Friday, May 8, 2015

Kwanini kinaporomosha shilingi ya Tanzania?

Thamani ya Shilingi ya Tanzania imekuwa ikiporomoka kwa kasi sana ndani ya miezi mitano iliyopita
Itakumbukwa kwamba mpaka kufikia Januari mwaka jana Dola ilikuwa ikibadilishwa kwa Sh1,630 na ilikuwa ikiporomoka taratibu mpaka kufika Sh1,850 na Sh1,900 ilipofika Februari mwaka huu. Kwa sasa ni zaidi ya Sh2,000.
Kuna sababu mbalimbali zinasababisha kuporomoka kwa thamani ya shilingi.
Zipo sababu za kiuchumi ambazo pia zimegawanyika kwa kigezo cha ndani na za nje. Vilevile zipo sababu za sera na usimamizi wa sheria za nchi kuhusu masuala ya kifedha.
Sababu ya kwanza ambayo husababisha kushuka kwa thamani ya fedha ya nchini yoyote ni urari wa kibiashara (balance of trade).
Katika urari wa biashara, kinachoangaliwa ni namna nchi inavyoweza kuuza vitu nje pia inavyoagiza vitu kutoka nchi za nje. Kama nchi inatumia bidhaa nyingi za nje kuliko zile za ndani na inauza vitu nje kwa kiasi kidogo kuliko inavyoviagiza basi thamani ya fedha ya nchi hiyo lazima ishuke kwa kasi.
Kwa Tanzania bidhaa nyingi tunazozitumia ni za nje hivyo tunahitaji zaidi Dola ili tuweze kununua bidhaa hizo katika soko la dunia. Hii inapekea hitaji la shilingi liwe dogo ikilinganishwa na hitaji la Dola hivyo thamani ya Dola inakuwa juu kuliko ya Shilingi ya Tanzania.
Suala jingine linaloweza kuathiri thamani ya fedha ya nchi yoyote ni masuala ya uwekezaji kutoka nje yaani Foreign Direct Investment (FDI).
Uwekezaji wa nje ukiongezeka kwa kiasi kubwa husababisha thamani ya fedha ya nchi husika kupanda kwa sababu hitaji lake linakuwa kubwa kwa wawekezaji ambao wanaendesha miradi yao kwa gharama kubwa kwa fedha ya nchi husika.
Hatujapata bado tamko la serikali ama takwimu zozote zinazoonyesha kama uwekezaji kutoka nje umepungua ama wawekezaji wamepunguza mitaji lakini ni moja kati ya sababu ambazo za kushuka ama kupanda kwa thamani ya fedha katika nchi husika.
Thamani ya fedha inaweza pia kuathiriwa na uwekezaji ambao unavuka mipaka ya nchi na sekta mbalimbali kwa lugha ya kimombo; portfolio Investment.
Hii ni aina ya uwekezaji ambao huendeshwa kwa mitaji ya hisa kwa watu kutoka katika mataifa mbalimbali kwa mfano mtu anaweza kuwa ni Mtanzania lakini akawa anahisa katika kampuni ya Uingereza.
Kukiwapo na portifolio investment nyingi hapa kwetu hisa zake zitakuwa zinauzwa kwa shilingi hivyo watu wa mataifa mbalimbali watahitaji kuinunua ili waweze kuwekeza.
Uwekezaji wa namna hii hapa kwetu upo kwa kiasi kidogo sana hivyo inasababisha hitaji la shilingi kwa watu wa mataifa mengine lisiwe kubwa kitu ambacho kinashusha thamani ya fedha yetu.
Nchi ambazo taasisi zake za kifedha zinatoa riba kubwa kwenye mitaji ya fedha ya wateja wake huvutia watu wengi kununua fedha ya nchi hiyo kwa ajili ya kunufaika.
Kwa bahati mbaya hapa nchini suala la riba limekuwa linanufaisha upande mmoja yaani taasisi za kifedha. Taasisi za fedha zinatoza wateja wake riba kubwa wakati mwingine zaidi ya asilimia 13 kwenye mikopo ambayo wateja wanakopa kutoka katika taasisi hizo.
Wakati huohuo, watu ambao wanawekeza fedha zao kwenye taasisi hizo kupitia mfumo wa akaunti ya muda maalumu ama fixed deposits, hupewa ongezeko la riba kwa kiasi kidogo, mara nyingi ikiwa ni chini ya asilimia sita.
Suala hili linaathiri thamani ya fedha ya Tanzania kwa sababu watu ambao wanawekeza katika mitaji ya fedha wanapata ongezeko dogo la riba.
Sababu ya nje ni kuimarika kwa Dola ya Marekani. Taarifa ya mwenendo wa Dola ya Marekani ya Oktoba 2014, inaonyesha kuwa imekuwa ikiimarika na inaweza ikaendelea kufanya hivyo mpaka mwishoni mwa mwaka 2015.
Wachambuzi wa uchumi wa kimataifa wanahusisha kuimarika kwa Dola ya Marekani na mambo ambayo tayari nimeyaainisha.
Moja ni kwamba baada ya mtikisiko wa kiuchumi (2008 – 2009) uwekezaji katika mitaji ya hisa kwa watu wa mataifa mbalimbali umerejea katika hali yake.
Benki Kuu ya Marekani imerejesha ongezeko la riba katika mitaji ya fedha hivyo watu wananua dola zaidi ili waweze kunufaika kwa kuziwekeza kupitia benki.
Marekani kwa sasa ni nchi ya kwanza duniani kwakuwa na uwekezaji kutoka nje ya nchi. Pia, ongezeko la uzalishaji wa mafuta katika nchi hiyo ambao umepunguza uagizaji wa bidhaa hiyo kutoka nje umesababisha pia ongezeko la thamani ya dola kwani watu wa nchi hiyo wanahitaji fedha za nchi nyingine kama ilivyokuwa awali.
Sababu ya mwisho na muhimu ni suala la uwezo wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuweza kusimamia kikamilifu sera, sheria na kanuni za fedha.
BOT inapaswa kusimamia matumizi ya fedha za Tanzania kwani kwa mujibu wa sheria ya fedha ya mwaka 2006, shilingi ya Tanzania ndio fedha halili kwa malipo ya bidhaa na huduma hapa nchini.

Thursday, May 7, 2015

Saturday, April 4, 2015

Masomo ya Jumapili ya Paska "mwaka B wa Kanisa (Tarehe 05/04/2015)

05

 APRILI
 Heri ya Paska Masomo ya Mwaka "B".

SOMO  1: Mdo. 10:34, 37- 43
Somo katika kitabu cha Matendo ya Mitume.
  Petro akafumbua kinywa chake, akasema, Jambo lile ninyi mmelijua, lilionea katika Uyahudi wote likianzia Galilaya, baada ya ubatizo aliohubiri Yohane; habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu; naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu aikuwa pamoja naye. Nasi tu mashahidi wa mambo yote yaliyotendeka katika nchi ya Wayahudi na katika Yerusalemu; ambaye walimwua wakamtundika mtini. Huyo Mungu alimfufua siku ya tatu, akamjalia kudhihirika, si kwa watu wote, bali kwa mashahidi waliokuwa wamekwisha kuchaguliwa na Mungu, ndiyo sisi, tuliokula na kunywa naye baada ya ufufuka kwake kutoka kwa wafu. akatuagiza tuwahubiri watu na kushuhudia ya kuwa huyu ndiye aliyeamriwa na Mungu awe mhukumu wa wahai na wafu. Huyo manabii wote humshuhudia, ya kwamba kwa jina lake kila amwaminiye atapata ondoleo la dhambi.

WIMBO WA KATIKATI. 
Zab. 118:1-2, 16-17, 22-23. 
1.Aleluya.
            Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema
  kwa maana fadhili zake ni za milele.
           Israeli na aseme sasa,
    Ya kwamba fadhili zake ni za milele.

K. siku hii ndiyo aliyoifanya Bwana, Tutashangilia na kuifurahia.

2. Mkono wa kuume wa Bwana umetukuzwa;
                   Mkono wa kuume wa Bwana hutenda makuu.
     Sitakufa bali nitaishi,
                   Nami nitayasimulia matendo ya Bwana.
(K)
3. Jiwe walilolikataa waashi
                Limekuwa jiwe kuu la Pembeni.
     Neno hili limetoka kwa Bwana,
                Nalo ni ajabu machoni petu (K)

Monday, March 30, 2015

UJUMBE WA BABA MTAKATIFU SIKU YA VIJANA (JUMAPILI YA MATAWI 29/03/2015)

Heri wenye moyo safi maana hao watamwona Mungu ndiyo kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya Siku ya Vijana Kijimbo inayoadhimishwa na Mama Kanisa, Jumapili ya Matawi tarehe 29 Machi 2015 kama sehemu ya maandalizi ya Siku ya 30 ya Vijana Kimataifa itakayoadhimishwa Jimbo kuu la Cracovia, Poland, mwezi Julai 2016.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wa maadhimisho ya Siku ya vijana kijimbo anagusia hamu ya vijana kuwa na furaha na anaendelea kuchambua kwa kina na mapana kauli mbiu ya ujumbe huu kwa kuwakumbusha vijana kwamba, Kristo ni utimilifu wa furaha ya mwanadamu, changamoto kwa vijana kuhakikisha kwamba, wanatunza ndani mwao moyo safi na kamwe wasibeze upendo wa dhati.

Baba Mtakatifu anawataka vijana wakati mwingine kwenda kinyume cha mawimbi ya maisha ya ujana, kwa kutambua kwamba, fainali iko uzeeni. Wawe ni watu makini katika maisha na maamuzi yao na kamwe wasikubali na kumezwa na malimwengu kwani watajikuta wapweke na hawana matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Vijana katika maisha waoneshe ari na moyo wa kupenda kwa dhati.

Hija ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Vijana Kimataifa huko Cracovia, Poland inaongozwa na Hotuba ya Heri za Mlimani, ambayo kimsingi ni muhtsari wa mafundisho makuu ya Yesu, chemchemi ya furaha ya kweli na amani ya ndani. Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, kila mtu duniani yuko kwenye mchakato wa kutafuta furaha ambayo inapata chimbuko lake kutoka kwa Mwenyezi Mungu anayeijaza mioyo ya waja wake, kama yanayobainisha Maandiko Matakatifu, kielelezo cha umoja na mshikamano kati ya mwamini na nafsi yake; mwamini na Mungu pamoja na jirani zake.

Baba Mtakatifu anaendelea kusema kwamba, dhambi ilipoingia ulimwenguni, ilichafua usafi wa mioyo ya binadamu, kiasi kwamba, dhambi ikawa ni kizingiti cha mwanadamu kuweza kukutana moja kwa moja na Muumba wake; furaha ya kweli ikakosa dira na mwelekeo sahihi; mwanadamu akatumbukia katika huzuni na mahangaiko ya ndani. Mwanadamu akamlilia Mwenyezi Mungu, naye akakisikia kilio chake na kumtuma Mwanaye mpendwa, Yesu Kristo ili aweze kumfungulia mwanadamu malango mapya ya kukutana na Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anawaambia vijana kwamba, ni kwa njia ya Yesu Kristo wanaweza kupata utimilifu wa wema na furaha ya kweli. Yesu Kristo ndiye mwenye uwezo wa kuzima kiu ya matarajio ya vijana katika maisha, ambao wakati mwingine wanadanganywa na malimwengu kwa kuwapatia njia za mkato.

Baba Mtakatifu Francisko kwa namna ya pekee kabisa anawaalika vijana kuhakikisha kwamba, wanatunza usafi wa moyo kwa kujenga na kudumisha mahusiano mema na matakatifu kati yao na jirani zao. Moyo wa mtu n ikisima cha mawazo na vionjo, changamoto kwa vijana kuhakikisha kwamba, mawazo yao yanakuwa safi pasi na mawaa mbele ya Mungu na binadamu. Moyo safi wenye uwezo wa kujenga mahusiano bora.

Baba Mtakatifu anawaalika pia vijana kujenga utamaduni wa kutunza mazingira kwani hii ni sehemu ya ekolojia ya binadamu, ambayo inapaswa kuwa kweli ni safi, kama kielelezo makini cha mahusiano bora  kati ya mwamini na Muumba wake pamoja na kazi ya uumbaji ambayo Mungu amemkabidhi mwanadamu kuitunza na kuiendeleza. Vijana waonje upendo wa Mungu anayewaangalia kama mboni ya jicho lake!

Baba Mtakatifu anawakumbusha vijana kwamba, ujana ni moto wa kuotea mbali; ni wakati ambapo mbegu ya upendo ambao unajikita katika ukweli, wema na ukuu unaanza kuchanua pole pole katika maisha ya vijana. Baba Mtakatifu anawaangalisha vijana kuwa makini ili mbegu hii ya upendo isije ikachafuliwa na hatimaye kuharibiwa. Hapa vijana wanatakiwa kuwa makini na kamwe wasikubali kuyumbishwa na mawimbi ya maisha ya ujana kwa kubeza upendo, kiasi cha kuugeuza kuwa ni mahali pa kukidhi tamaa za mwili. Lakini ikumbukwe kwamba, upendo wa kweli unajikita katika wema, umoja, uaminifu na uwajibikaji. Vijana wanapaswa kuwa ni wana mapinduzi kwa kwenda kinyume na mawimbi haya potofu na dhidi ya utamaduni wa raha za mpito ambazo mara nyingi zimewaachia vijana machungu katika maisha.

Vijana wawe waaminifu na kuwajibika barabara kwa kuonesha jeuri kwamba, wanafahamu kupenda kwa dhati. Baba Mtakatifu anasema, ana imani kubwa na vijana na kwamba, anawaombea, ili kamwe wasitindikiwe na ujasiri huu. Vijana wanaalikwa kwa namna ya pekee kabisa na Baba Mtakatifu kuhakikisha kwamba, wanamtafuta Mwenyezi Mungu kwa njia ya: sala, tafakari ya Neno la Mungu na upendo kwa jirani. Kusali ni kuongea na kujadiliana na Fumbo la Utatu Mtakatifu yaani: Mungu Baba, Mungu Mwana na Mungu Roho Mtakatifu. Vijana wajenge utamaduni na mazoea ya kusali vyema na daima.

Tafakari ya Neno la Mungu imwilishwe kwa njia ya upendo na huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Kwa njia hii, vijana wataonja na kutambua uwepo endelevu wa Mungu katika maisha yao; Mungu ambaye anaendelea kutekeleza mpango wake kwa maisha ya kila kijana. Vijana wamkimbilie Mwenyezi Mungu wakiwa na mioyo safi pasi na woga wala makunyanzi mioyoni mwao. Vijana wanaposikia kwamba, wanaitwa na Mwenyezi Mungu katika miito mitakatifu, wasisite kusema, Ndiyo na kwa njia hii wataweza kuwa kweli ni mbegu ya matumaini kwa Kanisa na jamii inayowazunguka. Vijana watambue kwamba, mapenzi ya Mungu katika maisha yao ndicho kiini cha furaha yao ya kweli.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha ujumbe wake kwa Siku ya Vijana Kimataifa katika ngazi ya kijimbo inayoadhimishwa Jumapili ya Matawi kwa kumshukuru Mtakatifu Yohane Paulo II ambaye miaka thelathini iliyopita alithubutu kuanzisha ndani ya Kanisa Siku ya Vijana Kimataifa. Hii ni hekima ya Kimungu na sauti ya kinabii ambayo imeliwezesha Kanisa kuwashirikisha vijana wengi matunda ya maisha ya kiroho. Mtakatifu Yohane Paulo II msimamizi wa Siku za Vijana Kimataifa, awaombee vijana wakati huu wa maandalizi kuelekea katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Kimataifa itakayofanyika Jimbo kuu la Cracovia, nchini Poland. Bikira Maria aliyejaa neema, uzuri na usafi wote, awasindikize vijana katika hija hii.

Tazama aleleya kuu hapa

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR