:23).

Mpenzi msomaji wa kijitabu hiki, nakutakia Kwaresima njema na mfungo wenye heri na toba ya kweli mbele za MUNGU kwa kuleta mabadiliko ya kweli katika maisha yetu ili kufungua mifereji ya neema na baraka katika mtu binafsi, familia na Jumuiya. Tukumbuke kwamba dhambi huzuia baraka na neema toka kwa MUNGU hata kurudisha nyuma maisha yetu ya kiroho na maendeleo katika familia. Hivyo, katika kipindi hiki cha Kwaresima tukitumie kwa kufanya toba ya kweli kimatendo ili kuondoa vikwazo vyote vinavyo zuia maendeleo yetu kiroho na ya kifamilia kwa kuwa tayari kumegwa kuwa chakula kwa wengine kwa njia ya ukarimu wetu. Tujitahidi katika kushiriki Ibada ya Njia ya Msalaba ikichukuliwa katika mtazamo wa kufanya toba na kuomba msamaha kwa MUNGU. Kushiriki Sakramenti vema hasa Sakramenti ya upatanisho ili mfungo, na toba yetu vipate kibali machoni pake MUNGU na kushiriki matakatifu.
MUNGU akubariki na kukulinda. Nakutakia kwaresima njema.

“Wakati umetimia na ufalme wa MUNGU umekaribia, Tubuni na kuiamini Injili.” (Mk 1:16).


NJIA YA MSALABANjia ya Msalaba ni ibada ya Mateso na Kifo cha KRISTO. Tunasafiri naye kiroho kutoka kwenye nyumba ya Pilato hadi Kalvari. Tunakumbuka yote yaliyotukia tangu alipohukumiwa hadi alipozikwa karibuni. Tunafanya ibada hii kwa kuwa karibu na YESU anayeteseka kwa ajili yetu na kuwa karibu na Bikira MARIA Mama wa Mateso. Hivyo, tufikiri juu ya ubaya wa dhambi zetu na kuzijuta na kudhamiria kuziacha kweli. Pili, tufikiri juu ya Fumbo la Mapendo ya YESU kwa BABA yake na kwetu sisi wanadamu. Ibada hii itusaidie kuonja wokovu uliotujia kwa Mateso, Kifo na Ufufuko wa Mkombozi wetu, YESU KRISTO.




Sala mbele ya AltareEe, Mkombozi wangu, ninakuja leo kufuata njia ile uliyoshika siku ya kufa sadaka yetu. Nimetubu dhambi zangu zote; ninataka kugeuza mwendo wangu; ninaomba kwako niwapatie roho za waamini marehemu waliomo toharani, rehema zote zilizotolewa na Kanisa kwa Njia ya Msalaba. Nawe MARIA Bikira Mtakatifu, uliyefuata njia ile nyuma ya mwanao YESU, uniangalie kwa wema, unitie Moyo Mkuu, nisipende dhambi tena, nikivumilia kazi na usumbufu na mateso na matukano yatakayonipata.

**************
Umekosa nini we YESU,/ Kushtakiwa bure kwa Pilato
Wenye kustahili hukumu, Si wewe, si wewe BWANA, ni sisi.

KITUO CHA KWANZA - YESU anahukumiwa afe
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Pilato anamhukumu YESU ingawa haoni kosa lake, anawaogopa Wayahudi. Anabembeleza urafiki wa Kaysari. Ee YESU usiye na kosa, hata mimi ningeweza kutenda mema mengi, lakini naogopa macho ya wenzangu, na maneno yao. Ee BWANA, uniima-rishie utashi wangu, nijitegemee katika kushika madaraka yangu.

BABA yetu… – Salamu MARIA… -Atukuzwe BABA…
K. Ee BWANA, Utuhurumie. W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**************
Ole Msalaba huo mzito, / Apagazwa mwana mpenzi wa MUNGU. / Mwili waenea mateso, / Alipa, alipa madhambi yetu
KITUO CHA PILI - YESU anapokea msalaba
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

YESU anakubali kuelemewa na msalaba kwa ajili ya wokovu wa watu. Ndivyo anavyonifundisha moyo wa sadaka, moyo wa kujitolea na kujisahau kwa ajili ya wengine. Ee YESU wangu mkarimu, mimi pia ninao msalaba wangu: jirani zangu, mwenzangu wa ndoa, watoto, wazazi wangu, kazi zangu, joto, baridi, njaa, kiu, vishawishi, magonjwa na matatizo mengine ya maisha, wajibu wangu kwa MUNGU, kwa umma na kwa Kanisa. Hayo yote ni msalaba. Unipe ukarimu wako ee YESU, niyapokee bila kunung’unika, na kuyabeba vema.

BABA yetu… -Salamu MARIA… -Atukuzwe BABA…
K. Ee BWANA, Utuhurumie. W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**************
Ona Muumba mbingu na nchi, / Yupo chini mzigo wamwelemea, / Na mtu kiumbe chake kwa ukali, / Ampiga, ampiga bila huruma.
KITUO CHA TATU - YESU anaanguka mara ya kwanza
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

YESU amedhoofika sana, anaanguka chini, kisha anasimama, anaendelea na safari ya ukombozi. Ee YESU uliyeanguka chini ya msalaba kwa ajili ya udhaifu, ukasimama tena; usiniache katika tamaa nikianguka dhambini, bali nisimame mara moja, nikufuate.

BABA yetu… -Salamu MARIA… -Atukuzwe BABA…
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**************
Huko njiani we MARIA, / Waonaje hali ya mwanao, / Ni damu tupu na vidonda, / Machozi, machozi yamfumba macho.
KITUO CHA NNE - YESU anakutana na mama yake
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Wote wawili mama na mwanawe wanaumia sana moyoni kwa ajili ya dhambi zangu. Ee YESU, Mwana wa MARIA, unitilie moyoni mwangu upendo na ibada kwa Bikira MARIA; unijalie na ulinzi wake, nisitende dhambi tena.

BABA yetu… -Salamu MARIA… -Atukuzwe BABA…
K. Ee BWANA, Utuhurumie. W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**************
Kwa Simoni heri ya kweli, / Mimi pia YESU nisaidie, / Kuchukua mzigo wa ukombozi, / Kuteswa, kuteswa pamoja nawe.
KITUO CHA TANO - Simoni wa Kirene anamsaidia YESU
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Nausifu ukarimu wa Simoni wa Kirene. Ee BWANA unijalie ukarimu kama huo, niitikie nami wito wa kukusaidia kuchukua msalaba. Nitoe zaka na michango yote ya uenezaji wa dini; nijitolee mimi mwenyewe katika kazi ya maendeleo ya dini. Uwajalie vijana wengi wito wa Upadre, waweze kuchukua msalaba pamoja nawe kwa ajili ya wokovu wa dunia. Uwaimarishe viongozi wa dini. Ustawishe moyoni mwa waamini wote mwamko wa utume.

BABA yetu… -Salamu MARIA… -Atukuzwe BABA…
K. Ee BWANA, Utuhurumie. W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**************
Uso wa YESU Malaika, / Betlehemu walikuabudu, / Bahati yake Veronika, / Kupangusa, kupangusa Mfalme wa Mbingu.
KITUO CHA SITA - Veronika anapangusa uso wa YESU
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Mama huyu ni kinyume kabisa cha Pilato. Veronika anajua analopaswa kutenda, na analitenda bila kujali macho na maneno ya makundi ya watu waovu. Ee YESU, uliyemtuza Veronika zawadi ya picha ya uso wako juu ya kitambaa, unijalie ushupavu na ujasiri wake wa kutenda mema, ili roho yangu ipambwe kwa chapa ya uungwana na utakatifu wako.

BABA yetu… -Salamu MARIA… -Atukuzwe BABA…
K. Ee BWANA, Utuhurumie. W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

Wakimvuta huku na huku, / Wauaji wanamchokesha bure, / Chini wanamtupa bado kwa nguvu, / Aibu, aibu yao milele.
KITUO CHA VII - YESU ANAANGUKA MARA YA PILI
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Ee YESU uliyelegea mno kwa mateso makali, unapoanguka mara ya pili kwa ajili ya udhaifu wa mwili, wanionya kwamba hata mimi naweza kurudi dhambini kwa udhaifu wa moyo. Nipe basi neema ya kuepuka nafasi za dhambi na visa vyenye kunikwaza na kunirudisha dhambini.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amni. Amina.

Wanawake wa Israeli, / Msilie kwa sababu hiyo, / Muwalilie hao kwa dhambi, / Upanga, upanga ni juu yao.
KITUO CHA VIII - AKINA MAMA WANAMLILIA YESU
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Asanteni sana akina mama kwa moyo wenu wa huruma. Ee YESU uliyetulizwa na wanawake, unipe moyo wa kuwaheshimu akina mama wote. Uwaite na wasichana wengi waingie utawa, ili watulize moyo wako Mtakatifu kwa sala na sadaka zao.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

Mwokozi sasa ni ya tatu, / Waanguka chini ya msalaba, / Katika dhambi za uregevu, / Nijue, nijue kutubu hima.

KITUO CHA IX - YESU ANAANGUKA MARA YA TATU
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Ee YESU unayezidi kudhoofika kwa mateso unaanguka mara ya tatu, upate kunistahilia neema ya kuutiisha mwili wangu na kuusulibisha, licha ya kuepuka nafasi za dhambi. Mara nyingi mno ninajibovusha kwa kupenda mno starehe, anasa na tafrija. Ee YESU mwema, nisaidie kuufuata mfano wa Mtakatifu Paulo, niutese mwili wangu na kuutumikisha, ili nipate siku moja tuzo mbinguni.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

Muje Malaika wa Mbingu, / Funikeni mwiliwe kwa huruma, / Vidonda vyake na utupu, / Askari, askari wamemvua.
KITUO CHA X - YESU ANAVULIWA NGUO
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Askari wanamvua kwa nguvu nguo yake, iliyogandamana na madonda yake; wanayaamsha mara moja mateso yote aliyoteswa tangu mwanzo. Ee YESU, unayavumilia mateso makali haya, upate kunifundisha kuuvua kwa nguvu moyoni mwangu urafiki mbaya, au kitu kingine chochote kile kinachoharibu urafiki wa MUNGU, hata ikipasa kutoa sadaka kubwa.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

Hapo MKRISTO ushike moyo, / BWANA wako alazwa msalabani, / Mara miguu na mikono, / Yafungwa, yafungwa kwa misumari

KITUO CHA XI - YESU ANASULIBIWA MSALABANI
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Ee YESU uliyepigiliwa misumari msalabani, nakutolea akili na utashi wangu, vifungwe pamoja na miguu yako, nipate kuwaza, kusema na kutenda siku zote yale tu yanayolingana na utukufu wa msalaba wako Mtakatifu. Ee YESU, mimi ni mfungwa wako. Nisaidie kuimarisha kifungo hicho kwa sala, Sakramenti na fadhila za KiKRISTO.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**********
YESU mpenzi nakuabudu, / Msalabani unapohangaika, / Nchi yatetemeka kwa hofu, / Na jua, na jua linafifia.
KITUO CHA XII - YESU ANAKUFA MSALABANI
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Ee YESU uliyekufa msalabani kwa ajili ya dhambi zangu, unijalie niichukie dhambi, nisiishi kamwe katika dhambi. Nifahamu kwamba nilipobatizwa kwa jina lako, nilibatizwa katika mauti yako ili utu wangu wa kale usulibishwe nawe, mwili wa dhambi uangamizwe nisitumikie tena dhambi.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**********
Mama MARIA mtakatifu, / Upokee maiti ya Mwanao, / Tumemwua kwa dhambi zetu, / Twatubu kwake na kwako.

KITUO CHA XIII - YESU ANASHUSHWA MSALABANI
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Ee YESU uliyeshushwa msalabani baada ya kufa, unijalie nidumu katika maisha ya kujitoa sadaka mpaka siku ya kufa kwangu. Nielewe na kukubali kwamba baada tu ya kufa ndio mwisho wa vita na mashindano ya KiKRISTO.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

Pamoja nawe kaburini, / Zika dhambi na ubaya wa moyo, / YESU tuwe Wakristo kweli, / Twakupa twakupa sasa mapendo.
KITUO CHA XIV - YESU ANAZIKWA KABURINI
- Ee YESU, tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu.

Ee YESU, ulizikwa kaburini, ukafufuka siku ya tatu. Mimi pia nilizikwa pamoja nawe kwa njia ya ubatizo katika mauti yako. Kwa vile wewe ulifufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa BABA, unijalie nami nifufuke, yaani nishike mwenendo mpya, mwenendo wa uzima wa milele.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

**********
Katika roho yangu BWANA, / Chora mateso niliyokutesa, / Nisiyasahau madeni, / Na kazi, na kazi ya kuokoka.(Hiari yako - Mbele ya Altare)

KITUO CHA XV - YESU AMEFUFUKA
- Ee YESU tunakuabudu, tunakushukuru.
- Kwa kuwa umewakomboa watu kwa Msalaba wako Mtakatifu

Habari njema aliyotuletea YESU ni kwamba baada ya kila Ijumaa Kuu huja sikukuu ya Pasaka; kwamba punje ya ngano isipoanguka ikafa, hukaa hali hiyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa maozo mengi. Twakushukuru, ee YESU, kwa mateso yako, lakini twakushukuru hasa kwa ufufuko wako, kwa kuwa huo ndio unaotupa hakika ya kuwa hatukuzaliwa kwa ajili ya mateso na maumivu, bali kwa ajili ya heri ya milele.

BABA yetu -Salamu MARIA -Atukuzwe BABA.
K. Ee BWANA, Utuhurumie W. Utuhurumie.
Roho za waamini wapate rehema kwa MUNGU, wapumzike kwa amani. Amina.

*********
SALA YA MWISHO
Mbele ya Altare: YESU wangu, kwa uchungu wote ulioona juu ya msalaba, na kwa kuzimia kwako kwa ukali wa mateso, unijalie nguvu ya kuvumilia kwa moyo taabu zote sasa na saa ya kuzimia kwangu. Nawe MARIA Mamangu, kwa uchungu wote ambao moyo wako umejaa ulipomwona mwanao mpenzi kuinama kichwa na kuzimia, unifadhili nife kifo chema.

SALA YA KUMWOMBA YESU ALIYETESWA
YESU wangu,/ kwa masikitiko uliyoyaona hata ya kuzimia roho,/ na kwa jasho la damu ulilotoka kwa sababu ya dhambi zangu,/ unitie uchungu wa kweli juu ya makosa yangu! YESU wangu, / kwa msongo wa moyo uliouona kutolewa na Yuda,/ unifanyizie nikae amini kwako,/ nisikutoe bado vile nilivyofanya mpaka leo!/ YESU wangu, uliyefungwa kama mtu mwovu,/ niunganishe nawe kwa vifungo vya mapendo yako! YESU wangu,/ kwa madharau uliyodharauliwa, / na machukizo uliyochukizwa mbele ya Ana,/ Kaifa na Herodi,/ uniwezeshe kuvumilia kwa saburi matukano nitakayotukanwa na watu! / YESU wangu, kwa maumivu uliyovumilia mwilini mwako ulipopigwa fimbo nyingi mno,/ nijalie nguvu ya kustahimili maumivu ya ugonjwa, / na kukataa furaha zote mbaya!/ YESU wangu, /kwa mateso uliyoona ulipotiwa taji la miiba,/ unipe neema ya kutokubali tena mawazo yoyote ya majivuno na ya uchafu!/ YESU wangu, /uliyechukua msalaba wako mzito kwa ajili ya dhambi zangu, / unitie moyo mkuu, / nikubali kwa uvumilivu taabu na sulubu zote za maisha yangu! / YESU wangu, uliyemwaga damu yako yote juu ya msalaba kwa ajili yetu,/ nifanyizie niwe hai kwa ajili yako tu!/ YESU wangu, kwa kiu kikali ulichoona kwa ajili yangu,/ nifanyizie nisikukasirishe tena kwa kupenda mno chakula au kileo!/ YESU wangu, kwa uchungu wote uliouona juu ya msalaba,/ na kwa kuzimia kwako kwa ukali wa mateso,/ nijalie nguvu za kuvumilia kwa moyo taabu zote saa ya kuzimia kwangu!/ Nawe MARIA Mama yangu, kwa uchungu wote ambao moyo wako umejaa / ulipomwona Mwanao mpenzi akiinama kichwa na kuzimia,/ unifadhili nife kifo chema! Amina. 

na Abel Reginald

Monday, February 24, 2014

Waraka kuhusu Elimu Katoliki wazinduliwa mjini Vatican



Majiundo ya majadiliano ya kitamaduni katika shule za Kikatoliki: ili kuishi kwa pamoja utamaduni wa upendo. Ni hati iliyowasilishwa kwa waandishi wa habari mjini Vatican na Viongozi wakuu wa Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki, chini ya uongozi wa Kardinali Zenon Grocholewski

Ni hati ambayo imepitishwa na Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 28 Oktoba 2013, kama kumbu kumbu ya miaka 48 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha hati kuhusu elimu inayojulikana kama "Gravissimum Educationis". Hii ni hati muhimu sana kuwahi kutolewa baada ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Kardinali Grocholewski anasema, mwaka 2015, Kanisa litafanya Jubilee ya Miaka 50 tangu hati juu ya Elimu ilipochapishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa vatican. Kanisa Katoliki limekuwa ni mdau mkubwa katika sekta ya elimu kwani kuna zaidi ya vijana billioni moja wanaopata elimu kutoka katika: shule na taasisi za elimu zinazosimamiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki. Kuna waalimu na wafanyakazi millioni 58 ambao wameajiriwa kwenye shule na taasisi hizi.

Takwimu zinaonesha kwamba, katika kipindi cha Mwaka 2008 hadi mwaka 2011 kumekuwepo na ongezeko kubwa la wanafunzi wanaosoma katika shule na taasisi za Kanisa Katoliki sehemu mbali mbali za dunia. Idadi hii imepungua Barani Ulaya, lakini imeongezeka Barani Afrika, Asia na Oceania. Idadi ya wanafunzi wanaosoma kwenye shule na taasisi za Kanisa katika nchi changa ingeweza kuongezeka, lakini kuna mambo kadhaa ambayo bado yanakwamisha jitihada hizi.

Baadhi ya sababu hizi ni vita, kinzani na majanga asilia. Kuna uhaba mkubwa wa waalimu duniani na kwamba, kuna upungufu wa waalimu millioni 1.7, ili kufikia lengo la kuwa na waalimu wenye sifa na ubora unaotakiwa na UNICEF. Hali hii ni mbaya zaidi Barani Afrika, kwani takwimu zinaonesha kwamba, kuna mwalimu mmoja kwa wanafunzi mia moja!

Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki limeendelea kusaidia kutoa utambulisho wa shule na taasisi zinazoendeshwa na kumilikiwa na Kanisa Katoliki. Kanisa linatambua kwamba, shule na taasisi hizi ni mahali pa ushuhuda wa imani unaowashirikisha, waamini walei pamoja na watawa ambao kwa kiasi kikubwa wanatekeleza utume wao kwenye sekta ya elimu.

Hati hii mpya anasema Kardinali Zenon Grocholewski inagusa kwa karibu zaidi changamoto mbali mbali za mwingiliano wa kitamaduni unaojitokeza kutokana na utandawazi na maendeleo sayansi na teknolojia. Walengwa wakuu wa hati hii ni wazazi na walezi we nye dhamana ya malezi na majiundo kwa watoto wao; waalimu, majaalimu na wafanyakazi ambao kwa pamoja wanaunda Jumuiya ya walezi.

Hati hii ni msaada mkubwa kwa Tume za Mabaraza ya Maaskofu kuhusu elimu pamoja na wadau mbali mbali wanaojihusisha na sekta ya elimu. Hii ni nyenzo ya majadiliano ya kitamaduni inataka kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu; uhuru wa kidini kwa kuzingatia utambulisho wa Kanisa Katoliki. Neno msingi ni majadiliano!

Lengo ni kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kitamaduni katika sekta ya elimu, ili kujenga na kuimarisha utamaduni wa upendo, dhamana inayotekelezwa na Kanisa katoliki katika sekta ya elimu na kama sehemu ya utangazaji wa Injili ya Furaha.

Askofu mkuu Angelo Vincenzo Zani, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la elimu anasema, tema ya majadiliano ni sehemu ya mchakato wa utume unaofanywa na Mama Kanisa katika sekta ya elimu. Hii ni changamoto iliyotolewa na Makardinali kunako Mwaka 2008 kwa kuhamasisha Kanisa kushirikiana na wadau mbali mbali katika sekta ya elimu, ili kuchangia maboresho ya elimu duniani. Kunako mwaka 2008, wawakilishi kutoka dini na madhehebu mbali mbali walichangia kuhusu umuhimu wa elimu katika mwingiliano wa tamaduni.

Baraza likaanza kazi yake kwa baraka na utashi wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kunako mwaka 2011 muswada wa hati hii, ukapitishwa na wajumbe wa Baraza la Kipapa la elimu. Mang'amuzi ya majadiliano ya kitamaduni ni jambo ambalo limeonesha mafanikio makubwa sehemu mbali mbali za dunia.

Kunako Mwaka 2015 Kanisa litaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ulipochapisha Waraka kuhusu elimu. Mwaka huu pia Kanisa litaadhimisha Jubilee ya Miaka 25 tangu Katiba kuhusu elimu ilipochapishwa na kufanya rejea kuhusu vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kusimamiwa na Kanisa Katoliki.

Friday, February 14, 2014

MPANGO KAZI WA VIWAWA PAROKIA YA BOKO 2014


UTANGULIZI
Kwa mwaka 2013, Vijana Parokia ya Boko tulifanikiwa kuyafanikisha matukio yote tuliyokuwa tumejipanga.
Pamoja na ufanisi huo yapo mengi ambayo yalishindwa kufanikiwa kwa asilimia zote na hii nikutokana na hali mbaya ya uchumi kwa Vijana wetu, na chama chetu kwa ujumla.
Kwa Mwaka 2014, Halmashauri ya VIWAWA Parokia imeridhia kupunguza baadhi ya matukio, ili kuweza kuleta ufanisi zaidi.
Kutokana na kutokuwepo kwa mashindo ya Vijana ya Dekania (dekania Cup) na  ya Jimbo (Pengo Cup), Uongozi wa Parokia umeona pia ni vyema kutoa mashindano ya Paroko Cup kwa Msimu huu.
MATUKIO YA MWAKA 2014
1.      Tutakuwa na  Mafungo ya Vijana wote wa Parokia yatakayo fanyika mwanzo wa kipindi cha kwaresima, na Mafungo haya hatafanyikia Mlango wa Imani Bagamoyo. Lengo la mafungo haya ni kuwafanya vijana waweze kuanza kutafakari safari ya Ukombozi wa Mwanadamu kwa Mateso, Kifo na Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo.
2.      Hija ya Vijana jimbo kuu la Dar es salaam itafanyikia Parokia kwetu Juma la nne la kwaresima siku ya Jumamosi.
3.      Siku ya JUMATATU YA PASAKA VIJANA WETU WOTE WA PAROKIA watakutana pamoja kwa ajili ya kusheherekea Ufufuko wake Bwana, hii ikiwa ni pamoja na kushirikishana mambo mbali mbali ya kimaisha.
4.      Mwanzo wa mwezi wa saba tutakuwa na ziara ya UINJILISHAJI JIMBO LA MBULU; Licha ya kwamba mwaka jana tulifanya ziara katika Jimbo hili kwa kutembelea Parokia tatu, bado changamoto za Kiimani ni kubwa sana ambapo sasa jamii ya kule inahitaji elimu zaidi juu ya mambo ya kiimani.
Hivyo kwa mwaka huu tunaenda na ujumbe wa IMANI MSINGI WA KANISA, na kuelimisha kwa kina zaidi juu utume wetu,
Tunatarajia kutembelea Jumla ya parokia nne, kwa ziara hii wenyeji wetu ni Parokia ya Dareda, zaidi ya hayo pia tutapata nafasi ya kutembelea mbuga ya wanyama ya Ngorongoro
5.      Tamasha la Vijana; huu ni utamaduni wetu wa kila mwaka, tamasha la mwaka huu litafanyika mwezi wa nane na litakuwa na semina, michezo ya ndani ambayo ni Maigizo, Ngoma, Kwaya, Nyimbo, Vichekesho na Show mbali mbali, tamasha hili linatarajiwa kufanyika kwa muda wa siku mbili(ijumaa jioni hadi Jumapili baada ya Misa).
6.      Kongamano la Ujirani Mwema (Parokia ya Bunju na Boko) halmashauri ya Viwawa Parokia inatarajia kuandaa kongamano la Ujirani mwema kwa Vijana na Viongozi wa Halmashauri ya Walei wa Parokia hizi, Kongamano hili litafanyika mwezi wa kumi na moja.
7.      Mwisho wa mwaka tunatarajia kuwa na semina ya siku moja kwa vijana wote; Lengo ni kuwakumbusha vijana wajibu wao katika kanisa na jamii kwa jumla.
NB: LIPA ADA YA CHAMA KWA MAENDELEO YA CHAMA CHETU, PIA UNAWEZA KULIPIA ADA ZA USHIRIKI YA MATUKIO YOTE YA VIWAWA KWA MWAKA 2014 KATIKA ACCOUNT YETU YA CRDB TAWI LA TEGETA.
ADA KWA MWEZI NI SHS 2000/= NA KWA MWAKA NI TSHS 24,000/= KWA KILA KIJANA.
ADA ZA USHIRIKI WA MATUKIO YOTE YA MWAKA NI TSHS 276,000/=
ACCCOUNT  NAME:VIWAWA PAROKIA YA BOKO
 ACCCOUNT  NO: 01524526820100


RATIBA HII YAWEZA KUBADILIKI KWA SABABU AMBAZO ZITAKUWA NJE YA UWEZO WETU, MATUKIO HAYA YAKIGONGANA NAYA PAROKIA YAKO ONYESHA UTII, FUATA YA PAROKIA.


TAREHE
TUKIO
WAHUSIKA
MAHALI
19/01/2014
MKUTANO MKUU
VIONGOZI WA VIGANGO, KANDA NA JUMUIYA
BOKO
08/03/2014
MAFUNGO
VIJANA WOTE
BAGAMOYO
16/03/2014
KIKAO CHA HALMASHAURI
VIONGOZI WA VIGANGO
BOKO
29/03/2014
HIJA
VIJANA WOTE
PAROKIANI-BOKO
5-6/04/2014
MAFUNGO
VIONGOZI WA PAROKIA, VIGANGO NA JUMUIYA
CONSOLATA – BUNJU-KIDEKANIA
13/04/2014
MISA YA MATAWI

VIJANA WOTE
DONBOSCO UPANGA
19/04/2014
MATENDO YA HURUMA
VIJANA WOTE
KIJIJI CHA FURAHA MBURAHATI –KIJIMBO
21/04/2014
GET TOGETHER
VIJANA WOTE

01/05/2014
SOMO WA VIWAWA (MT. YOSEPH)
VIJANA WOTE
DONBOSCO –UPANGA-KIJIMBO
11/05/2014
KIKAO CHA HALMASHAURI
VIONGOZI WA VIGANGO
 RAFAEL
08/06/2014
MKUTANO MKUU
VIONGOZI WA VIGANGO, KANDA NA JUMUIYA
BOKO
28-29/06/2014
KONGAMANO LA VIJANA JIMBO
VIJANA WOTE
SEKONDARI YA LOYOLA
01-07/07/2014
ZIARA YA UINJILISHAJI
VIJANA WOTE
JIMBO LA MBULU
20/07/2014
KIKAO CHA HALMASHAURI
VIONGOZI WOTE WA VIGANGO
MBWENI
15-17/08/2014
TAMASHA LA VIJANA
VIJANA WOTE
BOKO
23/08/2014
MAFUNGO
VIJANA  WOTE
BAGAMOYO-KIDEKANIA
21/09/2014
KIKAO CHA HALMASHAURI
VIONGOZI WOTE WA VIGANGO
RAFAEL
01-06/10/2014
KONGAMANO LA VIJANA KITAIFA
VIJANA WOTE
JIMBO LA NJOMBE(KITAIFA)
19/10/2014
KIKAO CHA HALMASHAURI
VIONGOZI WOTE WA VIGANGO
BOKO
15/11/2014
UJIRANI MWEMA
VIJANA BOKO NA BUNJU
BOKO
06/12/2014
SEMINA
VIJANA WOTE

13/12/2014
SEMINA
VIJANA WOTE
ST. GASPER – MBEZI-KIDEKANIA




18/01/2015
MKUTANO MKUU
VIONGOZI WA PAROKIA, VIGANGO NA JUMUIYA
BOKO








NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR