Monday, September 29, 2014

MASOMO YA JUMAPILI TAREHE 28/09/2014 MWAKA" A" WA KANISA

28
 SEPTEMBER
 JUMAPILI YA 26 YA MWAKA "A" 2014.


RATIBA ZA IBADA

KIGANGO CHA BOKO.
IBADA YA MISA YA KWANZA 12:15 – 1:45 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 2:00 – 3:50 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA TATU SAA 4:00-5:20 ASUBUHI
KIGANGO CHA MBWENI.
IBADA YA MISA YA KWANZA 1:15 – 2:55 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 3:00 – 4:50 ASUBUHI
KIGANGO CHA MT. RAFAEL.
IBADA YA MISA YA KWANZA 1:00 – 2:55 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 3:00 – 4:50 ASUBUHI
KIGANGO CHA ANTHONY WA PADUA – MBWENI MPIJI.
IBADA YA MISA NI 3:00 – 5:00ASUBUHI

SOMO  1. Eze. 18:25-28
Bwana ameniambia hivi: Ninyi mwasema; Njia ya Bwana ni sawa. Sikilizeni sasa, Enyi nyumba ya Israeli; je! njia yangu siyo iliyo sawa? Njia zenu sizo zisizo sawa? Mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, atakufa katika uovu huo; katika uovu wake alioutenda atakufa. Tenamtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki, ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi, hatakufa. 

SOMO  2. Flp. 2:1-11


Ikiwako faraja yo yote katika Kristo, yakiwako matulizo yo yote ya mapenzi, ukiwako ushirika wo wote wa Roho, ikiwako huruma yo yote na rehema, ijalizeni furaha yangu, ili mwe na nia moja, mwenye mapenzi mamoja, mwenye Roho moja, mkinia mamoja. Usitende neon lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa na bora kuliko nafsi yake. kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo yake mwenyewe. Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu;ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa binadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.

  INJILI.Mt. 21:28-32


 Yesu aliwaambia wakuu wa makuhanina wazee, Mwaonaje? mtu mmoja alikuwa na wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, mwanangu, leo nenda kafanya kazi katika shamba la mizabibu. Akajibu akasema, Naenda, Bwana;  asiende. Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akijibu akasema, sitaki; baadaye akatubu, akaenda. je! katika hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya babaye? Wakamwambia, Ni yule wa pili. Basi Yesu akawaambia, Amin, nawaambia, watoza ushuru na makahaba wanatangulia mbele yenu kuingia katika ufalme wa Mungu. kwa sababu Yohana alikuja kwenu kwa njia ya haki, ninyi msimwamini; nanyi hata mlipoona, hamkutubu baadaye, ili kumwamini.


Matangazo
jiandaye na Kongamano la ujirani kati ya Parokia ya Boko na bunju' mwema, nunue Ticketi yako sasa kwa Tshs 18,000. Kongamano litafanyika kuanzia tarehe 28-29/11/2014, Parokiani Boko w

 

 

 


Sunday, September 28, 2014

SALA YA KUMWOMBEA MGOJWA


Ee Bwana Yesu Kristo, ulishirikisha ubinadamu wetu kwa hiari yako upate kuwaponya wagojwa na kuwaokoa wanadamu wote.
Sikiliza kwa huruma sala zetu, umjalie afya ya mwili na roho huyu ndugu (taja jina lake) yetu. Mfariji kwa kinga yako, mpe nafuu kwa nguvu yako.
Msaidie atumaini kuokoka kwa njia ya mateso, kama ulivyotufundisha kutumaini hapo ulipoteswa kwa ajili yetu.
Utujalie sisi sote amani na furaha zote za ufalme wako huko unakoishi daima na milele. Amina

Thursday, September 25, 2014

Hawa Wote Walikuwa na sisi na Wengine Bado wapo na sisi Utume wa Viwawa unazidi kusonga mbele




 vijana wa Parokia ya Bunju wakiwa na mlezi wao kipindi hicho 2012 kutoka kushoto ni Getruda, Fr, Paul Malewa, Lucy Linuc

Vijana wa Parokia ya Boko wakiwa kijiji cha furaha mbweni waliposhiriki semina ya siku moja(2012) 


Ruben, Diana na wengine ambao kwa sasa hatujui utume wao wanafanyia wapi
Vijana wa Kigango cha Bunju(kwa sasa Parokia) wakiwa katika ibada ya Matawi 2012 Don Bosco Upanga

Viongozi wa Kigango cha Bunju(kwa sasa Parokia)kutoka kushoto ni Lily Machota na Fredinando
Sister mlezi wa VIWAWA Parokia ya Boko Sir. Sabina

Aliyekuwa Padre Mlezi wa VIWAWA Parokia ya Boko PD. Dominiki Mwaluko kwa sasa ni Paroko Parokia ya Kunduchi
vijana wakitumbuiza kwenye sherehe ya Pentekoste


Monday, September 22, 2014

MASOMO YA DOMINIKA YA TAREHE 21/09/2014, JUMAPILI 25 MWAKA A


21
 SEPTEMBER
 JUMAPILI YA 25 YA MWAKA "A"
2014 


RATIBA ZA IBADA
KIGANGO CHA BOKO.
IBADA YA MISA YA KWANZA 12:15 – 1:45 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 2:00 – 3:50 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA TATU SAA 4:00-5:20 ASUBUHI
KIGANGO CHA MBWENI.
IBADA YA MISA YA KWANZA 1:15 – 2:55 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 3:00 – 4:50 ASUBUHI
KIGANGO CHA MT. RAFAEL.
IBADA YA MISA YA KWANZA 1:00 – 2:55 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 3:00 – 4:50 ASUBUHI
KIGANGO CHA ANTHONY WA PADUA – MBWENI MPIJI.
IBADA YA MISA NI 3:00 – 5:00ASUBUHI

SOMO  1. isa. 55:6-9
Mtafutuni Bwana, maadamu anapatikana,
Mwiteni, maadamu anapatikana,Mwiteni, maadamu yu karibu;
Mtu mbaya na aache njia yake,
Na mtu asiye haki aache mawazo yake;
Na amrudie bwana. naye atamrehemu;
Na arejee kwa Mungu wetu,
Naye atamsamehe kabisa.
maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana. Kwa maana kwa vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.
SOMO 2.Flp.1:20-24,27
Kristo ataadhimishwa katika mwili wangu; ikiwa kwa maisha yangu, au ikiwa kwa mauti yangu. Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida. Ila ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua silitambui. Ninasogwa katikati ya mambo mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo; maana ni vizuri zaidi sana; bali kudumu katika mwili kwahitajiwa zaidi kwa ajili yenu. Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo.
INJILI. Mt. 20:1-16
Yesu aliwaambia wanafunzi wake: ufalme wa mbinguni umefanana na mtu mwenye nyumba, aliyetoka alfajiri kwenda kuajiri wakulima awapeleke katika shamba lake la mizabibu. Naye alipokwisha kupatana na wakulima kuwapa kutwa dinari, aliwapeleka katika shamba lake la mizabibu. Akatoka mnamo saa tatu, akaona wengine wamesimama sokoni wasiokuwa na kazi; na hao nao akawaambia, Enendeni nanyi katika shamba langu la mizabibu, na iliyo haki nitawapa. Wakaenda. Akatoka tena mnamo saa sita na saa kenda, akafanya vile vile. Hata kama saa kumi na moja akatoka, akakuta wengine wamesimama, akawaambia, Mbona umesimama hapa mchana kutwa bila kazi? Wakamwambia, kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri. Akawaambia, enendeni nanyi katika shamba la mizabibu. Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia msimamizi wake, waite wakulima, uwalipe ujira wao, ukianzia wa mwisho hata wa kwanza. Na walipokuja wale wa saa kumi na moja,walipokea kila mtu dinari. Na wale wa kwanza walipokuja, walidhani kwamba watapokea zaidi; na hao pia wakapokea kila mtu dinari. Basi wakiisha kuipokea, wakamnng’ukia mwenye nyumba, wakisema, Hao wa mwisho wametenda kazi ya saa moja tu, nawe umewasawazishia na sisi tuliostahimili taabu na hari za mchana kutwa. Naye akamjibu mmoja wao, akamwambia, Rafiki, sikudhulumu; hukupatana nami kwa dinari? Chukua iliyo yako, uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema? vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho.

Sunday, September 21, 2014

KWANINI UFUNGE NDOA

“Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—MHUBIRI 4:12.
JE, UNAPENDA kwenda kwenye harusi? Wengi wanapenda, kwa sababu mara nyingi hizo huwa pindi zenye kufurahisha sana. Bwana na bibi-arusi wanavalia mavazi yenye kupendeza kwelikweli. Zaidi ya hilo, nyuso zao zinaonyesha kwamba wana shangwe nyingi! Siku hiyo, wana furaha nyingi na inaonekana wana matazamio mengi mazuri ya wakati ujao.
2 Hata hivyo, ukweli ni kwamba ndoa nyingi leo ziko mashakani. Ingawa tunawatakia mema wenzi wapya wa ndoa, nyakati nyingine tunajiuliza: ‘Je, ndoa hii itakuwa na furaha? Itadumu?’ Majibu ya maswali hayo yanategemea ikiwa mume na mke wanaamini na kutumia shauri la Mungu kuhusu ndoa. (Methali 3:5, 6) Wanahitaji kufanya hivyo ili waendelee kukaa katika upendo wa Mungu. Acheni tuchunguze majibu ya Biblia kwa maswali haya manne: Kwa nini ufunge ndoa? Ikiwa utafunga ndoa, utachagua mwenzi wa aina gani? Unaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya ndoa? Na ni nini kinachoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa waendelee kuwa na furaha?
KWA NINI UFUNGE NDOA?
3 Watu fulani wanaamini kwamba siri ya kuwa na furaha ni kufunga ndoa na kwamba huwezi kamwe kutosheka au kuwa na furaha maishani ikiwa huna mwenzi wa ndoa. Hilo si kweli hata kidogo! Yesu, ambaye alikuwa mseja, alisema useja ni zawadi, naye aliwahimiza wale wanaoweza waupe nafasi. (Mathayo 19:11, 12) Mtume Paulo pia alizungumzia faida za useja. (1 Wakorintho 7:32-38) Hata hivyo, Yesu na Paulo hawakuweka sheria kuhusu jambo hilo; na ‘kukataza kufunga ndoa’ ni ‘fundisho la roho waovu.’ (1 Timotheo 4:1-3) Lakini wale wanaotaka kumtumikia Yehova bila kukengeushwa wanaweza kufaidika kwa kuendelea kuwa waseja. Basi, si jambo la hekima kufunga ndoa kwa sababu ndogo-ndogo, kama vile kufunga ndoa kwa sababu tu wenzako wamefunga ndoa au kwamba wanakutia moyo ufanye hivyo.
4 Kwa upande mwingine, je, kuna sababu nzuri za kufunga ndoa? Ndiyo. Ndoa pia ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, inatimiza mambo fulani mazuri na inaweza kuleta furaha. Kwa mfano, ndoa nzuri ndio msingi bora wa maisha ya familia. Watoto wanahitaji kulelewa katika mazingira yanayofaa wakiwa na wazazi wanaowapenda, wanaowatia nidhamu, na kuwapa mwongozo. (Zaburi 127:3; Waefeso 6:1-4) Hata hivyo, kusudi la ndoa si kupata na kulea watoto tu.
5 Fikiria andiko la msingi la sura hii pamoja na mistari inayotangulia: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake. Lakini itakuwaje kwa yule aliye peke yake akianguka wakati ambapo hakuna mwingine wa kumwinua? Tena, wawili wakilala pamoja, watapata joto; lakini aliye peke yake anawezaje kupata joto? Na mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—Mhubiri 4:9-12.
6 Andiko hilo linazungumzia hasa faida ya urafiki. Bila shaka, ndoa ni muungano wa marafiki wa karibu zaidi. Kama andiko hilo linavyoonyesha, katika muungano huo wenzi wa ndoa wanaweza kupata msaada, faraja, na ulinzi. Ili kifungo cha ndoa kiwe imara zaidi, mengi zaidi yanahitajika. Kamba yenye nyuzi mbili, kama mstari huo unavyodokeza, inaweza kukatika. Lakini kamba yenye nyuzi tatu zilizosokotwa au kufumwa pamoja haikatiki kwa urahisi. Lengo kuu la mume na mke linapokuwa kumpendeza Yehova, ndoa yao ni kama kamba yenye nyuzi tatu. Kwa kuwa Yehova anahusishwa kabisa, ndoa hiyo inakuwa muungano imara sana.
7 Pia, katika ndoa ndipo tu tamaa za ngono zinaweza kutoshelezwa inavyofaa. Ni katika kifungo hicho tu ambapo mahusiano ya kingono huonwa kwa kufaa kuwa chanzo cha shangwe. (Methali 5:18) Hata baada ya mtu kupita kipindi ambacho Biblia inakiita “upeo wa ujana”—wakati ambapo tamaa za ngono huanza kuwaka—huenda bado akahitaji kuzuia tamaa hizo. Zisipozuiliwa, tamaa hizo zinaweza kumwingiza katika mwenendo mchafu au usiofaa. Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuwapa watu ambao hawajafunga ndoa shauri hili: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.”—1 Wakorintho 7:9, 36; Yakobo 1:15.
8 Hata kuwe na sababu gani za kufunga ndoa, mtu anapaswa kuona mambo kihalisi. Kama Paulo alivyosema, wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Watu waliofunga ndoa hupata matatizo fulani ambayo waseja hawapati. Hata hivyo, ukiamua kufunga ndoa, unaweza kufanya nini ili upunguze matatizo na kuwa na furaha zaidi? Njia moja ni kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima. Etaendelea

Tafakari ya Neno la Mungu Domonika ya 25 ya Mwaka A,

Mpendwa, tunatafakari masomo ya Jumapili ya 25 ya mwaka wa A wa Kanisa, tukialikwa kuwa na matumaini daima katika kumtafuta Bwana na kutambua kuwa wema wa Mungu ni wa milele kwa watu wote na fikra zake ni tofauti na fikra za kibinadamu. Katika somo la kwanza Waisraeli wako utumwani Babeli kwa sababu hawakutii mausia ya Bwana na zaidi wanaona hawawezi kusamehewa dhambi zao, wamepoteza tumaini na wanaona kana kwamba Mungu amewatupa na kuwaacha kabisa. Zaidi ya hilo wanaongeza kosa jingine tena la kumwona Mungu anayefikiri kama wao, wanafikiri hawezi kuwasamehe tena.


Mpendwa, katika shida yao hiyo Mungu anamtuma Nabii Isaya awaambie kuwa fikra na njia za Mungu ni za juu mno ni tofauti na fikira za kibinadamu kiasi kwamba si rahisi kuzielewa. Zaidi ya hilo Isaya anawakumbusha kuacha njia zao mbaya na kumrudia Bwana. Kumrudia Bwana si tu kuacha dhambi, bali pia kubadili namna ya kumtazama Mungu, Mungu aliye haki na mkamilifu. Mawazo haya yatajitokeza waziwazi katika Injili ambapo tunaona Mungu anayewapenda wote wadhambi kwa wema.


Mtume Paulo akikoleza ujumbe wa nabii Isaya anawaambia Wafilipi, hata kama kuna shida katika maisha yao watambue kuwa kuishi kwao ni Kristu, ndiyo kusema la maana katika maisha yao ni Kristu mfufuka. Mara kadhaa watu wapatapo shida huanza manunguniko dhidi ya Mungu na kusahau kwamba yote waliyonayo yametoka kwake. Wanasahau kuwa, kwa njia ya msalaba yaani njia ya mateso, Kristu ametustahilisha kwenda mbinguni. Ndiyo kusema, hata sisi tuliodhaifu tunapaswa kupitia njia ya mateso ili kuweza kufika Mbinguni. Kwa hakika mtume Paulo anapoandika barua hii kwa Wafilipi yuko katika wakati mgumu yaani kuchagua kufa ili akae na Kristu au kuendelea kuhubiri Injili kwa mataifa, na mwisho anaona ahitimishe fikra zake akisema kuishi kwangu ni Kristu na kufa ni faida. Hapa tunaonja imani ya Paulo ilivyozama katika Mwana wa Mungu.

Tujiulize je kwetu sisi kuishi na kufa, twaweza kuvipokea kama alama ya ushindi katika imani kama Mtume Paulo? Mpendwa msikilizaji jitafiti na hivi unapokuwa umechoka, unapokuwa umefikia mwisho wa maisha yako uweze kusema nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza na imani nimeilinda sasa kufa kwangu ni faida na kuishi kwangu ni Kristu!


Mpendwa mwana wa Mungu tukiongozwa na mwinjili Mathayo, tunapata kuonja kuwa mawazo ya Mungu ni ya juu sana kuliko yetu. Jambo hili linajionesha wazi katika Injili ya leo pale ambapo Bwana wa shamba anawaajiri watu mbalimbali katika masaa tofauti na mwishoni anawalipa ujira sawa. Mpendwa katika hali ya kawaida, Bwana huyu angepaswa kuwalipa tofauti kwa maana muda wa kazi ulikuwa tofauti. Kuwalipa ujira sawa pia ni namna ya kusema kuwa uvivu uendelee katika ulimwengu, tuseme hakuna ile haki ya kawaida yaani common justice! Hii ni namna yetu ya kufikiri na hata namna ya watu wa wakati huo, lakini je Mwinjili anataka kutuambia nini? Je Bwana afikiri kama sisi?


Kwa hakika kuwalipa ujira sawa maana yake, wema wa Mungu ni kwa ajili ya wema na wabaya. Wale walioajiriwa kwanza ndio walisadikiwa kuwa wema na wale wa baadaye ndio kundi wakilishi la walio wabaya. Pamoja na hilo kuna jambo jingine jema, kwamba mwenye shamba anapenda kila mmoja afanye kazi, asiishi bila wajibu, ajisikie katikati ya jumuiya ya watu kwa maana kazi huleta heshima. Kwa jinsi hiyo kazi ya wokovu inaendelea na inawaletea heshima watu wote.
Mfano huu wa mwenye shamba unatufundisha kuwa Mungu si mhasibu wala meneja anayewalipa watu kulingana na jasho lao tu, bali kulingana na upendo wake aliokusudia tangu alipoumba ulimwengu. Hatuna uwezo wa kupata stahili yoyote toka kwa Mungu kwa nguvu zetu bali kwa uweza wake, huruma yake na mapendo yake ya milele. Kwa wazo hili tunarudi kwa nabii Isaya anayetuambia kuwa njia zake ni za juu mno na mawazo yake hatuwezi kuyafikia. Tunaalikwa kutambua kuwa wokovu si kwa maveterani peke yao bali hata vijana wanaokuja saa kumi na moja jioni! Hakutakuwa na upendeleo wowote katika wokovu cha msingi ni kumtafuta Bwana madamu anapatikana. Tumsifu Yesu Kristu.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya Cpps

Wednesday, September 17, 2014

MAHUSIANO KABLA YA NDOA

Katika ulimwengu, mahusiano ya karibu ya kimwili kabla na nje ya ndoa yanakubalika, na hata kushabikiwa. Vipindi vya uchumba vinahesabika kama nyakati za wahusika hao wawili kuona kama ‘wanafaana’. Hili mara nyingi linawapelekea katika kuwa na mahusiano ya karibu ya kimwili.
Inasikitisha kwamba katika makanisa mengi vijana wanauiga mtindo huu huu, na wale walio katika nafasi za mamlaka – uongozi wa kanisa, wazazi, nk., hawashughuliki na hili suala kwaumakiniunaohitajika.Vijanawanaachiwa kujiamulia wenyewe mipaka katika hili suala nyeti, badala ya kupewa miongozo ya Kibiblia iliyo wazi.
Hebu tuwe wazi tokea mwanzo ya kwamba Mungu hachanganyikani; Neno lake halijaficha jambo. Ndani mwake, tunaona maono na mpango wake vilivyo dhahiri, kwa watu wake na Kanisa lake. Ni wazi kwamba hataki tujichanganye na ulimwengu na njia zake. Na wala Mungu hataki sheria na kuhukumiana Kanisani mwake, ambavyo havina nguvu yoyote ya kumbadilisha mtu. Anachotaka ni Wakristo wote wahakikishwe na Roho Mtakatifu kuhusu dhambi kupitia Injili ya Yesu Kristo ambayo inaweka mpaka ulio wazi na kutuonyesha tunapaswa tusimame juu ya msingi upi. Hii ndiyo maana ninaamini tunapaswa kurejea kwenye msingi – Neno la Mungu – ili tuone anasemaje juu ya hili suala.
MIILI YETU NI VIUNGO VYA KRISTO
Hebu tuangalie Mungu anavyoiona ndoa na mahusiano nje ya ndoa, na tutaona ya kwamba uhusiano wowote wa kimwili nje ya ndoa, uwe wa aina yo yote ile, unahesabika kuwa ni dhambi machoni pa Mungu. Si suala la ‘Tuweke wapi mipaka?’ kwa sababu tukijaribu kuweka mipaka ya aina yoyote, tutaivuka tu. Ni kama lile tangazo la breki za magari lisemavyo, “Usianzishe jambo ambalo hutaweza kulizuilia!”

1 Wakorintho 6:15 inasema: “Je, hamjui ya kuwa miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo vya kahaba? Hasha!” Kwa hivyo, si roho zetu tu zilizounganika na Kristo; nafsi yetu yote ni mmoja naye. Mistari ya 16 – 17 inasema, “Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, ‘Wale wawili watakuwamwilimmoja.’Lakiniyeyealiyeungwa na Bwana ni roho moja naye.”
Paulo hapa anasema waziwazi ya kwamba ni lile tendo la ndoa linalowaunga watu kuwa mwili mmoja, na hili linapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Katu hatupaswi kusahau ya kuwa roho zetu, nafsi zetu na miili yetu imeungwa pamoja na Kristo. Siku hizi Wakristo wengi wanafanya wanavyopenda na miili yao, pasipo kutambua madhara ya rohoni yanayotokana na matendo yao. Kwenye kifungu hiki Paulo anaweka utofauti kati ya dhambi ya mwili na dhambi nyingine; katika zinaa unatenda dhambi dhidi ya mwili wako kwa sababu unafanyika kuwa mmoja na yule mnayeunganika naye kimwili. Uzinzi ni uhusiano wowote wa kimwili nje ya ndoa. Uongo, wizi, hasira, nk. ni tofauti; haya ni matunda ya tamaa zetu za kimwili.
Ikiwa Mungu aliamua kuweka utofauti kati ya dhambi katika miili yetu na dhambi nyingine, tunapaswa kuwa makini sana, na kuufahamu moyo wake katika hili suala. Msitari wa 18 unasema, “Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake; ila yeye afanyaye zinaa hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe.” Hatupaswi kusahau ya kuwa miili yetu pamoja na roho zetu vimeungwa na Kristo, na tunapotenda zinaa ni jambo zito sana machoni pa Mungu. Mistari ya 19-20 inatukumbusha ya kuwa mwili wetu ni hekalu la Roho Mtakatifu, na tunahimizwa, “mtukuzeni Mungu katika miili yenu.”
MWILI UNAPASWA KUSULUBIWA
Katika Wagalatia 5:24-25, Paulo anasema, “Na hao walio wa Kristo wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.” Kila Mkristo ana uelewa fulani wa maana ya haya Maandiko. Lakini kwa wale wanaotamani kutembea rohoni, na wako tayari kuoa au kuolewa, yana maana zaidi maishani mwao.

Tumeitwa kuisulubisha miili yetu na tamaa zake. Hii ndio maana tunahitajika kuusikia ujumbe wa Msalaba kila wakati kwa sababu unatukumbusha kujikana nafsi zetu na kuyapoteza maisha. Hakuna nafasi ya kudanganyana, wala kujaribisha mambo… Sisi ni watu waliochaguliwa ambao miili yetu ni mali ya Bwana Yesu Kristo.
Iweje, basi, tuwaze ya kuwa ni sahihi kwa watu wawili waliochumbiana rasmi au vinginevyo, kufanya mambo wanayoruhusiwa kufanya tu mume na mke, eti kwa kuwa wamefikia uamuzi wa kuwa wenza? Uamuzi wa watu wawili wa kuoana huko mbeleni unapaswa umaanishe ya kwamba wataheshiminiana kwa utimilifu mbele za Bwana. Hadi siku ya kuoana, Bwana anawataka waishi maisha safi na matakatifu.
Vijana, sikilizeni… isipokuwa una uhakika moyoni mwako ya kuwa uhusiano umeanzishwa na Mungu, usithubutu kuuingia. Ukitaka kuufahamu mpango wake, na mtu aliyekuandalia kuwa mwenzi wako, fahamu ya kuwa atakufunulia.
Mkishafahamu ya kuwa ni mpango wa Mungu muoane, na ikiwa mnafahamu maisha ya utakatifu mnayopaswa kuishi kabla ya harusi, hakuna hatari. Mnaweza mkachumbiana na kutiana moyo katika kuheshimiana, kwa sababu mmehakikishiwa mioyoni mwenu ya kuwa mnapaswa kuishi maisha matakatifu mbele za Bwana hadi mtakapooana. Utakuwa na kicho kitakatifu cha uwepo wa Mungu katika maisha ya mwenzi wako na kufanyika kielelezo kwa wengine.
Ndio maana unapaswa uthibitike katika kile Mungu anachosema, ili pasiwepo na kubahatisha. Je, kuna mahusiano ya aina yoyote ya kimwili kabla ya ndoa yanayokubalika? Hasha! Neno la Mungu liko wazi sana juu ya hili suala.
MANUKATO YA UHUSIANO SAFI NA MTAKATIFU
Labda tayari uko katika uhusiano wa kimwili nje au kabla ya ndoa, na Bwana anakunenea ya kwamba si sahihi. Ushauri wangu ni kwamba utubu na ufanye uamuzi imara wa kuacha mahusiano yote ya kimwili mara moja; na usigeuke nyuma. Si jambo ambalo linafanyika hatua kwa hatua, wala si jambo la kuchukulia kwa wepesi. Neema ya Mungu ipo kukusaidia. Na ikiwa ninyi wawili mnafahamu mioyoni mwenu ya kuwa mmeandaliwa kuoana, basi jitunzeni hadi siku hiyo, mheshimiane kama vile ndugu wa kiume anavyomheshimu ndugu wa kike kanisani, na katika kufanya hivyo muishi maisha matakatifu na safi. Injili ya Msalaba wa Yesu Kristo inaleta jawabu kwa, na kuchora msitari ulio wazi katika kila jambo tunalokabiliana nalo maishani mwetu. Inatusaidia kuenenda katika uhakikisho, na kwa maana hiyo tunatembea katika ushindi. Wakristo wa kila rika, walio kwenye ndoa na ambao wako bado, wanahitajika wasikilize kwa umakini kile Mungu anachosema katika Neno lake ili waweze kuishi maisha matakatifu na kufanyika vielelezo kwa wengine. Je! si ni jambo la utukufu moyo wako unapokushuhudia ya kuwa kuna hali ya usafi katika uhusiano wa ndugu wanaotaraji kufunga ndoa? Hili linaleta harufu nzuri ya manukato inayopendeza. Je, ni ushuhuda wa jinsi gani wa nguvu ya Injili watu wawili wanapooana juu ya huu msingi!

Ninaamini huu ndio mpango wa Mungu kwa Kanisa lake na kwa watoto wake. Hakuna haja ya kukata tamaa. Mungu yu hai; anaweza kuleta watu wawili pamoja. Anajua ya mbeleni. Anajua kila kitu kuhusu maisha yetu, na shauku yake ni sisi tuishi maisha safi na matakatifu. Ndio maana ni heri kusubiri, kuliko kujaribisha mambo. Fungua moyo wako; mwache Mungu azungumze na wewe na akushawishi. Kwa Yesu Kristo hakuna kuchelewa. Leo inaweza ikawa siku yako ya kumtangazia Bwana ya kuwa unaenda kuishi maisha yako ya Ukristo kabla ya ndoa kwa kulifuata Neno lake.

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR