Sunday, October 18, 2015

YAFAHAMU MAJIMBO YA UCHAGUZI MANISPAA YA KINONDONI

MAJIMBO YA UBUNGO, KINONDONI NA KAWE – CCM INAWEZA KUAMBULIA PATUPU
Na. Julius Mtatiro,
Mkoa wa Dar Es Salaam una jumla ya majimbo ya uchaguzi 8, ambayo yamo katika wilaya tatu za Kinondoni, Ilala na Temeke. Katika uchambuzi wa leo tutajikita katika majimbo matatu ya wilaya ya Kinondoni, ambayo ni Ubungo, Kinondoni na Ilala.
Utangulizi
Kinondoni ni wilaya yenye ukubwa wa kilomita za mraba 531 na imepakana na Wilaya ya Bagamoyo upande wa Kaskazini, upande wa Kaskazini Mashariki inapakana na Bahari ya Hindi, upande wa Kusini inapakana na Manispaa ya Ilala, upande wa Kusini Magharibi inapakana na Wilaya ya Kisarawe na upande wa Magharibi inapakana na Wilaya ya Kibaha.
Kutokana na sensa ya mwaka 2012 wilaya ya Kinondoni ina watu 1,775,049 ambapo wanaume ni 860,802 na wanawake 914,247 na ina ongezeko la watu kwa wastani wa asilimia 5 kwa mwaka.
Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imegawanyika katika Tarafa 4, Kata 34, Jumla ya Mitaa ni 171, Idadi ya Majimbo ya Uchaguzi ni matatu (3) ambayo ni Kawe, Kinondoni na Ubungo.

JIMBO LA UBUNGO:
Julius  S. Mtatiro's photo.
Kisiasa jimbo la Ubungo limekuwa chini ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) muda wote tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini Tanzania. Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2000 na 2005 ulishuhudia ushindani mkubwa wa kisiasa na CCM haikupata usingizi. Mwaka 2000 mgombea wa CUF Hussein Mmasy alimtikisa Keenja wa CCM ambapo Ndugu Mmasy alipata zaidi ya asilimia 40 ya kura zote.
Katika uchaguzi wa mwaka 2005 kijana mwingine, John Mnyika wa CHADEMA aliitikisa CCM ipasavyo. Jumla ya wapiga kura 314,065 walijiandikisha na kura 9,776 ziliharibika. Mgombea wa CCM wakati huo Charles Keenja kupata kura 93,493 sawa na asilimia 51.6 dhidi ya John Mnyika wa Chadema aliyepata kura 45,164 sawa na asilimia 24.9 huku wagombea wa CUF na NCCR kwa pamoja wakipata jumla ya kura 37,735 sawa na asilimia 20.8. Pia CCM ilishinda viti vya udiwani 11 katika kata 11 za jimbo la ubungo wakati huo. Pamoja na matokeo hayo, vyama vya upinzania havikuwa vimejipanga vya kutosha na uchaguzi uliambatana na hila nyingi kutoka kwa CCM.
Mwaka 2010 ulikuwa na nuru ya pekee ambapo jimbo la Ubungo liliangukia mikononi mwa CHADEMA, Mgombea wake John Mnyika alipigiwa kura 66,742 sawa na asilimia 49.56 wakati mgombea wa CCM Bi. Hawa Ng’umbi alipata kura 50,544 sawa na asilimia 37.53 na Julius Mtatiro wa CUF alipata kura 12,964 sawa na asilimia 9.63 ya kura zote.
Kati ya mwaka 2010 na 2014 mbunge wa Ubungo, mhe. John Mnyika amejipambanua kama kiongozi anayewajibika kwa ajili ya maslahi mapana ya taifa, na hiyo ni sifa muhimu mno kwa siasa za sasa. Katika utekelezaji wa ilani yake ya uchaguzi kwa kiasi kikubwa hajafanikiwa katika suala la uhaba wa maji. Maji ni tatizo kubwa sana katika jimbo la Ubungo, pamoja na juhudi zote alizofanya jambo hili limekuwa gumu. Taarifa za ndani zinaonesha kuwa, serikali haijawekeza nguvu kubwa katika miradi ya maji Ubungo kwa kuhofia kumpa sifa Mnyika na kufanya jimbo hilo lisirudi CCM kirahisi katika uchaguzi wa mwaka 2015.
Pamoja na hisia hizo, ukweli ni kuwa Mahitaji ya maji katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwa sasa ni mita za ujazo 170,760 kwa siku lakini huduma inayopatikana kutoka katika mifumo ya maji ya DAWASA ni chini ya asilimia 45 ya mahitaji halisi na eneo linaloathirika zaidi na uhaba wa maji ni jimbo la Ubungo ambalo linaongozwa na Mnyika. Kwa sababu jukumu la kuleta maji ni la serikali huku kazi ya mbunge ikiwa ni kuhimiza na kushauri, John Mnyika hatakosa cha kuwaeleza wapiga kura kuhusu suala hili.
Wapiga kura wengi wa jimbo la Ubungo ambao ni vijana wanaendelea kumuunga mkono John Mnyika kwa sababu mara kwa mara anatoa taarifa ya mambo yaliyoshindikana na kwa nini imekuwa hivyo na kwa hakika, kati ya majimbo ambayo hayawezi kurudi CCM katika uchaguzi wa 2015 ni pamoja na hili la Mnyika. Hii inachangiwa hasa na ushirikiano wa vyama vya UKAWA, ikiwa UKAWA itamuunga mkono mgombea mmoja tu, John Mnyika atashinda tena kirahisi lakini UKAWA isiposimamisha mgombea mmoja kuna uwezekano mkubwa kwamba CCM wakajaribu kulichukua jimbo la Ubungo ukizingatia kuwa linachangia kwa kiasi kikubwa katika kujenga uchumi wa jiji la Dar Es Salaam na taifa kwa ujumla. Hili si jambo la kupuuza hata kidogo.

JIMBO LA KINONDONI:
Julius  S. Mtatiro's photo.
Jimbo la Kinodoni limekuwa chini ya Chama Cha Mapinduzi kwa muda mrefu. Kwa vipindi kadhaa, mbunge wa sasa Idd Azzan Mohamed ameendelea kushinda chaguzi. Pamoja na suala la kukosekana kwa usawa wa ushindani wa kisiasa na upendeleo ambao wagombea wa CCM wamekuwa wakipata kutoka kwa vyombo vya dola, Sababu kubwa ya kufanya jimbo hili liendelee kuwa chini ya CCM ni wagombea wasiotoa ushindani mkubwa kutoka vyama vya upinzani. Mwaka 2005 wagombea wa CUF na CHADEMA walipata jumla ya kura 41,775 sawa na asilimia 29. 9 huku CCM chini ya Idd Azzan ikishinda kwa kura 94,387 sawa asilimia 67.7.
Ushindi wa CCM ulipungua kwa kasi mwaka 2010 ambapo wagombea wa CUF na CHADEMA walipata jumla ya kura 50,015 sawa na asilimia 47.88 wakati CCM chini ya Idd Azzan ikipata kura 51, 372 sawa na asilimia 49.18, kwa hiyo katika uchaguzi wa 2010 CCM iliwazidi wagombea wa CHADEMA na CUF kwa kura 1357 sawa na tofauti ya asilimia 1.3.
Kwa hali ilivyo sasa,wananchi wanaonesha kumchoka mbunge Idd Azzan wa CCM na chama chake kinaweza kumleta mgombea mwingine ili kubadilisha ladha, kuweka mikakati mipya na kuwafanya wananchi wajione wako chini ya mtu mwingine. UKAWA pia itapaswa kumuweka mgombea mmoja kwa sababu nguvu ya CHADEMA na CUF kwa kura katika uchaguzi wa mwaka 2010 zilipishana kidogo tu (zinakaribiana mno).
Inajionesha wazi kwamba katika uchaguzi wa mwaka 2015 CCM itapoteza jimbo la Kinondoni hata kama itabadilisha mgombea. Sharti moja tu ambalo litaifanya CCM ishinde tena ni ikiwa vyama vya CHADEMA na CUF vitaweka wagombea tofauti, lakini kwa msimamo wa pamoja wa UKAWA ikiwa vyama vinavyounda UKAWA vitaweka mgombea mmoja imara na vikajipanga, jimbo hili halitaongozwa na CCM baada ya uchaguzi huo na kwa hiyo litaangukia mikononi mwa vyama vya UKAWA.
Kwa hakika hatuwezi kusema kwamba jimbo la Kinondoni limekuwa na mafanikio yoyote makubwa katika kipindi cha miaka minne iliyopita. Matatizo makuu ya wananchi katika maeneo ya uchumi, biashara na vipato yameendelea kuwa palepale, huduma za kijamii zinapatikana vizuri kwa wananchi walio na kipato: kwa ujumla matatizo ya jimbo la Kinondoni ni sawasawa na matatizo ya Ubungo, Kawe na Dar Es Salaam, wananchi watapenda kuona mbunge anayekuwa karibu nao zaidi na atakayefanya juhudi za wazi kuwatoa sehemu moja kuwapeleka nyingine.

JIMBO LA KAWE:
Julius  S. Mtatiro's photo.
Jimbo la Kawe ni kati ya majimbo yaliyopata bahati njema ya kuongozwa na wabunge wanawake katika nyakati kadhaa. Bi. Rita Mlaki wa CCM ameliongoza jimbo hilo kuanzia mwaka 2000 hadi 2010. Katika uchaguzi wa mwaka 2005 Bi.Mlaki alipata ushindi mkubwa wa asilimia 63 uliotokana na kura 64,074 dhidi ya vyama 11 vilivyoweka wagombea katika uchaguzi huo. Vyama vya CUF na CHADEMA kwa pamoja vilipata asilimia 33 iliyotokana na kura 33,522 huku vyama vingine 8 vikipata asilimia 3.1 kutokana na kura 4163.
Nguvu ya mwanamama mwingine, Bi. Halima James Mdee wa CHADEMA ilifanya mabadiliko makubwa katika uchaguzi wa mwaka 2010 ambao ilitarajiwa angepambana na Bi. Lita Mlaki(Aliyeshindwa dhidi ya Bi. Angela Kizigha katika kura za maoni ndani ya CCM).
Katika kinyang’anyiro hicho kilichowakutanisha kina mama wawili dhidi ya mwanasiasa maarufu na nguli mhe. James Francis Mbatia wa NCCR, nyota ya Bi. Halima Mdee wa CHADEMA iling’ara na akapata ushidi wa kura 43,365 sawa na asilimia 43.17 akifuatiwa na mwanamama mwenzie Bi. Angela Kizingha wa CCM aliyepata kura 34,412 sawa na asilimia 34.26 huku James Mbatia wa NCCR na Mapeyo Shaabani wa CUF kwa pamoja wakipata kura 21,091sawa na asilimia 21, na wakati huohuo, vyama vingine 5 vilivyoweka wagombea katika uchaguzi huo vikiambulia kura 1528 sawa na asilimia 1.58 ya kura zote.
Tangu kuchaguliwa kwake, Bi. Halima Mdee amejipambanua kama mwanamke jasiri na mpambanaji. Mara kadhaa amejitosa katika mapambano ya kudai haki za umiliki wa ardhi kwa wananchi huku akijaribu kusimamia suala la uporwaji wa maeneo ya wazi unaofanywa na vigogo na hata serikali yenyewe. Ujana wa Halima Mdee, kuwa karibu na wapiga kura na faida ya kuwa mwanamke kunamfanya awe na nafasi kubwa kutetea kiti chake katika uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015.
Kitisho chochote cha CCM kumshinda Bi. Halima Mdee katika uchaguzi ujao kitaondolewa na uwepo wa UKAWA, kwa maana kwamba kama UKAWA ikimsimamisha kama mgombea pekee, atapata faida ya kupigiwa kura za NCCR na CUF ambazo ni asilimia zaidi ya 20 na hivyo anaweza kupata ushindi wa kishindo wa zaidi ya asilimia 60.
Katika jimbo la Kawe mwaka 2015, sera muhimu zitajikita katika masuala yaleyale yanayowakabili wananchi wa Dar Es Salaam hususani makazi (kwa sababu Kawe ni mji unaokua), ukosefu wa ajira, uhakika wa huduma za kijamii ikiwemo upatikanaji wa maji n.k.


Friday, October 16, 2015

Lowassa atuma salamu za rambirambi kifo cha Filikunjombe

 Lowassa atuma salamu za rambirambi kifo cha Filikunjombe
Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA), Edward Lowassa ametuma salamu za rambirambi kwa chama cha Mapinduzi(CCM) na familia ya aliyekuwa mbunge/mgombea wa jimbo la Ludewa Deo Filikunjombe aliyefariki pamoja na watu wengine watatu katika ajali ya Helikopta iliyotokea jana jioni maeneo ya mbuga ya Selous mkoani Morogoro.
Helikopta hiyo iliyokuwa inaongozwa na Kapt.William Silaa(marehemu) ilidaiwa kupata hitilafu na baadae kupoteza mawasiliano jana jioni ilipokuwa safarini kutoka Dar es salaam kuelekea Njombe.
Helikopta hiyo ilianguka kwenye mbuga ya Selous na kupelekea vifo vya watu wote wanne waliokuwemo.
“Filikonjombe alikuwa Mbunge mahiri aliyesimama imara kutetea maslahi ya wananchi wa jimbo lake la Ludewa na watanzania kwa ujumla,” amesema Lowassa.
“Alikuwa mwiba kwa serikali ya Chama chake CCM kutetea maslahi ya nchi, mfano ni katika kashfa ya Escrow ambapo alikuwa Makamu Mwenyekiti wa kamati iliyochunguza kashfa hiyo.”
“Mwenyezimungu awape moyo wa subira, familia, jamaa, marafiki na wananchi wa Ludewa, katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na mpendwa wao,” amesema Lowassa.
Ni pigo lingine kubwa ambalo katika kipindi kifupi Taifa limepata, huku bado likiwa na kidonda cha kuondokewa na wanasiasa wengine mahiri,Mchungaji Christopher Mtikila, Celina Kombani, Dr Abdallah Kigoda na Dr Emanuel Makaidi aliyefariki jana
Kwa mujibu wa Zitto Kabwe, ambaye ndiye msimamizi wa mazishi ya Filikunjombe, amesema miili ya marehemu wote wanne imehifadhiwa katika Hospitali ya jeshi Lugalo kwa ajili ya kufanyiwa utambuzi na madaktari kutokana na miili hiyo kuwa katika hali mbaya ya kuungua.
Baada ya utambuzi huo, taratibu za mazishi zitaendelea.

Deo Filikunjombe afariki dunia kwenye ajali ya Chopa

 Tanzia : Deo Filikunjombe afariki dunia kwenye ajali ya Chopa
Aliyekuwa mbunge wa jimbo la Ludewa, Deo Filikunjombe ambaye alikuwa anatetea nafasi hiyo kupitia chama cha Mapinduzi(CCM), amefariki kwenye ajali ya helikopta iliyotokea jana usiku ndani ya Pori la Akiba la Selous lililopo eneo la Kilombero mkoani Morogoro. Filikunjombe ni mmoja wa abiria wanne waliokuwa ndani ya chopa hiyo ambao wamethibitishwa kupoteza maisha. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Jerry Silaa,Meya wa Manispaa ya Ilala anayemaliza muda wake, Capt.William Silaa baba mzazi wa Jerry ndiye aliyekuwa rubani wa chopa hiyo ambaye naye amepoteza maisha. “Kwa masikitiko makubwa nimepokea taarifa rasmi kutoka kwa timu ya uokoaji imefanikiwa kufika eneo la ajali na kukuta abiria wote na rubani wamepoteza maisha,” ilisomeka sehemu ya taarifa ya Jerry Silaa. “Nimepoteza Baba na rubani mzuri wa nchi yetu Capt.William Silaa,nimepoteza rafiki na kiongozi wangu Mhe.Deo Filikunjombe. Nawapa pole wote waliopoteza ndugu zao. Nawaombea marehemu mapumziko ya Amani.” “Nawashukuru wote walioshirikiana na familia kusaidia uokozi,” . “Namshukuru Mhe.Rais Jakaya M Kikwete, Dr.John Pombe Magufuli, IGP Ernest Mangu, Katibu Mkuu MU Dr.Meru, Kampuni ya Everest Aviation ,Wabunge, MaDC, Maafisa wa TCAA na wote walioshiriki kuwatafuta wahanga wa tukio hili,” ilimaliza sehemu ya Taarifa ya Silaa Wakati Taifa bado likiwa limeshikwa na butwaa kutokana na vifo vya aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara Dr Abdallah Kigoda, aliyezikwa jana na siku hiyohiyo kutokea kifo cha Dr Emanuel Makaidi, Mwenyekiti wa NLD na mgombea ubunge jimbo la Masasi, leo tena Taifa linaamka na kushuhudia kumpoteza kijana shupavu aliyekuwa miongozi mwa wabunge mahiri kuwahi kutokea ndani ya chama cha Mapinduzi, Deo Filikunjombe. Ni misiba..misiba..misiba, hakika uchaguzi wa mwaka huu unatengeneza historia ya aina yake na ya kuhuzunisha. Filikunjombe anakuwa mgombea ubunge wa sita kufariki ndani ya kipindi kisichozidi majuma sita. Mungu ailaze roho yake mahali pema, AMEN

Monday, October 12, 2015

MAGUFULI LEO YUPO LINDI




WAJUE WAGOMBEA WA URAIS TANZANIA 2015

Tukiwa tunakaribia kabisa tarehe 25/10/2015, hebu leo tujikumbushe wasifu wa Wagombe wa Urais na vyama vyao.

1. Mh. Edward Ngoyai Lowassa KUPITIA CHAMA CHA CHADEMA NA KUUNGWA MKONO NA UKAWA.

 

WASIFU:   

Edward Ngoyai Lowassa alizaliwa tarehe 26 August 1953, katika kijiji cha Ngarash wilayani Monduli mkoa wa Arusha, akiwa ni mtoto wa 4 kati ya watoto 23 wa mzee Ngoyai Lowassa. 
ELIMU:
1961 – 1967: shule ya msingi Monduli1968-1971: shule ya sekondari Arusha1972 – 1973: St. Marry’s High School (Milambo High School) Tabora.1983 – 1984: Chuo Kikuu cha BATH Uingereza M.Sc (Development Studies).
UZOEFU KAZINI
1995 – 2000 – Waziri nchi ofisi ya makamu wa Rais Mazingira, Muungano nakuondoa umasikini. 2000 -2005 – Waziri wa maji na maendeleo ya mifugo.
Desemba 2005 Februari 2008 Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.
1985 – 2005 – Mbunge wa Monduli (ccm).
2010 – 2011 – Mwenyekiti Kamati ya bunge ya ulinzi na usalama na mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa .
 2011 – 2015 – Mwenyekiti kamati ya bunge ya mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa. 
28/07/2015 – Kujitoa CCM na kujiunga na CHADEMA 

Mhe. Edward Lowassa amemuoa Regina Lowassa na kujaliwa kupata watoto watano, watatu wa kiume na wawili wa kike

 Edward Lowassa ni shabiki wa michezo na alikuwa mchezaji mzuri wa mpira wa kikapu.

2. Dk. John Pombe Magufuli kupitia cha cha  CCM

 -1x-1

WASIFU: 

 John Pombe Magufuli alizaliwa Oktoba 29, 1959 katika Wilaya ya Chato ambayo ni mojawapo ya wilaya tano za mkoa mpya wa Geita uliopo kaskazini magharibi mwa Tanzania.

Wilaya ya Chato ilikuwa sehemu ya Wilaya ya Biharamulo mkoani Kagera na ni mwaka 2012 tu ndipo ilipohamishiwa Mkoa wa Geita. Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, Chato ina jumla ya wakazi 365, 127. 
ELIMU
Magufuli alipata elimu ya msingi katika Shule ya Chato na masomo ya sekondari ya awali katika Seminari ya Katoke, Biharamulo. Alimalizia kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Lake, mkoani Mwanza. Kidato cha sita alimalizia katika sekondari ya Mkwawa mkoani Iringa.
Wasifu wa Magufuli unaonyesha kwamba alipata cheti cha Stashahada ya Ualimu katika Chuo cha Elimu Mkwawa mnamo mwaka 1982 – alikojikita zaidi katika masomo ya hisabati na kemia.
Kati ya mwaka 1985 hadi 1988, Magufuli alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa ajili ya masomo yake ya shahada ya kwanza ya ualimu wa kemia na hisabati.
UZOEFU KAZINI
John Pombe Magufuli ni mwanasiasa Mtanzania wa CCM ambaye aliwahi kutumikia Baraza la Mawaziri la Tanzania, kama Waziri wa Ujenzi tangu 2010. Hapo awali alikuwa Naibu Waziri wa Ujenzi tangu 1995 hadi 2000, Waziri wa Ujenzi tangu 2000 hadi 2006, Waziri wa Ardhi na Makazi tangu 2006 hadi 2008, na Waziri wa Mifugo na Uvuvi kutoka 2008 hadi 2010. Aliwahi kuwa Mbunge wa jimbo la Chato tangu mwaka 1995. Yeye ndiye mgombea Urais wa CCM katika uchaguzi mkuu wa 2015.

3. Mh. Anne E. Mghwira kupitia chama cha ACT-Wazalendo

 WASIFU: 
 Bi. Anna Mghwira ni mwenyekiti wa kitaifa wa chama kipya cha siasa, ACT – Wazalendo. Alizaliwa tarehe 23 Januari 1959 katika hospitali ya mkoa wa Singida, Kata ya Mungumaji, Kitongoji cha Irao manispaa ya Singida Mjini. (Mwezi Januari mwaka huu ametimiza miaka 56).
Baba mzazi wa Anna alikuwa diwani na kiongozi wa TANU kabla ya CCM hadi mwaka 1985, mama yake alijishughulisha na kilimo na ufugaji na wazazi hawa kwa ujumla walijipatia watoto tisa, akiwemo Bi. Anna.
ELIMU
Anna aliendelea na masomo ya Chuo Kikuu mwaka 1982 baada ya kujiunga Chuo Kikuu cha Thiolojia (Chuo Kikuu cha Tumaini) na kuhitimu shahada ya Thiolojia mwaka 1986.
Mwaka huohuo 1986 alijiunga Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam akitafuta shahada ya Sheria na akaimaliza na kutunukiwa mwaka 1986.
Kati ya mwaka 1987 – 1998, Bi Anna aliendelea na shughuli za ujenzi wa Taifa, akifanya kazi ndani na nje ya nchi na kupata uzoefu mkubwa sana.
Safari ya Elimu ya Bi. Anna ilikamilikia Chuo Kikuu cha Essex nchini Uingereza ambako alianza shahada ya uzamili ya sheria (LLM) mwaka 1999 na kutunukiwa mwaka 2000.
Licha ya kuwa mwanasheria na mtheologia aliyebobea, pia amefanya kazi za maendeleo kwa muda mrefu na ana uzoefu katika uendeshaji wa serikali za mitaa, uzoefu wa utumishi katika mashirka ya kimataifa, kitaifa na mashirika ya dini ambamo amejihusisha na masuala ya wanawake, watoto, wakimbizi, utawala na haki za binadamu.
Anna  alianza siasa tangu wakati wa TANU akiwa ni mwanachama wa Umoja wa Vijana wa Tanu (Tanu Youth League) na aliwahi kushinda tuzo mbalimbali kutokana na ushiriki wa juu katika TANU lakini baadaye ilipoanzishwa CCM alipunguza ushiriki wake ili ajipe muda katika masomo na baadaye ndoa na malezi ya watoto.
Kwa kipindi kirefu hakuwa anajihusisha na siasa hadi alivyoamua kujiunga na CHADEMA mwaka 2009 ambako alishika nafasi mbili tu za Uenyekiti wa baraza la wanawake ngazi ya wilaya na Katibu wa Baraza la wanawake Mkoa.
Mwezi Machi 2015 alijiunga rasmi na chama cha ACT – Wazalendo na katika Mkutano Mkuu wa kwanza wa chama hicho, yeye ndiye akachaguliwa kuwa mwenyekiti wa kwanza wa ACT.
 August 20 2015 ACT walikaa Kikao Dar na kuyapitisha Majina mawili, Anna Elisha Mgwira kuwa Mgombea wao wa Urais kwenye Uchaguzi Mkuu wa Tanzania  October 2015 na Mussa Yusuph kuwa Mgombea Mwenza wake.

4. Hashim Rungwe Spunda- Chama cha 

Ukombozi wa Umma (CHAUMA)

 


WASIFU wa Hashim Rungwe Spunda.
Hashim Rungwe Spunda, ni Wakili wa Mahakama Kuu ya Tanzania akifanya kazi zake kama wakili binafsi. Alizaliwa tarehe 01 Januari 1949 katika eneo la Ujiji, mkoani Kigoma (Ametimiza miaka 66 mwezi Januari mwaka huu). Hashim Rungwe ameoa na ana watoto watano.
ELIMU.
Mwaka 1975 alisoma ngazi ya Cheti katika Taasisi ya Kukuza Mauzo (Tafsiri yangu) ya Dar Es Salaam, mwaka 1977 alisoma Lugha ya Kifaransa kwa ngazi ya cheti katika taasisi ya “Alliance Francais” ya jijini Dar Es Salaam na kisha akasoma lugha ya kiarabu na elimu ya dini ya kiislamu kwa ngazi ya shahada katika Chuo Kikuu cha Mfalme Abdul kilichoko Saudi Arabia kati ya mwaka 1979 – 1982.
Mwaka 1989 – 1989 alisoma Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam ngazi ya Cheti, akichukua masomo ya Usimamizi wa Umma lakini pia mwaka 1991 alisoma ngazi ya cheti hapo hapo Chuo Kikuu, akijikita katika eneo la Historia ya Afrika na Falsafa ya Historia na Masuala ya Maendeleo (Tafsiri yangu).
Hashim aliendelea zaidi kielimu alipoamua kubobea katika sheria, alijiunga na Chuo Kikuu Huria Tanzania na kusoma shahada ya sheria kuanzia mwaka 1996 na kuhitimu mwaka 2003 na mwaka huohuo 2003 akasajiliwa kuwa wakili wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Kwa upande wa ajira, Hashim amefanya kazi na mashirika mbalimbali ya ndani ya nchi. Kwa mfano, kuanzia mwaka 1969 hadi 1973 amekuwa ni Ofisa aliyeajiriwa serikalini na kufanya kazi katika idara mbalimbali za sekta ya umma.
Kisiasa, Hashim aliwahi kuwa mwanachama imara wa TANU kati ya mwaka 1966- 1977 na kisha CCM kati ya mwaka 1977 – 1995. Ndiyo kusema kuwa wakati mfumo vyama vingi unaanzishwa mwaka 1992 yeye alikuwa mwanachama wa CCM kwa miaka mitatu zaidi kabla ya kuhamia NCCR Mageuzi mwaka 1996.
Alipokuwa NCCR alishiriki hatua mbalimbali za chama hicho katika kupigania mabadiliko, lakini alijiondoa NCCR mwaka 2012 na kuanzisha chama cha siasa kinachojulikana kama CHAMA CHA UKOMBOZI WA UMMA (CHAUMMA) na baada ya kuanzisha chama hicho alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kitaifa wa CHAUMMA mwaka 2014 na anashikilia wadhifa huo hadi hivi sasa.

 

 5.Fahmi Nasoro Dovutwa- Chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP)
 
WASIFU: Historia yake Fahmi Nasoro Dovutwa ni Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP). Alizaliwa Februari 27, 1957 mjini Kisarawe mkoani Pwani (Amefikisha miaka 58 Februari mwaka huu).
4. Hashim Rungwe Spunda
1 2 3

JINSI YA KUPIGA KURA TAREHE 25/10/2015

 
1.  Mkabidhi Msimamizi wa kituo kadi yako ya Kupigia Kura,
2.  Jina lako litasomwa kwa sauti kubwa ili Mawakala wa Vyama vya Siasa waliopo kituoni wasikie,
3.  Wasimamizi wa vituo, na hata Mawakala wa vyama vya siasa wakiwa na shaka wana haki ya kukuuliza maswali ili wajidhihirishe,
4.  Msimamizi wa kituo atakukabidhi karatasi 3 za kura  – yaani ya( Rais, Mbunge na Diwani) na pia atakuonyesha jinsi ya          kukunja karatasi hizo,
5.  Utaenda sehemu maalum iliyotengwa kwa ajili ya Kupiga Kura yako,
6.  Utaweka alama ‘V’ ndani ya chumba kilichopo chini ya Mgombea unayemtaka.
 7.  Utatumbukiza karatasi zako za Kura katika masanduku ya Kura kwa jinsi utakavyoelekezwa.
 8.  Kabla ya kuondoka ,utachovya kidole chako kidogo cha mkono wa kushoto katika Wino Maalum usiofutika kwa urahisi.
 
 

YAFAHAMU MAJIMBO YA MANISPAA YA ILALA



MAJIMBO YA ILALA, SEGEREA NA UKONGA – CCM ITAKUWA NA WAKATI MGUMU

Halmashauri ya Manispaa ya Ilala ipo kati ya Latitudo 6 na 7 kusini mwa Ikweta na kati ya Longitudo 39 na 40 Mashariki, ina eneo la kilomita za mraba 210 ambapo zaidi ya asilimia 75% ya eneo hilo ni eneo la mji. Manispaa hii imepakana na Manispaa za Kinondoni na Temeke kwa upande wa Kaskazini na Kusini, Mkoa wa Pwani kwa upande wa Magharibi na Bahari ya Hindi katika ukanda wa Pwani wenye urefu Kilomita 10 kwa upande wa Mashariki na hapa ndipo Ikulu ya Tanzania inapatikana.
Kwa mujibu wa Sensa ya watu na makazi ya iliyofanyika Agosti 2012, Ilala ina jumla ya wakazi wapatao 1,220,611, ambapo Wanaume ni 595,928 na wanawake ni 624,683
Manispaa ya Ilala ina Majimbo matatu (3) ya Uchaguzi ambayo ni Ilala lenye Kata 10, Ukonga lenye Kata 8, na Segerea lenye Kata 8.
Shughuli muhimu za kiuchumi katika Manispaa ya Ilala ni biashara, viwanda, kilimo na uvuvi pamoja na huduma za kiuchumi na kijamii. Pato la wastani la mkazi wa Manispaa ya Ilala ni sh.489, 204.00 kwa mwaka.
JIMBO LA ILALA
Kisiasa, jimbo hili limekuwa ngome ya Chama Cha Mapinduzi tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi nchini Tanzania. Katika chaguzi zote 1995, 2000, 2005 na 2010 – Ilala imeendelea kuipatia CCM ushindi mkubwa. Kwa ajili ya kuweka kumbukumbu vizuri tutaangalia chaguzi mbili zilizopita, ule wa mwaka 2005 na 2010.
Katika Uchaguzi wa mwaka 2005 jumla ya vyama 11 viliweka wagombea ubunge kwenye jimbo la Ilala. Kati yao, ni wagombea wawili tu ndiyo walionesha ushindani. Wagombea tisa walipata jumla ya kura 2917 sawa na asilimia 5.9. Mgombea wa CUF wakati huo Omar Mnyanga Ahmad alipata kura 9,637 sawa na asilimia 19.6 na Azzan Zungu Mussa wa CCM aliibuka na ushindi mkubwa wa asilimia 74.5 uliotokana na kura 36,629.
Katika uchaguzi wa mwaka 2010, jimbo la Ilala lilishuhudia ukuaji wa upinzani. Mara hii idadi ya wapiga kura ilishuka na hata ushindi wa mbunge wa CCM aliyetetea kiti chake kwa mara ya pili ulikuwa mdogo. Vyama 11 viliweka wagombea ambapo CCM ikimsimamisha Azzan Zungu ilipata kura 25,940 sawa na asilimia 66.77 na CHADEMA ikaibuka katika nafasi ya pili ikiwa na kura 8,053 sawa na asilimia 20.73 huku CUF ikiwa nafasi ya tatu kwa kura 3,988 sawa na asilimia 10.27. Vyama vingine 8 vilipata jumla ya kura 472 sawa na asilimia 1.22. Uchaguzi huu ulishudia kuporomoka kwa ushindi wa Zungu kutoka asilimia 74.5 mwaka 2005 hadi 66.77 mwaka 2010.
Jimbo la Ilala linakabiliwa na tatizo kubwa la askari wa jiji kunyanyasa wamachinga, ukosefu wa miundombinu ya uhakika (barabara) na ukusanyaji kodi mkubwa ambao haulingani na maendeleo halisi wanayopata wananchi. Hata hivyo, kukosekana kwa mtandao wa uhakika wa vyama vya upinzani katika jimbo hili, ukaribu wa mbunge wa Ilala kwa vijana wa mjini, vyama vya wapinzani kutokujua wapiga kura halisi wa Ilala (Wengi wanafanya kazi na biashara Kariakoo na Ilala huku wakiishi nje ya jimbo hilo) huku CCM ikijua wapi itawapata wapiga kura hao, na kukosekana kwa mpinzani wa uhakika mwenye uzoefu na jimbo hilo – ni sababu ambazo zina faida kubwa kwa CCM.
CCM wanataraji kumrudisha Azzan Zungu na hivyo jimbo la Ilala linaweza kuchukuliwa tena na CCM walau kwa ushindi wa asilimia 50 – 55, japokuwa akitokea mshindani imara kutoka vyama vya UKAWA atapunguza ushindi wa CCM kwa kiasi kikubwa.
JIMBO LA SEGEREA
Segerea imekuwa sehemu ya jimbo la Ukonga tangu uchaguzi Mkuu wa Mwaka 1995. Dr.Militon Makongoro Mahanga amekuwa mbunge wa jimbo la Ukonga (Segerea ikiwamo) kutokea mwaka 2000 hadi 2010. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilipotangaza kugawa baadhi ya majimbo kabla ya uchaguzi wa mwaka 2010, jimbo la Ukonga liligawanywa mara mbili na kuzaa jimbo la Segerea.
Katika Uchaguzi wa Mwaka 2005 ambao Segerea ilikuwa sehemu ya jimbo la Ukonga, Makongoro Mahanga wa CCM alipata kura 126,955 sawa na asilimia 62.7 ya kura zote za jimbo la Ukonga la wakati huo (likijumuisha Segerea), alifuatiwa na Bethuel Pori Heko wa CUF aliyepata kura 51,519 sawa na asilimia 25.4 na wa tatu alikuwa Jacob Chacha Florence wa CHADEMA aliyepata kura 12,297 sawa na asilimia 3.8. Wagombea wengine 12 waliotokana na vyama 12 ambavyo havijatajwa hapa – walipata jumla ya kura 11,833 sawa na asilimia 5.9 ya kura zote. Jumla ya vyama 15 vilisimamisha wagombea.
Mwaka 2010 wakati jimbo la Ukonga lilipogawanywa na Segerea kuzaliwa, Makongoro Mahanga wa CCM alikuja kugombea Segerea na alishinda kura za maoni ndani ya chama chake, safari hii ikionekana angekuwa na kazi nyepesi kwa sababu jimbo la Segerea lina kata chache tu. Uchaguzi wa mwaka 2010 ulikuwa mgumu sana kwa Makongoro Mahanga na CCM. Matokeo ya mwisho yaliyotangazwa yanaonesha alijipatia ushindi mwembamba mno wa asilimia 41.7 dhidi ya asilimia 37.49 za CHADEMA na asilimia 17.94 za CUF. Asilimia hizo zilitokana na kura 43,554 za CCM, kura 39,150 za CHADEMA na kura 18,737 za CUF, ambapo CCM ilimsimamisha Makongoro Mahanga, CHADEMA ikamuweka Fred Tungu Mpendazoe na CUF ikimsimamisha Kimangale Ayoub Musa.
Ndio kusema, kama UKAWA ingekuwepo mwaka 2010, kura za CHADEMA na CUF zingetosha kuipa UKAWA ushindi wa asilimia 55.94 na kuipita CCM kwa asilimia 14.24. Hivyo, jimbo la Segerea kwa mwaka huu 2015 lina kila sababu ya kwenda chini ya vyama vya UKAWA ikiwa vitasimamisha mgombea mmoja na awe mtu anayefahamika kama ilivyokuwa kwa Mpendazoe mwaka 2010. Japokuwa taarifa zilizopo ni kuwa, Bwana Mpendazoe hatagombea tena katika uchaguzi wa mwaka huu 2015.
Dr. Militoni Makongoro Mahanga bado anaweza kurejeshwa na CCM kwa sababu ya uzoefu wake na hata mtandao wake ndani ya CCM, lakini ikiwa atasimama tena au ataletwa mgombea mpya, jambo hili halitakuwa kitisho kikubwa kwa UKAWA ikiwa wataweka mtu anayeuzika. Kwa kifupi, jimbo la Segerea ni kati ya maeneo ambayo CCM ina wakati mgumu sana kutokana na kuchokwa kwa chama chenyewe na hata Mgombea waliyenaye, sababu kuu zikiwa kushindwa kukidhi haja ya maendeleo ya wananchi kama ambayo walitegemea.
JIMBO LA UKONGA
Hili ndilo jimbo mama ambalo taarifa zake zimeelezewa katika sehemu ya uchambuzi wa jimbo la Segerea, kwa sababu miaka ya 2000 – 2010 jimbo hili liliijumuisha Segerea kama sehemu yake kabla ya kugawanywa na Segerea kujitenda. Kwa sababu hiyo, Uchambuzi juu ya jimbo la Ukonga utaanzia mwaka 2010 kwa kuzingatia kuwa miaka ya nyuma imekwishaelezwa.
Katika uchaguzi wa Mwaka 2010 baada ya Makongoro Mahanga kugombea Segerea, jimbo mama la Ukonga lilibaki peke yake na hivyo kufanya uchaguzi Mkuu kama lilivyo (bila kuhusisha Segerea). Jumla ya vyama 12 viliweka wagombea katika jimbo hili na mvutano mkubwa ulijitokeza kati ya CCM na CHADEMA ambapo mgombea mpya wa CCM Eugen Mwaiposa Elishiringa alijizolea kura 28,000 sawa na asilimia 53.07 ya kura zote huku Binagi James Chacha wa CHADEMA akipata kura 17,059 sawa na asilimia 32.34 ya kura zilizopigwa. Mgombea wa CUF Heko Bethuel Pori alijipatia kura 5,220 sawa na asilimia 9.89. Wagombea wengine kutoka vyama 9 walipata jumla ya kura 1,470 sawa na asilimia 2.8 ya kura zote.
Joto la siasa katika jimbo hili limekwishapanda sana kwa sababu Meya wa Manispaa ya Ilala Jerry Silaa analihitaji jimbo hilo kwa udi na uvumba. Pamoja na kutofanya vizuri katika nafasi yake ya umeya ukizingatia kuwa Ilala imeendelea kuwa na matatizo makubwa ya wazi yasiyotatulika (Mfano: Masoko kuwa machafu kupita kiasi huku makampuni ya ushuru yanachukua mabilioni ya pess kinyemela), bado Silaa ambaye ana nafasi kubwa ya kupitishwa na CCM – atakuwa karata muhimu sana kwao. Vyama vya UKAWA ili kulipata jimbo la Ukonga vitapaswa kupata mgombea kijana (Chini ya Miaka 40) mwenye sifa na mvuto kuliko Jerry Silaa na tena awe mtu mwenye uzoefu na umaarufu wa kutosha kupambana na Silaa wa CCM. Jimbo la Ukonga litakuwa gumu kwa pande zote UKAWA na CCM na upande wowote ambao utajipanga kimkakati, atalichukua.



NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR