Saturday, January 10, 2015

Neno la Mungu, Siku kuu ya Ubatizo wa Bwana jumapili ya tarehe 11/01/2015

Mpendwa mwana wa Mungu, tuko tena pamoja katika ile habari ya furaha ndiyo kushirikishana mapendo ya Mungu kwa njia ya Neno lake. Leo ndipo tunahitimisha kipindi cha Noeli kwa Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana na tunaanza kipindi cha kawaida cha mwaka wa Kanisa. Kumbe leo pia ni Dominika ya kwanza ya kipindi cha Mwaka wa Kanisa.

Katika somo la kwanza Nabii Isaya anatupeni habari juu ya mtumishi wa Mungu ambaye anapokea Roho wa Mungu na kazi yake itakuwa kuwahukumu mataifa kwa haki. Ni nuru na mwanga kwa mataifa. Sifa yake nyingine ni mtulivu na mnyenyekevu na hakati tamaa kwa maana mkono wa Mungu uko juu yake. Mtumishi huyu anakabidhiwa Roho wa Mungu kwa sababu ya kazi ya kimungu ambayo ni kujenga amani na kuunganisha vilivyovunjika.

Kadiri ya Injili ya Luka 4: 18-19 mtumishi huyu ni Yesu Kristu. Anakuja kwa ajili ya kutangaza mwaka wa Bwana ambapo wafungwa na vipofu wataondolewa katika shida zao. Kristu amekwisha fika kwetu kazi yetu sasa ni kupokea ujumbe wake. Namna ya kupokea ujumbe ni kuitika kwanza ule mpango wa Yohane Mbatizaji na Isaya wa kutengeneza njia ya Bwana, kuondoa visiki na mabonde. Tunapaswa kufanya hivyo kwa sababu tunasikia kuwa huyu ajaye hatumii nguvu bali upendo na hivi anahitaji ushirikiano. Kwa jinsi hiyo ni kuweka ubatizo wetu katika matendo.

Mtume Petro akielewa vema nia na mpango wa Mungu anasimama kama tusomavyo katika kitabu cha Matendo ya Mitume na kusema hakika Mungu hana upendeleo cha msingi ni kufanya bidii ya kumcha Bwana. Oneni jinsi ambavyo neno la Mungu linavyopiga kasi, anasema Mtume Petro, si tu kwa Wayahudi bali kwa ajili ya wote. Lakini kwa nini fundisho hili?, Ni kwa sababu kulikuwa na upinzani dhidi ya ubatizo wa wapagani. Kumbe Mtume Petro anasema, Kristu mpakwa mafuta wa Bwana amepiga kazi ya kichungaji baada ya kutiwa mafuta na Roho wa Bwana bila kubagua. Ni fundisho kwetu kujiimarisha katika utume na kuimarisha umoja kamili na watu wote milki ya Mungu. Toeni bure kwa maana mmepewa bure.

Katik Injili ya Marko tunapata fundisho la unyenyekevu wa Yohane Mbatizaji na unyenyekevu wa Kristu. Yohane Mbatizaji anakiri udogo wake ambao ni wa chini kabisa. Maana hata kushindwa kushika gidamu ya viatu vya Yesu Kristo. Anatufundisha moja kwa moja kuwa safari ya kumpenda Mungu yatudai kushuka mpaka sakafuni. Mkombozi mwenyewe pia ni kielelezo kingine cha hali ya juu kuhusu unyenyekevu. Anajishusha kwanza na anakuwa mtu, kana kwamba hiyo haitoshi anaamua kubatizwa wakati hana doa la dhambi. Anatufundisha kujishusha kukaa pamoja na wadhambi, maana tunabatizwa ili kuokolewa katika uvuli wa dhambi ya asili kwanza na kuweza kupokea neema za Mungu.

Bwana anapobatizwa yafaa tuangalie mambo yaliyo tokea. Jambo la kwanza ni kupasuka kwa mbingu, ambalo linatupa habari ileile ya Nabii Isaya katika Dominika za majilio. Nabii anauliza mbona umetufanya tukose kukutii? Mbona umetuacha hata tukasahau kukucha wewe Bwana? Is. 63:15-19. Isaya anauliza haya maswali kwa maana ni kama hakuna upatano kati ya mbingu na nchi. Sasa tendo la kupasuka kwa mbingu ni ishara ya mapatano kati ya mbingu na nchi na mpatanishi ni Kristu katika uwezo wa Utatu Mtakatifu.

Jambo la pili ni alama ya njiwa, alama hii yatukumbusha kile kilichotokea wakati wa mafuriko ya Nuhu. Wakati huo mbingu na dunia vilifungwa na njiwa alipotokea akiwa na tawi la mzeituni ilimaanisha kuwa amani imerejeshwa. Ndiyo kusema kwa ishara ya njiwa kuna amani, ni Roho Mtakatifu afanyaye kazi katika Yesu Kristu chanzo cha amani. Mpendwa jambo la pili kuhusu njiwa katika agano la kale alimaanisha nguvu waliyopewa Manabii na hivi Kristu waziwazi ana nguvu hiyo kwa ajili ya kutenda kazi ya Mungu.

Sauti kutoka juu yamaanisha kuwa Kristu ni wa juu na pia Mungu anaongea na watu wake kwa njia yake aliye mwanae mpenzi. Mpendwa msikilizaji yafaa kukumbuka pia jambo jingine nalo ni lile la Joshua anapowavusha wana wa Israeli pale Jordani, anapovuka mto anapokea Roho wa Mungu ili apate nguvu ya kuwafikisha salama katika nchi ya ahadi. Ni katika mantiki hiyohiyo Masiha anapotoka majini Roho wa Mungu anashuka juu yake ili awaongoze wana wa Mungu katika uhuru na kweli ili wafike mbinguni. Watu wanaoongozwa na Bwana kuelekea kwenye uhuru na kweli ndo sisi, wajibu wetu ni kusikia sauti ya mchungaji mwema. (Yn. 10)

Mpendwa ninakutakieni heri na baraka tele katika sikukuu ya ubatizo wa Bwana na nakuomba usisahau wajibu wako ulioupokea kwa njia ya ubatizo, na kwa namna hiyo utakuwa unasherehekea pia ubatizo wako kila siku ya maisha yako.
Tumsifu Yesu Kristo.

SHIRIKA LA DAMU TAKATIFU LAPATA MASHEMASI WAPYA WANNE

Leo Jumamosi, tarehe tarehe 10 Januari 2015 Askofu msaidizi Titus Mdoe wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, ametoa  Daraja la Ushemasi kwa Watawa wanne wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, C.PP.S., Ibada iliyoadhimishwa kwenye Parokia ya Mtakatifu Nicholaus, Kunduchi, Mtongani, Jimbo kuu la Dar es Salaam.

Hawa ni Majandokasisi waliohitimu masomo yao ya falsafa na taalimungu na tarehe 9 Januari 2015 wamepokelewa rasmi kuwa ni Wamissionari wa Shirika la Damu Azizi ya Yesu, katika Ibada iliyoongozwa na Mheshimiwa Padre Reginald Mrosso, C.PP.S. Mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania.

Yafuatayo ni mahubiri aliyoyatoa katika Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuwapokea Frt. Lauriano Januari Mushi, Innocent Emmanuel Miku, John Eleuteri Mlay pamoja na Emmanuel Joseph Makusaro kuwa Wamissionari. Ibada hii imefanyika kwenye Parokia ya Mtakatifu Nicholaus, Kunduchi, Mtongani, Jimbo kuu la Dar es Salaam.

Read More
Katika barua yake kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa uliozinduliwa Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio Nov. 2014 na unaotarajiwa kufungwa rasmi tarehe 2 Feb. 2016, Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni sanjari na Siku ya Watawa Duniani, Baba Mtakatifu Francisko anaanza na maneno haya; napenda kusema neno moja kwenu na neno hilo ni furaha. Popote walipo watawa, ipo pia furaha. Wale wote waliosikia sauti ya Bwana wanaalikwa kufurahi: wimbo wetu wa katikati leo unatualika tufurahi kwa sababu sisi ni watu wa ufufuko na watu wake Mungu – Zab. 95: kwa sababu dunia imeuona wokovu wa Mungu. Ninyi vijana wapendwa mko hapa kwa sababu mnaamini katika huo ufufuko, katika huo uzima wa milele wa kimungu.

Leo tunamshukuru Mungu kwa sababu ndugu zetu hawa wamefikia hatua hii kubwa katika maisha yao ya wito na ya Kanisa kwa ujumla katika kumtumikia Mungu na watu wake. Tunasoma maneno haya katika - Zab. 100:3 – jueni kwamba Bwana ndiye Mungu, ndiye aliyetuumba, nasi tu watu wake, taifa lake na kondooo wa malisho yake. Ufahamu huu ni muhimu sana katika maisha ya mwanadamu ye yote. Ni chanzo cha wito mbalimbali katika maisha ya kawaida na katika kanisa. Ye yote yule anayetambua Mungu ni nani, atapata mwelekeo wa kimungu katika maisha yake. Asiyetambua hilo, hupoteza mwelekeo wa kimungu katika maisha yake.

Mtume Paulo katika - 1 Tim. 6:15-16 – anaandika hivi – wakati wake mwenye heri atalidokeza tokeo la yeye aliye peke yake mtawala, Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana, Yeye peke yake hawezi kufa. Amekaa katika mwanga usiosogeleka. Hakuna mwanadamu aliyemwona, wala awezaye kumwona. Heshima na enzi ya milele ni yake. Amina. Tunaona kuwa ufalme na utawala wa kweli ni wake.

Ufahamu huu unatupelekea kutambua kuwa tumeitwa kumtumikia yeye tu na si kitu kingine cho chote kile – Mt. 4:10 – Yesu akamwambia, nenda zako shetani, kwa maana imeandikwa– umwabudu Bwana Mungu wako, ukamtumikie yeye peke yake. Na katika Kumb. 6:13 – ndiye Bwana Mungu wako utakayemwogopa, ndiye utakayemtumikia na kuapa kwa jina lake.

Somo la kwanza toka Nabii Isaya – “Injili ya Ufalme wa Mungu” - mwandishi anaandika neno hili wakati Waisraeli wamekuwa huru toka Babeli - linaelezea habari ya ukombozi. Waisraeli wanatoka katika utumwa. Wanafurahi. Nanyi pia tafakarini sana hali yenu – mjiweke huru kwa ajili ya Mungu. Yule aliyeufahamu ukombozi wa Mungu, anajiweka huru kwa ajili yake. Nanyi kuweni huru siku zote kwa ajili ya kumtumikia Mungu na mumtumikie kwa furaha siku zote za maisha yenu. Nabii Isaya– anatambua kuwa thamani ya maisha iko katika uhuru wa kimungu. Huo ndio uhuru wa kweli na wenye kuleta wokovu.

WHO IS A CONSECRATED PERSON?

He is a person who has an experience of God and especially as an Absolute. One who deeply aware of his encouter with God and having received a special gift which is divine and trinitarian. This is more than reading or hearing about God (Cf. Mk 8:27-29 – ungamo la Petro – baada ya Yesu kuwauliza – watu wasema mimi ni nani? ). And because in encoutering God he knows himself, then the experience of his weakness, fragility and suffering leads him to see God as an Absolute — God is all, man is nothing. Hence, the first task of consecrated person is to reveal the primacy of God to the world. All vocations reveal the mystery of Christ: the lay vocation reveals the face of Christ facing towards the world, the priestly vocation reveals the face of Christ facing towards the community and the consecrated vocation reveals the heart of Christ turned towards the Father. The consecrated person lives for God and only for God. The first value of our vows is to sing the primacy of God in our lives.

Waraka wa Kitume Injili ya Furaha,“Evangelii Gaudium” uliochapishwa na Baba Mtakatifu Fransisko unatoa kipaumbele cha kwanza kwa furaha ya Injili, kwa kuwaalika waamini kushirikisha furaha yao inayopata chimbuko kutoka katika huruma na upendo wa Mungu kwa wanadamu. Katika mwono huu, Kristo ni kiini cha Injili na kwamba, Kanisa linaalikwa kufanya mageuzi makubwa kama sehemu ya Uinjilishaji.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kusema – furaha ya Injili inajaza mioyo na maisha ya wale wanaokutana na Kristo. Pamoja na Yesu Kristo, furaha inazaliwa upya tena. Sura ya 4 – mwanzoni - ya waraka wa Pili wa Mtume Paulo kwa Wakorintho – inazungumzia juu ya watumishi kwa ajili ya Kristo. Mstari wa sita – kwani Mungu aliyesema, Mwanga ung’ae kutoka gizani, ndiye yeye anayeng’aa mioyoni mwetu tupate kwa mwanga wake kuutambua utukufu wa Mungu uliopo usoni mwa Yesu Kristo. 2 Kor. 4: 6…. Mnaalikwa muwe mwanga wake Kristo. Kwa maisha yenu na ushuhuda wenu wa maisha, Kristo aendelee kuonekana duniani. Maisha haya mnayotaka kufuata yawe changamoto kwa wale wote ili wanapowaona ninyi wazidi kumpenda na kumtumikia Mungu Baba.

Katika barua kwa mwaka wa watawa – Baba Mtakatifu Francis anamtaja wazi Mtakatifu Francisko wa Assisi kama mfano wa kuigwa, yeye aliyefanya Injili iwe njia yake ya maisha, akafanya imani ikakua na akahuisha kanisa na jamii, akaifanya iwe ya kindugu zaidi, lakini daima akiongozwa na Injili na ushuhuda wa maisha yake. Nanyi yapokeeni na yatimizeni mapenzi ya Bwana kama mtakatifiu Francis. Na imani yenu ionekane katika matendo yenu. Lengo lenu liwe tu ni kutangaza habari njema kwa kila kiumbe.

Neno la Mungu katika somo la Injili leo liwaongoze na kuwatafakarisha sana - Yesu ndiye masiha aliyepakwa mafuta, ambaye kadiri ya maandiko ya manabii ‘ndiye aliyepelekwa kuwatangazia maskini habari njema na kuutangaza mwaka wa Neema – Lk. 4, 18-19, pia katika Isa. 61: 1-2 - ‘Roho wa Bwana yu juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na vipofu kupata kuona tena, kuwaacha huru waliosetwa, na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa. Baada ya kusoma, akafunga kile kitabu, akampa mtumishi, kisha akaketi, watu wote wakamkodolea macho. Naye akaanza kuwaambia, andiko hili mlilolisikia limetimia leo’.

Nanyi ingieni katika programu hii ya kimasiha ya Yesu Kristo. Yaani muwe watangazaji mahiri wa ufalme wake na kuutangaza daima mwaka wa Bwana. Ujumbe huu bado u hai hata leo. Msijihangaishe na lo lote lile lililo nje ya programu hii. Katika kumfuata Kristo – Baba Mtakatifu katika barua yake kwa Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa anaendelea kusema – kuweni na mwanga na furaha, ng’aeni furaha. Isa. 66: 10-14 – shangilia pamoja na Yerusalemu, pigeni vigelegele kwa ajili yake, enyi nyote mnaomlilia, furahini, furahini pamoja naye ninyi nyote mlioomboleza kwa ajili yake Ili mpate kunyonya na kushibishwa maziwa ya faraja yake, na kufurahishwa kwa maziwa yake matukufu.

Maana, Bwana asema hivi; nitatiririsha amani na utulivu pande zote kama mto; nao utukufu wa mataifa kama kijito kifurikacho. Nanyi mtapata kunyonya, mtabebwa kifuani, na kubembelezwa juu ya magoti yake, mfano wa mwana anayefarijiwa na mama yake, ndivyo nami nitawafariji, nanyi mtafarijiwa moyo katika Yerusalemu. Kwa kuona hayo, moyo wenu utafurahi, na mifupa yenu itasitawi mfano wa majani mabichi na mkono wa Bwana utajulikana kwa watumishi wake, nayo ghadhabu yake kwa maadui zake.

Wote watakaoshiriki karamu hii ya Bwana na mwaliko huu mtakatifu watapata uzima wa milele. Ninyi mnataka kuingia katika karamu hii. Furahini pamoja na Bwana na furaha hiyo izae matunda katika maisha yenu.

Naye Mtakatifu Gaspari anatupa changamoto nyingine katika maisha ya ufuasi. Alipoanzisha Shirika la Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu alialika wafuasi wake wawe na upendo mkuu akisema ‘upendo ni kifungo kwa wamisionari wake’. Wakifungwa na upendo, Gaspari aliamini Wamisionari wake wataweza kueneza kwa maisha yao Tasaufi ya damu azizi. Tena watakuwa tayari kutoa huduma ya Neno la Mungu. Akinukuu maneno toka waraka wa Paulo kwa waefeso 1;6-8 – Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo …katika yeye ametuchagua kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu kusudi tuwe watakatifu na bila doa mbele yake katika upend.

Mtakatifu Gaspari aliamini kuwa upendo ukiwepo kazi ya Mungu itaendelezwa. Nasi tumwaminio tutapata uzima wa milele. Katika maisha yake alieneza sifa na utukufu wa neema hizi za Mungu, neema ambayo inatoka kwa mwanae mpendwa Kristo Yesu. Kutoka kwake Kristo tunaona ukombozi wetu na tuna msamaha wa dhambi. Nanyi muwe na upendo mkuu kwa Mungu Baba na Mwanae anayewajalia roho ya kutaka kumtumikia yeye kwa ulimwengu wa leo wenye changamoto nyingi za maisha.

Ninyi leo mnakuwa Wamisionari wanashirika. Mtakatifu Gaspari hakuona ibada kwa Damu azizi ya Yesu kama ibada nyingine ya kawaida, bali aliona ni kama kiini kabisa cha dini. Mtakatifu Gaspari mwenyewe anasema, ‘ni njia salama ya kufikia utakatifu binafsi na chachu ya maisha mapya ya jumuia na nguvu imara ya kazi ya kitume.

Pengine twaweza kujiuliza kama Kristo alishamwaga damu yake kwa ajili yetu sote, nafasi yangu ni ipi leo katika kuutangaza upendo huu wa Kristo? Kwa nini nihangaike kufanya mengi kama Kristo tayari ameshatukomboa? Waraka wa mtume Paulo kwa Wakolosai 1:24 unatupatia jibu “ nayatimiliza katika mwili wangu yale yaliyopungua katika mateso kwa ajili ya mwili wake yaani kanisa lake”

Nihitimishe homilia hii nikinukuu tena maneno ya Baba Mtakatifu Francis katika barua yake kwa Mwaka wa Watawa, akisema – nataka niseme neno moja kwenu, nalo ni furahini. Po pote walipo watawa na watu wa maisha ya wakfu, waseminari, wanaume na wanawake, vijana, ipo furaha, ipo daima furaha. Ni furaha ya upya, furaha ya kumfuata Kristo, furaha ambayo Roho Mtakatifu atupatia. Siyo furaha ya ulimwengu. Somo la pili la leo linatoa mwelekeo – Ebr. 13:12-15, 20-21- habari juu ya maisha mapya katika ufufuko.

Sisi tumepatanishwa na Mungu kwa njia ya kifo cha mwanawe, tumeokolewa kwa ufufuko wake. Sisi ni viumbe vipya. Ni watu wa ufufuko. Mnapoaanza maisha mapya katika shirika letu na ndani ya kanisa – jitahidini nanyi kuwa wapya katika yote – ishini maisha ya ufufuko. Maneno ya Petro Mtume yawaongoze“tuishi kama watakatifu kwa mfano wa Mungu aliyetuita kati
ka imani”.

Wednesday, January 7, 2015

Nendeni Jangwani kwa ajili ya Mwaka 2015

Katika Maandiko Matakatifu tunasoma yafuatayo: "Mara akaongozwa na Roho kwenda jangwani, akakaa huko siku arobaini akijaribiwa na shetani" (Marko 1:12-13).Yesu anaenda Jangwani na kukaa huko kwa muda wa siku arobaini. Lengo la kwenda jangwani si kujaribiwa ila kujiandaa kwa kazi iliyokuwapo mbele yake, kazi ya kumkomboa mwanadamu. Yesu alikwenda kutafakari kazi yake yote na yale yatakayompata katika kazi hiyo. Yesu alikwenda kutengeneza dira ya utekelezaji wa kazi ya ukombozi.

Read More
Nasi tunapoanza Mwaka Mpya 2015 tunahitaji kuingia katika 'jangwani' la kiroho na kimaisha ili kujitengenezea dira ya utekelezaji kwa mwaka mzima. Tujiwekee malengo binafsi, malengo ya familia, Jumuiya, kanda, kigango, parokia, jimbo na mahali pa kazi. Ni kipindi cha kujiwekea malengo ya kiroho, kiuchumi na kijamii. Mathalani. Mfano :
KIROHO: Jipangie mwaka huu unataka kufika wapi? Panga mambo yako ya kukua kiroho;tafakari ya Neno la Mungu; sala binafsi, sala za familia, ushiriki wako katika Jumuiya, kanda, kigango, parokia na kijimbo. Panga kushiriki mafungo ya kiroho, semina za kiroho, hija na matendo ya huruma. Ushiriki wako katika vipindi vya Kwaresma, Pasaka, Majilio na Krismas n.k.
KIUCHUMI: Tengeneza dira ya kiuchumi mwanzoni mwa mwaka kwa kupanga unataka kufika wapi kiuchumi mwaka huu. Usiache suala la uchumi likuendeshe bali wewe ulitawale kwa kufuata utakachojipangia mwanzoni mwa mwaka. Utajikuta unafanya mambo mengi kwa mpangilio hadi unafurahia maisha. Panga bajeti ya mwaka mzima; mapato na matumizi yako yaandike ili yakuongoze.
Bajeti yako iwe shirikishi ili itekelezeke, isiwe siri yako. Shiriki au ongoza kupanga bajeti ya mwaka ya familia, jumuiya, parokia, jimbo na mahali pa kazi. Iheshimu bajeti hiyo. Bajeti yako ianze na matumizi ili ikuongoze kupanga mapato. Kama mapato ni madogo kulingana na matumizi; fanya ubunifu, fikiria fursa mpya na zifanyie kazi, pia punguza matumizi yasiyo ya lazima, kadi za michango isiyo ya lazima, vikao visivyo na tija vitakavyokugharimu n.k. Wakati mwingine ni heri ya lawama kuliko fedheha!
Panga zaka yako, sadaka, majitoleo, michango ya Jumuiya, mavuno ya parokia, mavuno ya jimbo n.k usikurupuke kila siku na kwenda kutoa 'makombo' hayana nafasi mbele ya Mungu ni sawa na kujiletea 'laana' maishani mwako.
Mambo mengine muhimu ya kupanga katika dira ya mwaka huu ni pamoja na kushiriki matukio muhimu ya kijamii. Ni mwaka wa kura za maoni ya kupata katiba ya nchi yetu, usithubutu kupanga kutokushiriki, huo ni wajibu wa kila raia wa Tanzania.
Kushiriki uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais. Ili tupate viongozi wazuri, wachamungu, waadilifu na wakweli, jitokeze ili uchaguliwe na/au uchague kiongozi atakayetufaa kuiongoza jamii na nchi yetu.
Mwaka wa Familia utafungwa rasmi mwaka huu, Je, umeambulia nini kiimani? Umejiwekea mikakati gani ya kutengeneza mapungufu yaliyo ndani ya familia yako? Shiriki vyema semina za mwaka wa familia. Huu pia ni Mwaka wa Watawa Duniani, Je, unashiriki namna gani katika kuhamasisha, kukuza na kulea miito mitakatifu ndani ya Kanisa?
Huu ni mwaka wa uchaguzi wa viongozi wa Kanisa - walei kuanzia ngazi ya Jumuiya ndogondogo hadi Taifa. Jitokeze uchaguliwe na uchague viongozi hao. Shiriki kikamilifu kwani kanisa linakuhitaji.
Yote hayo yanatuhitaji kwenda 'jangwani' ili kujipanga. Tumshirikishe Mungu kupitia sala na mafungo. Tumkabidhi Mungu malengo yetu ya mwaka 2015. Tujitathmini mara kwa mara juu ya utekelezaji wa malengo hayo. Tuache kuishi kwa mazoea, mwaka 2015 tuwe wahalisia, tusibahatishe! Tuepuke mikwaruzano, tuongeze furaha na ufanisi. Tuwe 'Kristu' katika maisha yetu ya kila siku ili kuisaidia jamii. Tuache kulalamika lalamika, tuchukue hatua.

Tuesday, January 6, 2015

UMOJA WA VIJANA DEKANIA YA MT. GASPER DEL BUFFALO - kufanya uchanguzi wa Viongozi tarehe 10/01/2015

Dekania ya Mt. Gasper ni Dekania ilipo katika Jimbo kuu la Dar es salaam, inaundwa na Parokia kumi na moja ambazo ni  Parokia ya Bunju, Boko Tegeta, Madale, Bahari Beach, Mtongani, St. Gasper, Maria Del Mathias, Sala sala, Mt. Dominiko, Bikira Maria Mama wa huruma, Mbezi Beach  Pamoja na Parokia teule za Thomas More Mbezi Beach, Yohane Mtume, Nyaishozi Tegeta na Parokia ya Ununio tegeta.

Baada ya Baba mlezi wa vijana wa Dekania kuona mwenendo mbaya wa viongozi na kuamua kuwashirikisha Mapadre wote wa parokia za Dekani hii, kwa pamoja wameridhia kuvunja uongozi wa VIWAWA dekania, na kuitisha uchaguzi mpya ili wapatikane viongozi wapya watakao leta maendeleo kwenye dekania yetu.

Uchaguzi huo utafanyika tarehe 10/01/2015 Parokiani Bunju kuanzia saa 3:00 asubuhi, wajumbe wa uchaguzi huo ni Kamati tendaji ya VIWAWA, Parokia zote za dekania yetu.

Pia tarehe 17/01/2015 kutakuwa na Semina ya vijana wote wa Dekania itakayofanyikia Pale Parokiani St. Gasper na atakuwepo Msanii wa Nyimbo za Bongo Fleva Roma Mkatoliki.

IBADA YA MISA TAKATIFU YA UTOAJI DARAJA LA USHEMASI NA UPADRE LEO KANISA LA ST. JOSEPH, JIMBO KUU LA DAR ES SALAAM

Mafratel waliopata Ushemasi,
  1. Shemasi DanielMatugwa Vicent -  Parokia ya Changombe
  2. Shemasi Meinrad Bigirwamungu - Parokia ya Mtongani
  3. Shemasi Raymond AlbanoMbaula  -  Parokia ya Kigamboni
Na Shemasi aliyepata daraja la Upadre  ni Padre Tito Deogratius Rwegoshora - Parokia ya Kibaha

Baba Askofu Kardinal Pengo atangaza Kigango cha Orongoni kuwa Parokia na kitahudumiwa na Mapadre wa Shirika la Wamisionari wa Mt. Francis wa Asizi.
Pia ametangaza Parokia Teuli ambazo zitakuwa chini ya uangalizi mpaka zitakapokuwa Parokia ambazo ni;
  1. Kigango cha Ununio kilichokuwa chini ya parokia ya Tegeta na kitakuwa kinahudumiwa na Mapadre wa Shirika la Mt. Vicent wa Mbinga.
  2. Kigango cha Mt. Yohane Mtume Nyaishozi kilichokuwa chini ya Parokia ya Tegeta na kitakuwa kinahudumiwa na Mapadre wamisionari wa Maria Emaculate 
  3. Kigango cha Thomas More kilichokuwa chini ya Parokia ya Mt. Gasper kitakuwa kinahudumiwa na Mapadre wa Jimbo na Paroko atakuwa PD. Gilbert Makuru aliyekuwa Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mikocheni


Sunday, January 4, 2015

Masomo ya Tarehe 4/01/2015 mwaka B, wa Kanisa Dominika ya kwanza ya Mwaka Mpya 2015

04
 Januari
 Jumapili: ya tokeo la Mama Epifania.
SOMO  1. Isa. 60:1-6

 Ondoka, ee Yerusalemu, uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja na utukufu wa Bwana umekuzukia. maana tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu latazifunika......
somo 2. Efe. 3:2-5, 5-6 

Ndugu zangu; Ikiwa mmesikia habari ya uwakili wa neema ya Mungu niliyopewa kwa ajili yenu; ya kwamba kwa kufunuliwa nalijulishwa siri hiyo......


  INJILI.Mt. 2:1-12
Somo katika Injili ilivyoandikwa na Mathayo.

Yesu alipozaliwa Bethelehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, tazama, mamajusi wa mashariki walifiki Yerusalemu, wakisema, Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? kwa maana tuliiona nyota yake mashariki, nasi tumekuja kumsujudia. Basi mfalme Herode  aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye. Akakusanya wakuu wa makuhani wote na waandishi wa watu, akatafuta habari kwao; Kristo azaliwa wapi? Nao wakamwambia katika Bethlehemu ya Uyahudi; kwa maana ndivyo ilivyoandikwa na nabii, Nawe Bethlehemu, katika Nchi ya Yuda, Hu mdogo kamwe katika majumbe wa Yuda, kwa kuwa kwako atatoka mtawala atakaye wachunga watu wangu Israel. Kisha Herode akawaita wale Mamajusi faraghani, akapata kwao hakika ya muda tangu ilipoonekana ile nyota, Akawapeleka Bethlehemu, akasema, shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende kumsujudia, Nao waliposikia maneno ya mfalme, walishika njia; na tazama, ile nyota waliyoona mashariki ikawatangulia, hata ikaenda ikasimama juu ya mahali alipokuwapo mtoto.  Nao walipoiona ile nyota, walifurahi furaha kubwa mno. Wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia; nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na manemane. Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, wakaenda zao kwao kwa njia nyingine
Ratiba ya Ibada ya Jumapili ya tarehe 02/11/2014
Kigango cha Boko
Misa ya Kwanza- saa 12:15 Mpaka saa 1:45 Asubuhi.
Misa ya Pili        -  saa 2:00 Mpaka saa 3:50 Asubuhi.
Misa ya Tatu     -   saa 4:00 Mpaka saa 5:30 Asubuhi.

Kigango cha  Mt. Rafael Mbweni Malindi

Misa ya Kwanza   - saa 1:00 Mpaka saa 2:50 Asubuhi
Misa ya Pili            - saa 3:00 Mpaka saa 4:50 Asubuhi.

Kigango cha Mt. Fransisco wa Asizi - Mbweni
Misa ya Kwanza - saa 1:15 mpaka saa 2:50 Asubuhi.
Misa ya pili          - saa 3:00 mpaka saa 4:50 asubuhi

Kigango cha Mt. Anthony wa Padua - Mbweni Mpiji
Misa ni saa 3:00 mpaka saa 5:00 asubuhi

Wednesday, December 31, 2014

Masomo ya jumatano tarehe 31/12/2014

Jumatano, 31 Desema 2014
Jumatano katika Octava ya Kuzaliwa Bwana

1Yoh 2:18-21;
Zab 95: 1-2, 11-13;
Yn 1: 1-18

Jibu katika Neno la Mungu

Dibaji ya Injili ya Yohane ni nyimbo nzuri inayoimba juu ya simulizi ya Krismasi, fumbo la Umwilisho. Kutoka katika ufahamu huu wa binafsi wa kuishi na Kristo, Yohane alikuwa ameshawishika kwa kina sana kuwa Yesu ndiye Neno, Aliyekuwako tokea mwanzo pamoja na Mungu, Aliyekuwa mwili na kukaa kwetu. Andiko hili tukufu linatoa muunganiko wa imani ya Kikristo. Ukristo sio dini ya kitabu bali ni dini au neno la Mungu, sio neno lililoandikwa na lisilo nena, bali ni ya umwilisho na Neno liishilo. Kwahiyo, hususani katika Adhimisho la Ekaristi, wakati habari njema inapohubiriwa, ni Kristo Mwenyewe ndiye anayehubiri kupitia watumishi wake, wakitafuta jibu sawa la imani ipendwayo ambayo Yeye aliomba kwa wale wote ambao Aliwahubiria katika Palestina. Na kanisa ni katika kiini chake cha ndani, jumuiya ya wale wote wanaosikia neno la Mungu na kulizingatia. Swali ni, je, kama wanajumuiya wa hii jumuiya ya imani inayosikiliza, je, ni namna gani tunajibu?  Je, daima tupo tayali kujifungua wenyewe katika neno la Mungu namapenzi yake kwetu sisi? Au tunajikuta sisi wenyewe hatupendi, tusio badilika kutokana na nguvu ya neno la kubadilisha, isiyoenda kutokana na tofauti ya neema iletwayo?

Sala: Bwana, tuongoze katika upendo mkuu wa neno lako na tutie nguvu ya unyenyekevu katika kujibu na kutii imani. Amina.

"Amri ya maisha ya kikristo itaonekana si katika kitabu kilichoandikwa, ball ni katika tendo la binafsi la Roho Mtakatifu mwenye kumsukuma na kumwongoza Mkristo. Ni "sheria ya Roho ya uhai wa Kristo Yesu". "Maana Mungu amekwisha miminia mioyoni mwetu upendo wake kwa njia ya Roho Mtakatifu aliyetujalia". Jambo hili ni kweli pia kwa raume na mke wakristo na famllia ya klkrlsto. Mwongozo na sheria ya maisha yao ni Roho wa Yesu aliyemiminwa ndani ya mioyo yao katika adhimisho la sakramenti ya Ndoa. Katika mfululizo pamoja na Ubatizo katika maji na Roho, ndoa huweka upya sheria ya kiinjili ya upendo, na pamoja na zawadi ya Roho, hukaza zaidi katika mioyo ya waume na wake Wakristo. Upendo wao ukisafishwa na kuokolewa, ni tunda la Roho mwenye kufanya kazi katika mioyo ya waumini na kufanyiza, wakati huo huo, amri ya msingi ya maisha katika uhuru wa kimadaraka." – Baba Mtakatifu Yohani Paulo II, Wosia wa Kitume Familiaris Consortio (WAJIBU WA FAMILIA YA KIKRISTU KATIKA ULIMWENGU WA KISASA)- 63.

VIWAWA BOKO
www.viwawaboko.blogspot.com

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR