Sunday, November 3, 2013

Tafakari ya masomo ya leo dominika ya 31 mwaka C 03/11/13

Somo La Kwanza: Hek. 11:22-12:2
Wimbo Wa Katikati: Zab. 145: 1-2, 16-18, 123-14 (K)
Somo La Pili: 2 Thes.1: 11-2:2
Injili: Lk. 19: 1-10
Tafakari y ya masomo:
Injili ya leo, inatuadithia juu ya mtosa ushuru Zakayo. Zakayo alikuwa na mapungufu makuu mawili. Moja, alikuwa na upungufu wa asili, alikuwa mfupi wa kimo. Katika msongamano mkubwa uliokuwa unamfuata Yesu, alikuwa hana nafasi ya kumwona kwani watu warefu wangemzuia. Pili, alikuwa na upungufu wa kijamii. Kazi yake ya kutosa ushuru ilimfanya achukiwe na Wayahudi wenzake. Kwani, watosa ushuru walikuwa wadanganyifu kwa waliwatosa watu ushuru mkubwa zaidi, huku wakijitajirisha na pesa za ziada walizotosa watu. Hivyo basi, hawakupendwa na jamii ya  Wayahudi.

Pamoja na mapungufu haya ya kiasili na hata ya kijamii, ambayo yangekuwa sababu ya kutosha kabisa ya kumzuia Zakayo asimuone Yesu. Zakayo hakukubali, nafasi hii ya kumuona Yesu, impite. Alitoka mbio, akapanda juu ya mkuyu ili amuone Yesu. Yesu alizizawadia juhudi za Zakayo kwa kumuita, “Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa  kushinda nyumbani mwako.”

Yesu anamtumia Zakayo kutuonesha jinsi Mungu anavyozijali juhudi za wale wajitahidio bila kukata tamaa kutokana na mapungufu waliyonayo. Kama Zakayo asingejitahidi kutafuta mbinu za kumuona Yesu, hata kwa kupanda mkuyuni, angekufa bila kutimiza ndoto yake ya kutaka kumuona Yesu. Mara nyingi tumejiona kuwa kutokana na mapungufu yetu hatuwezi kutimiza ndoto zetu maishani. Tunapoteza muda tukisema kama ningekuwa na hili ama lile ningefanya hivi ama vile. Kama ningezaliwa mwanamke ama mwanaume ningefanya hili wala lile. Kama ningezaliwa katika familia iko hivi ningefanya hili ama lile; Kama ningekuwa na uwezo huu ama ule basi mambo yangu yangeenda vizuri; Kama muda huu, ndio ningekuwa mwanafunzi, ningesoma sana ili niwe na maisha mazuri zaidi. Mwanafunzi naye anasema, ningekuwa na akili kama fulani, ningefanya vizuri; ama ningekuwa shule bora zaidi ningesoma kwa bidii sana. Hizi ndoto za mchana hazitatusaidia. Kitakachotusaidia ni kukubali mapungufu yetu na hapo kuangalia ni kitu gani Mungu ametuwekea karibu kitakachotuwezesha kutimiza ndoto zetu. Kama Zakayo asingekuwa mtu wa jitihada, asingeona kuwa angeweza kupanda mtini na hivyo kuyashinda mapungufu yake. Kama Zakayo asingekuwa ni mtu wa maono, mkuyu ungeendelea kubakia mkuyu tu huenda ungekuwa mojawapo ya vikwazo vya kumzuia asimuone Yesu. Angeendelea kulalamika na hata kuulalamikia mkuyu. Zakayo alipoutazama mkuyu aliona jinsi unavyoweza kutumika kuwa kifaa cha kumwezesha kumuona Yesu na siyo kikwazo cha kumuona Yesu. Ufupi wake, japo ulikuwa ni upungufu wa asili ulikuwa sababu yake ya kuzitumia jitihada zake. Zakayo alikuwa na mtazamo chanya katika maisha. Mtazamo huu ulimfanya kuweza kuvibadilisha vizingiti katika njia yake ya maisha na kuvifanya ngazi ya kumwezesha kutimiza ndoto yake katika maisha. 

Sisi pia, inatubidi, kuangalia kwa makini kabisa ni mapugufu gani yanayotufanya tushindwe kutimiza ndoto zetu maishani.(ulevi? Wivu? Tamaa? Hasira? Uwongo? Uadui? Chuki? Uvivu? Nk.) Baada ya kuyaona mapungufu hayo, tuangalie kwa makini, tena sana, ni kitu gani Mungu ametuwekea karibu nasi ambacho kitatufanya tuweze kuyashinda mapungufu haya. Hakuna na tatizo lisilo na suluhu kwa wale wanaoamini. Ila tu ni lazima tukazie macho mapungufu yetu, tuangalie pia na zile nyenzo Mungu alizoweka karibu nasi ambazo zitatuwezesha kukwea na kuvishinda vikwazo hivvyo na baada ya kuviona tumuombe Mungu kwa bidii zote, kwani  yeye alikuja ili tuwe na uzima kamili (Jn 10:10) na siyo mapungufu. Zakayo aliona mti wa mkuyu, wewe pia inakubidi utafute mkuyu wako utakao panda, na hapo utamsikia Bwana akikuambia, “Leo, imenipasa niwe nyumbani mwako.” AMINA

Friday, November 1, 2013

Maadhimisho ya Siku ya Watakatifu wote na siku ya Marehemu wote

Papa afafanua kiini cha Maadhimisho ya Siku ya Watakatifu wote na siku ya Marehemu wote.



BabaMatakatifu Francisko akiendelea kutoa tafakari juu ya sala ya Nasadiki, kwa Jumatano hii, alilenga zaidi katika usharika na Watakatifu, kama Kateksimu ya Kanisa Katoliki inavyotukumbusha sisi kwamba, usharika huu ni kwa Mambo Matakatifu na kati ya watu Watakatifu (No. 948 ).

Papa alizama zaidi katika sehemu ya Pili ya kuw ana usharika na Marehemu Watakatifu , ukweli unaohitaji ufafanuzi zaidi katika imani yetu, akieleza pia kwamba, hutukumbusha pia kwamba, hatuko pweke, lakini kuna uwepo wa usharika wa maisha kwa wale wanaokuwa wa Kristu. Usharika mmoja unaoundwa na imani , katika ukweli wake, neno hili Watakatifu hurejea wale wanao mwamini Yesu Kristu kuwa ndiye Bwana wa Maisha na hivyo humwilishwa kwake Yeye ndani ya kanisa kupitia ubatizo. Na kwa namna hiyo , Wakristu wa kwanza waliitwa pia Watakatifu.

Papa aliendelea kufundisha , Usharika wa Watakatifu ni kina halisi cha maana ya Kanisa kwa sababu kama wakristu kupitia Ubatizo , tunafanywa kuwa washiriki wa maisha ya usharika mmoja na upendo wa Utatu Mtakatifu. Na hivyo sote tunaunganishwa mmoja kwa mwingine na kiungo cha ubatizo katika Mwili wa Kanisa. Na kupitia usharika huu wa kidugu, tunawekwa karibu zaidi na Mungu, na tukitakiwa kusaiidiana mmoja kwa mwingine kiroho.

Papa alieleza na kuirejea Injili Yohana ambayo inasema kwamba , kabla ya mateso yake, Yesu aliomba kwa Baba kwa ajili ya umoja kwa wanafunzi wake kwa maneno haya : “Naomba ili wote wawe kitu kimoja kama wewe, Baba , ulivyo ndani yangu , nami ndani yako. Naomba wawe kitu kimoja kusudi ulimwengu upate kuamini kwamba wewe ndiye uliyenituma "( 17:21). Kanisa , katika kweli yake kamili , ni usharika na Mungu , usharika wa upendo na Kristo na Baba katika Roho Mtakatifu shina la usharika huo. . Uhusiano huu baina ya Yesu na Baba ni dhamana kati ya Wakristo, iwapo pia sisi tumo ndani yake katika umoja huu, na tanuru la moto huu wa upendo katika Utatu Mtakatifu, basi tunaweza kweli kuwa na moyo na roho moja kati yetu kwa sababu upendo wa Mungu unauguza ubinafsi wetu , chuki zetu, utengano na miganyiko yetu ya ndani na nje.

Papa Francisko amesema, iwapo ushariki huu chanzo chake ni mzizi wa upendo ambao ni Mungu, basi pia kuna sababu za kufanya hima kutoa jibu landiyo katika muungano huu na Mungu, maisha ya ushirika wa udugu unaoongoza katika kuwa msharika na Mungu.

Hii ni sehemu ya pili ya usharika, ambayo Papa alitoa msisitizo zaidi, kuwataka watu wa Mungu,kupta uelewa mpana kwamba, imani yetu inahitaji msaada wa wengine , hasa katika nyakati ngumu. Alisema, tazama pia jinsi ilinavyokuwa vizuri kutoa msaada kwa mwingine katika maajabu haya ya imani! Papa alieleza kukemea mwelekea kukubatia tabia ya kutaka kujifungia binafsi, hata katika mazingira ya kidini, kiasi kwamba, inakuwa hata vigumu kwa wengine, hata kuomba msaada wa kiroho, kwa wale wenye uzoefu katika maisha haya ya Kikristu.

Papa alihimiza katika nyakati hizi ngumu ni muhimu kuwa imani kwa Mungu kupitia sala, na wakati huo huo, ni muhimu kupata ujasiri na unyenyekevu kuwa wazi kwa wengine. Papa amekumbusha ushirika wa watakatifu ni familia kubwa, ambapo vipengele vyote ni kusaidia na kusaidiwa yaani kusaidiana mmoja kwa mwingine. Kushirkiana na wengine katika parokia zetu, katika vyama , jumuiya, harakati na vikundi, kama sehemu ya maisha katika safari yetu ya imani, ni kutochoka kuomba msaada wa maombezi na faraja ya kiroho. Ni wakati wetu wa kusikiliza na kuwasaidia wale ambao hawaja jiunga nasi katika safari hii.

Papa alikamilisha Katekesi yake kwa kuchambua kipengele kingine cha usharika wa watakatifu, akisema kwamba, ushariki wa wakatifu huenda zaidi ya maisha ya dunia, inakwenda zaidi ya kifo kwa kuwa huduma milele. Usharika wa kiroho tunaopokea wakati wa Ubatizo hauvunjwi na kifo , lakini umeinuliwa na ufufuko wake Kristu, unao ipeleka roho katika mapito ya utimilifu wa maisha ya milele.

Papa aliendelea kubaini kwmba, kuna dhamana ya kina na isiyokuwa na mwisho kati ya wale ambao bado mahujaji katika dunia hii na wale ambao wamevuka kizingiti cha kifo na kuingia katika umilele. Wote hao huuundwa wakati wa ubatizo hapa duniani,na nafsi hutakatifushwa toharani na kufanywa wenye heri, kuingia katika makazi ya mbinguni ambako ni makazi ya familia moja kubwa. Ushirika huu kati ya nchi na mbinguni ni barabara ya maombezi , ambayo ni aina ya juu ya mshikamano, na pia ni msingi wa maadhimisho ya kiliturujia ya Watakatifu wote na Maadhimisho ya Marehemu wote kama itakavyokuwa siku chache zijazo.

Papa alimalizia kwa kumtaka kila mmoja alifurahie fumbo hili , na kumwomba Bwana neema zake , ili tuweze kuwa karibu zaidi naye na katika usharika na waamini wote, wake kwa waume ndani ya kanisa.
Wito wa Kuombea Iraki
Baada ya Katekesi, Papa akisalimia makundi mbalimbali, pia alilitaja kundi la mahujaji kutoa Iraki ambao walikuwa wakiwakilisha makundi mbalimbali ya kidini, toka yanayojionyesha kama ni utajiri wa Ukristu katika taifa la Iraki . Kundi hili liliongozwa na Kardinali Tauran Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya majadiliano na dini zingine. Papa alitoa wito kwa watu wote kukumbuka kuliombea taifa la Iraki ambalo kila kukicha hukumbana na majanga ya fujo na ghasi za kusitisha zinazofaywa na makundi mabalimbali. Tusali ili Iraki ipate kurejea katika njia ya majadiliano, maridhianao , amani, umoja na utulivu wa kudumu kitaifa.

Sikuku ya Watakatifu woteleo tarehe 01/11/2013

Somo La Kwanza: Ufunuo.7:2-4, 9-14
Wimbo Wa Katikati: Zaburi: 24:1-6 (K) 6
Somo La Pili: 1 Yoh. 3:1-3
Injili: Mathayo 5:1-12
Sikukuu ya Watakatifu wote
Kalenda ya Kanisa Katoliki inajumuisha sikukuu za watakatifu wengi na hata wafia dini. Lakini Novemba mosi, ni sikukuu ya watakatifu wote. Kweli tunasherehekea sikukuu za watakatifu fulani fulani katika siku tofauti lakini Novemba Mosi, tunasherehekea sikukuu ya watakatifu wote, wale tunaowajua na wale tusiowajua. Watakatifu ni wengi na wamefanya kazi nyingi tofauti tofauti lakini zote zikiwa na umuhimu wake katika kuiendeleza na kuikuza imani yetu. Watakatifu ni wengi na hatuwezi kuwajua wote. Hivyo sikukuu hii inawajumuisha pamoja kama kundi moja la watu walioyaishi maisha yao vyema hapa duniani. Sikukuu hii ni kichocheo katika maisha yetu ya imani kwani inatubidi tufuate nyayo zao, tuishe tukimtegemea Mungu zaidi ya chochote. Watakatifu walio pamoja na Mungu mbinguni wanatuombea na kutupa moyo sisi watakatifu tulio safarini kwenda mbinguni. Watakatifu tunao sherekea siku yao leo ni  mashujaa wa imani na kielelezo kwetu, wanatupa moyo kuwa, “Ndiyo kumfuata Kristo kunawezekana.” Kesho Novemba mbili tutawakumbuka marehemu wote. Hawa ni ndugu zetu, wasafiri wenzetu ambao tayari wameiacha dunia hii lakini bado hawajafika mbinguni, wanavikwa mavazi meupe (Ufu.7:9) wanatakaswa kabla ya kuingia mbinguni
Sherehe ya watakatifu wote inatukumbusha kuufuata wito wetu wa kuwa wana wa Mungu. Baada ya mwanadamu kuupoteza utu wake kwa kutenda dhambi, Mungu alimtuma mwanae ulimwenguni ili wale wote wamuaminio wapate ufalme wa milele (Yn. 3:16). Watakatifu wameshaupata ufalme huu wa milele ni wajibu wetu sisi wakristo kufuata mfano wao. Wao walishinda adui wa roho kwa kutumaini neema za Mungu.
Injili ya leo inatuonesha furaha ya watakatifu ilivyo, na njia inayotuwezesha kufika kufika mbinguni. Tunasikia kwamba, “Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.” Kumbe basi, tukitaka vita vya miaka michache hapa duniani vitatuletea furaha na heri ya milele. Inatubidi basi tuvumilie kabisa katika imani yetu, tujaribu kila tuwezavyo tuvishinda vishawishi kwani Mungu hatajaribu zaidi ya neema aliyotupa kuvishinda vishawishi hivyo.  Watakatifu tunaowakumbuka leo, wanatupenda wanatuombea kwa Mungu  ili tuwe pale walipo, karibu na Mungu na kwenye heri ya milele.  Sikukuu hii haina budi kuamsha matumaini makubwa mioyoni mwetu.
Sala:
Ee Mungu niongezee kiu na njaa ya kuyafanya mapenzi yako na siku moja niwe pamoja na watakatifu mbinguni tukikusifu na kuiombea dunia.
Amin

Thursday, October 31, 2013

Sherehe za Nadhari za kwanza Wanovisi wa Shirika la Carmelite sisters

Wanavosisi watano wa shirika la masista wakarmel wamisionari wa Mt. teresia wa Mtoto Yesu, watarajia kufunga naziri za kwanza za kitawa, ambao ni
  1. Betrice Faustine Urio
  2. Dorice Kalebi Tarimo
  3. Emeritha Joseph Kavishe.
  4. Hemilete Masika Sivatungika
  5. Salange Kavuke Syaghuswa.
 Ibada itafanyika katika Parokia ya Ekaristi Takatifu Lushoto, siku ya Ijumaa ya tarehe 01/11/2013,siku ya  Sherehe ya Watakatifu wote, Na itaongozwa na Askofu wa Jimbo la Tanga: Mhashamu Askofu Anthony Banzi.
 Na baada ya Ibada itafuata Tafrija fupi ya kuwapongeza katika nyumba ya wito wa kitawa ya Jumuiya ya Bikira Maria wa Mlima Karmel - lushoto KIALO,

Mungu awaongeze na Mt. Teresia wa Mtoto Yesu awe Mlinzi wako...

Tuesday, October 29, 2013

MASOMO YA DOMINIKA YA 31 YA MWAKA C. JUMAPILI TAREHE 03/11/13

JUMAPILI DOMINIKA YA 31 ya Mwaka C.
      RATIBA ZA IBADA 
KIGANGO CHA MH. ISIDORI BAKANJA- BOKO.
MISA YA KWANZA 12:15-2:00 ASUBUHI
MISA YA PILI     SAA 2:00-4:00 ASUBUHI
MISA YA TATU SAA 4:00-5:30 ASUBUHI
KIGANGO CHA MT. FRANCIS WA ASIZ-MBWENI 
MISA YA KWANZA SAA 1:10-3:00 ASUBUHI
MISA YA PILI SAA 3:00-4:30 ASUBUHI

KIGANGO CHA MT. RAFAEL-MBWENI MALINDI
IBADA NI MOJA TU ITAANZA SAA 3:00-5:00 ASUBUHI.


KIGANGO CHA ANTHONY WA PADUA-MBWENI TETA
MISA NI SAA 3:00-5:00.




DOMINIKA 31 ya mwaka C (masomo)
SOMO 1. HEK. 11:22- 12:2
Ulimwengu wote mbele zako Bwana, ni kama chembe moja katika mizani, na mfano wa tone moja la umande lishukalo asubuhi juu ya ardhi. Lakini wewe unawahurumia watu wote, kwa sababu unao uweza wa kutenda mambo yote; nawe wawaachilia wanadamu dhambi zao, ili wapate kutubu. Kwa maana wewe wavipenda vitu vyote vilivyopo, wala huchukii kitu cho chote ulichokiumba. Kwa kuwa hungalifanya kamwe kitu cho chote kama ungalichukia; tena kitu cho chote kingaliwezaje kudumu, ila kwa mapenzi yako? Au kitu kisichoumbwa nawe kingaliwezaje kuhifadhika? Lakini wewe unaviachilia vyote, kwa kuwa ni vyako, Ee Mfalme mkuu, mpenda roho za watu; maana roho yako isiyoharibika imo katika vyote. Kwa hiyo wawathibitishia kidogo kodogo hatia yako, wale wanaokengeuka kutoka katikala  njia njema; wawaonya, ukiwakumbusha kwa mambo yale yale wanayokosa, ili waokoke katika ubaya wao, na kukuamini wewe Bwana.

SOMO 2. 2THE. 1:11- 2:2
Kwa hiyo twawaombea ninyi sikuzote, ili Mungu wetu awahesabu kuwa mmekustahili kuitwa kwenu, akatimiza kila haja ya wema na kila kazi ya imani kwa nguvu; jina la Bwana wetu Yesu litukuzwe ndani yenu, nanyi ndani yake, kwa neema ya Mungu wetu na ya Bwana Yesu Kristo. Basi, ndugu, tunakusihini, kwa habari ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo, na kukusanyika kwetu mbele zake, kwamba usifadhaishwe upesi hata kuicha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, wala kwa waraka unaodhaniwa kuwa ni wetu, kana kwamba siku ya Bwana imekwisha kuwapo.

INJILI. LK. 19:1-10
Yesu alipoingia Yeriko alipita katikati yake. Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo. Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kupita njia ile. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani kwako. Akafanya haraka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha. Hata watu walipoona, walinung’unika wote, wakisema, ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi. Zakayo akasimama,  akamwambia Bwana, Tazama, Bwana nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang’anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. Yesu akamwambia, leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuoka kile kilichopotea.
             
  1.  Jumapili ya tarehe 03/11/13 tutakuwa na kikao cha halmashauri ya VIWAWA Parokia, kikao kitaanza mara baada ya misa ya pili...mahali na parokiani boko fika bila kukosa.
  2. Kigango cha mt. Raphael jumapili tarehe 3/11/2013 ni siku ya mnada wa mavuno waamini wote, ndugu jamaa na marafiki unaalikwa kuungano nao.
  3. jiandae na semina ya vijana wote wa parokia ya boko pamoja na parokia jirani tarehe 23/11/2013 taarifa kamili utazipata jumapili.


  1. tunawakumbusha vijana wote kuendelea kulipa ada kwa maendeleo ya chama chetu..... mapendo sana malipo kwa njia ya benk kwa jina na number hii :viwawa parokia ya boko account no 01524526820100 crdb bank tegeta branch
JIANDAE NA ZIARA YA UINJILISHAJI MWAKA 2014.....................

Monday, October 28, 2013

MJUE Kardinal Polycarp Pengo

Polycarp Pengo ni kardinali wa pili kutoka Tanzania, akiwa aliteuliwa mara baada ya kifo cha Laurean Rugambwa, kardinali wa kwanza kutoka kusini kwa Sahara.

Maisha yake.

Alizaliwa Mwazye (mkoa wa Rukwa) tarehe 5 Agosti 1944.
Baada ya masomo ya ngazi mbalimbali, alipewa upadrisho mwaka 1971 na Askofu Charles Msakila wa Jimbo Katoliki la Sumbawanga, akasoma teolojia ya maadili huko Roma, Italia, akijitwalia digrii ya udaktari mwaka 1977.
Kisha kufundisha somo hilo kwa muda mfupi kwenye seminari kuu ya Kipalapala (mkoa wa Tabora), alichaguliwa kuwa gombera wa seminari kuu ya Segerea hadi mwaka 1983.
Aliteuliwa askofu wa Nachingwea tarehe 11 Novemba 1983, akapewa daraja takatifu hiyo na Papa Yohane Paulo II tarehe 6 Januari 1984.
Tarehe 17 Oktoba 1986 alihamishiwa jimbo jipya la Tunduru-Masasi.
Tarehe 22 Januari 1990 alifanywa askofu mwandamizi wa Dar-es-Salaam na mwaka 1992, kardinali Laurean Rugambwa alipojiuzulu, akawa askofu mkuu.
Aliteuliwa na Yohane Paulo II kuwa kardinali tarehe 21 Februari 1998, akikabidhiwa parokia ya Nostra Signora de La Salette mjini Roma.
Pamoja na majukumu mbalimbali katika idara za Papa, tangu mwaka 2007 hadi 2013 alikuwa mwenyekiti wa Umoja wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki ya Afrika na Madagaska

Historia (Kanisa Katoliki)

Imani

, Imani,


Ingawa kwa Kiswahili neno imani lina maana mbalimbali (k.mf. "huruma"), ile kuu inahusiana na kitenzi kuamini, kinachofanana na kusadiki. Hapo ni kukubali ukweli wa jambo lisiloweza kuthibitishwa.
Katika dini msingi wake ni mamlaka ya Mungu aliyeshirikishwa ukweli huo kwa njia ya ufunuo maalumu ili kumsaidia binadamu amjue yeye, ajifahamu pamoja na maisha yake duniani na ahera.
Kwa msingi huo, au wa namna hiyo, mtu anaweza kushikilia jambo bila ya uthibitisho mwingine, ingawa pengine Ukristo unatia maanani pia akili katika ujuzi wa ukweli.
Kadiri ya Mtume Paulo imani ikifuatana na tumaini na upendo ni adili kuu mojawapo, msingi, mzizi na chanzo cha wokovu.

Roho ya imani katika maisha ya kiroho

Kila mara mtu anafuata ama umbile, asipopita fikra za kibinadamu tu, ama imani, anapolenga mbinguni kwa njia ya utakatifu. Roho hizo zinazotuongoza maishani ni namna maalumu za kupima, kuona, kuhisi, kupenda, kushabikia, kutaka na kutenda. Basi, roho ya imani ni kupima yote kwa mtazamo wa juu ambao unapita maumbile na kutegemea mamlaka ya Mungu katika kujifunua, na ukweli wake katika kutushirikisha utukufu. Tunaelewa zaidi roho ya imani tukiangalia iliyo kinyume chake, yaani upofu wa roho unaozuia mtu asione mambo ya Mungu isipokuwa kidunia na kutoka nje. Hivyo Israeli haikuelewa uteuzi wake kadiri ya ukweli wa Mungu ulio wa juu kuliko ukabila au ubaguzi wowote.
Imani ina mitazamo mipana kuliko huo kutokana na usahili wake unaoshiriki hekima ya Mungu. Juu sana kuliko mifuatano ya mawazo, ni tendo sahili ambalo tunamsadiki Mungu anayefunua na papo hapo anajifunua. Kwa tendo hilo lipitalo maumbile tunaambatana naye pasipo udanganyifu na hivyo katika giza tunalenga kutazama mambo ya Mungu, juu kuliko hakika zote za kibinadamu. Hakika inayotokana na imani tuliyomiminiwa na Mungu, inapita hata hakika ya akili tunayoweza kujipatia kwa kuzingatia miujiza inayothibitisha ufunuo wake.
Imani ni zawadi ya Mungu: “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu” (Ef 2:8). Ni kama hisi ya Kiroho inayotuwezesha kusikia ulinganifu wa mafumbo aliyotufumbulia, yaani kusikia sauti yake kabla hatujakaribishwa kumuona uso kwa uso.
“Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kujua tuliyokirimiwa na Mungu, nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. Basi, mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni. Lakini mtu wa rohoni huyatambua yote, wala yeye hatambuliwi na mtu. Maana, ni nani aliyefahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo” (1Kor 2:12-16). Ili ifanye hivyo imani inasaidiwa na vipaji vya akili na hekima, lakini yenyewe ndiyo inayotufanya tushike Neno la Mungu pasipo udanganyifu.
Ingawa mafumbo yake ni ya giza kwetu, adili la imani ni bora kuliko ujuzi mwangavu walionao malaika kwa umbile lao, kwa sababu imani tunayomiminiwa inalingana na uzima wa milele, kwa kuwa ndiyo mbegu yake. Malaika wenyewe walihitaji zawadi hiyo waweze kulenga hali ipitayo maumbile waliyoitiwa.
Mungu anapotujalia imani, anapenya roho yetu na kusema nayo si kwa mifuatano ya maneno, bali kwa wazo la ghafla. Imani ikifika, tunaachana na mfuatano wowote wa mawazo tuliokuwanao pamoja na sababu zake: tunaviweka chini ili imani ivikalie kama mtawala. Imani ikiangaza akili kwa mng’ao wa kweli zake, mara utashi unahisi joto la upendo wa Mungu.

Imani tuliyomiminiwa inatakiwa kustawi hadi kifo

Imani inatakiwa kukua kila siku. “Imani inaweza ikawa kubwa ndani ya Mkristo mmoja kuliko ndani ya mwingine, upande wa akili kutokana na hakika na imara kubwa zaidi katika kushika ufunuo, na upande wa utashi kutokana na utayari na utiifu au tumaini kubwa zaidi” kwa kuwa “imani tunayomiminiwa inalingana na zawadi ya neema, ambayo si sawa kwa wote” (Thoma wa Akwino). Yesu Kristo aliwasema wanafunzi wake kuwa “wa imani haba” (Math 6:30); kumbe alimuambia mwanamke Mkananayo, “Mama, imani yako ni kubwa!” (Math 15:28).
Imani inaweza kukua kwa upana na kwa dhati au nguvu. Inapanuka tunapozidi kujifunza yale yote Kanisa linayoyafundisha: wanateolojia wanayajua wazi, lakini si kwamba imani yao ni ya dhati na ya nguvu kadiri ilivyoenea. Kumbe tunakuta watakatifu wasiojua mengi katika hayo, lakini wanapenya mafumbo yalivyofumbuliwa na Injili kwa usahili. Mitume wa Yesu walimuomba imani hiyo waliposema, “Tuongezee imani” (Lk 17:5). Yesu akawaambia, “Yoyote mtakayoomba katika sala mkiamini, mtapokea” (Math 21:22). Tutayapokea hasa tukijiombea kwa udumifu yaliyo ya lazima au ya kufaa sana kwa wokovuwetu, kama vile ustawi wa maadili.

Ubora na uwezo wa imani

Thamani ya imani inapimwa na matatizo inayoyashinda katika majaribu: “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu… yeye aliyeambiwa: Katika Isaka uzao wako utaitwa, akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu… Kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahad, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto… Wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizungukazunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za [mbuzi]], walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya – watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao” (Eb 11:17-19, 33-34, 36-38). Mambo kama hayo yanatokea hata siku hizi. “Basi na sisi pia, tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu” (Eb 12:1-2).
“Mzingatieni Kristo aliyevumilia upinzani wa namna hiyo kutoka kwa wakosefu… Hapo katika tabu yoyote mtaona dawa katika msalaba wa Yesu. Humo mtakuta vielelezo vya maadili yote. Gregori Mkuu alisema tukiyakumbuka mateso ya Yesu hatutaona chochote kuwa kigumu au cha tabu tusiweze kukivumilia kwa subira na upendo” (Thoma wa Akwino). Imani ikistawi inatufanya kwa kawaida tuzidi kuhisi fumbo la Kristo; polepole hisi hiyo ipitayo maumbile inakuwa sala ya kumiminiwa yenye kupenya na kuonja, asili ya furaha na amani: “Furahini katika Bwana sikuzote; tena nasema, Furahini… Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu” (Fil 4:4,7).

Tuishije kwa roho ya imani?

Tunapaswa kuishi hivyo kwa kupima yote kwa mwanga huo wa juu: kwanza Mungu, halafu nafsi yetu, jirani na matukio yote.
Je, kuna haja ya kusema tumzingatie Mungu kwa imani? Bila ya shaka! Kwa kuwa mara nyingi tunamzingatia kwa dhana zisizo na msingi, kwa miguso ya kibinadamu mno na kwa maono yetu, badala ya kupitia ushuhuda alioutoa juu yake mwenyewe. Pengine hata tunaposali tunajisikiliza tu kwa kumkopesha Mungu mawazo yetu yanayotokana na umimi. Tunapojiamini kipumbavu tunaelekea kudhani huruma ya Mungu ni kwa ajili yetu, na haki yake kwa watu tusioelewana nao. Kumbe tukikata tamaa tunatilia shaka kimatendo upendo wa Mungu kwetu na huruma yake kuu. Kwa imani tunamuona Mungu kupitia mafumbo ya maisha na mateso ya Mwokozi na kupitia uhai wa Kanisa linalofanywa upya na ekaristi kila siku. Jicho la imani linasafika zaidi na zaidi kwa ufishaji wa hisi na maono, maoni na matakwa yetu: hapo tu unakuja kuanguka polepole ule utaj wa kiburi unaotuzuia tusione mambo ya Mungu au tuone tu vivuli vyake na tata zake.
Tunapaswa vilevile kujitazama kwa imani. Tukijitazama kibinadamu tu, tunaona ndani mwetu sifa za umbile ambazo mara nyingi tunazizidisha. Baadaye, majaribu yakituonyesha tulivyojidanganya tunavunjika moyo kwa urahisi. Kumbe kwa imani tunakuja kujua utajiri upitao maumbile ambao Bwana ametutia katika ubatizo na kutuongezea kwa ekaristi, yaani thamani ya neema inayotia utakatifu, ya uwemo wa Utatu mtakatifu pamoja na ukuu wa wito wa Kikristo. Tunakuja kujua pia vizuio vya ustawi wa uzima huo, k.mf. usahalifu wa mbegu ya uzima wa milele iliyopandwa ndani mwetu, na kiburi cha kipumbavu. Kwa mtazamo huo wa juu tunakuja kujua mapema kilema kinachotutawala na kivutio maalumu cha neema tulicho nacho, ambavyo cha kwanza kikomeshwe na cha pili kistawishwe.
Lakini tunayesahau zaidi kumtazama kwa imani ndiye jirani. Tunamtazama kibinadamu tu, tukiathiriwa na dhana zisizo na msingi, kiburi, wivu na vilema vingine. Kwa hiyo ndani yake tunakubali yale ambayo yanatupendeza kibinadamu, yanatufaidisha au kutukuza; kumbe tunahukumu yale ambayo yanatukinaisha, yanamfanya bora kuliko sisi na kutushusha. Dhambi ngapi za kuhukumu na kusingizia zinatokana na mtazamo huo uliofunikwa na utaji wa umimi! Tukijifunza kumtazama jirani kwa imani ni faida kubwa pande zote. Hapo tunakuja kuwaona wakubwa wetu kama wawakilishi wa Mungu, na kuwatii kwa moyo pasipo kuwasema. Tunaona kuwa wasiotupendeza wamekombolewa kwa damu ya Kristo, pengine ni viungo vya mwili wake vinavyokaribia moyo wake kuliko sisi: mara nyingi tunaishi miaka pamoja na watu safi tusitambue uzuri wa roho zao. Vilevile, tukija kuwatazama kwa imani wanaotupendeza, pengine tunavumbua wana maadili ya Kimungu kiasi cha kuzidisha na kutakasa mapendo tunayowaonea; pia kwa wema tunaona vizuio walivyonavyo kwa utawala wa Mungu na tunaweza kushauriana nao tusonge mbele katika njia yake.
Hatimaye tunapaswa kutazama kwa imani matukio yote ya maisha yetu, ya furaha na ya uchungu vilevile. Mara nyingi tunaridhika kuyaona upande wa hisi tu, au kwa akili iliyoathiriwa na dhambi. Mara chache tunayazingatia Kimungu, kwa kuona kwamba “katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema” (Rom 8:28): hata katika upinzani, matatizo makubwa yasiyotarajika na dhambi (tukiweza kujinyenyekesha kutokana nazo). Katika kukosewa haki na watu tunaweza kutambua haki ya Mungu ikiadhibu makosa ya siri ambayo hatulaumiwi na mtu; au tunahisi majaribu ya Kimungu, na utakaso unaokusudiwa kupatikana kwa njia ya hayo.
Kabla ya imani yetu kutakaswa kwa majaribu kadhaa ya aina hiyo, tujitahidi kukua katika imani, badala ya kupima yote kibinadamu tu. Ni lazima tujinyime mianga midogo na ya bandia ili tujaliwe ile ya juu; tuache kufuata mno akili yetu ili tuone uangavu mkuu wa mafumbo ya imani na kuishi kulingana nayo. Hivyo tunaelewa kwa nini hatutakiwi kuitikia vishawishi dhidi ya imani, bali kuvikataa au kuviruka kwa kukiri imani kwa dhati zaidi; Bwana anaviruhusu kwa maendeleo yetu tu.



Itaendeleaa ...........................

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR