Friday, March 27, 2015

Mwazo wa Juma kuu: Furaha, shangwe; mateso na huzuni!

Image result for sunday palms jesus in jerusalemMaadhimisho ya Jumapili ya Matawi, mwanzo wa Juma kuu ni kipindi cha: furaha na shangwe; mateso na huzuni; lakini pia ni kipindi cha matumaini kwa ajili ya ushindi wa Kristo mfufuka. Kanisa lina matumaini makubwa katika ile Siku ya kwanza ya Juma! Kanisa lataka kutuambia nini katika Jumapili hii ya matawi? Mwandishi mmoja anasema – kumfuata Kristo – mpole, kumfia Kristo ili tuweze kuuingia uzima wa milele pamoja naye. Ni lazima kumuiga Kristo katika sadaka ya kifo ili tumuige katika utukufu wa msalaba.
 Swali kubwa ni hili – kwa nini Mungu ameruhusu mateso? Nabii Ayubu – 31:37 – anapoongelea kuhusu mashindano ya mwisho anaomba Mungu ampe majibu. Jibu halionekani katika kitabu hiki cha Ayubu ila kinachoonekana ni kuwa fumbo la mateso lamezwa katika fumbo kuu la upendo la Mungu mwenyewe.
Kwa namna ya pekee, imani ya kikristo inaliishi fumbo hili – upendo mkuu wa Mungu. Haitoi jibu la moja kwa moja ni kwa nini ni kwa njia ya mateso ila twapata maelezo mbalimbali jinsi Mungu anavyotumia njia ya mateso kumkomboa mwanadamu. Mungu hutumia mateso ya mwanadamu ili kumkomboa mwanadamu. Ndiyo maana ya ibada yetu ya leo. Lakini fumbo labaki.
 Wainjili wetu wanaeleza historia ya mateso ya Yesu na kifo, lakini hawatoi jibu ni kwa nini lazima Yesu apitie njia ya mateso ili kutupatia wokovu. Ila wanaeleza matokeo yake kwamba kinachopatikana ni wokovu – matokeo ya mateso na kifo chake Kristo. Yaani matokeo yake ni wokovu wa mwanadamu.
 Mwinjili Marko – Mk. 15:39 – anasema tendo la kifo cha Yesu ndiyo sababu ya imani ya yule Akida – basi yule akida aliyesimama hapo alimwelekea, alipoona ya kuwa alikata roho jinsi hii, akasema, hakika huyu alikuwa mwana wa Mungu.
 Mwinjili Matayo – anaona ufufuko katika kifo cha Yesu – Mt. 27:52-53 – makaburi yakafufuka, ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala. Nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi.
 Mwinjili Yohani – Yoh. 19:30 – analinganisha kufa kwa Kristo na kutupatia roho – basi Yesu alipokwisha kuipokea ile siki, alisema, imekwisha, akainama kichwa, akaisalimu roho yake.
Mt. Paulo naye anaendelea kusaidia kutoa majibu anapowaandikia Wafilipi katika somo la pilia akiwaambia hivi: mwatakiwa kuwa wapole na wanyenyekevu na kuwa na mtazamo wa Kristo. Naye Kristo anaonesha wazi hilo – anajishusha na kuwa mwanadamu hata kufa msalabani.
  Habari juu ya mateso ya Kristo iko wazi katika somo la Injili. Ushuhuda wa imani anaotoa Mt. Petro juu ya ufuasi uko wazi katika fundisho la Yesu juu ya msalaba – Mk. 8:34-38 – mtu akitaka kuwa mfuasi wangu, ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake .... . Fundisho hili la imani linakamilishwa na maneno ya Yesu mwenyewe – ye yote yule anayetaka kunifuata ni lazima achukue msalaba wake na anifuate. Yawezekana pia katika maandiko haya ya Marko, anatoa mwaliko kwa wafuasi kumfuata Kristo kama anavyotualika.
Wote pamoja, Mwinjili Marko na Mtume Paulo – wanasisitiza haja ya kukubali mateso ili kukamilika katika maisha ya Kikristo. Ila wanaweka wazi kuwa hili si jambo la kibinafsi tu. Wote wanatambua kuwa katika Kristo hupatikana ukamilifu. Yesu kadiri ya Marko na Paulo ni zaidi ya mwalimu anayeongoza wengine tu. Anayefundisha watu ili wapate kuwa hai. Yesu ni uhai wenyewe, ni chanzo cha nguvu yetu sisi ya kumfuata yeye.
Ukiangalia kwa umakini wimbo kwa Kristo katika somo la Pili – jambo hili linakuwa wazi kabisa. Wimbo wazungumza habari ya umungu wake, anayejitoa kabisa na kuchukua aina ya mtumwa. Na baadaye kutukuzwa kwake mbinguni na kupewa jina la Bwana. Mwanazuoni mmoja anaandika hivi – ni nani ambaye angeweza kufanya hivyo? Mfano wa Kristo kujitoa kabisa ulifanywa ili kutoa wokovu. Kwa vile alifanya alichofanya, sisi twaweza kufanya anachotaka sisi tufanye.
Katika Injili ya Marko – na katika sehemu hii ya mateso – tunakutana na jumbe za wokovu zinazoelezea wazi wimbo huo. Ni nani awezaye kubisha kuwa sadaka aliyozungumzia Yesu si yeye mwenyewe? Siku ya karamu ya mwisho anajitoa mwenyewe awe chakula na kinywaji.   Tunaalikwa tuige mfano wa mtumishi mtii anayeteseka. Ndicho tunachoambiwa katika jumapili hii ya matawi. Lakini zaidi twaambiwa kuwa katika Kristo tunayo nguvu ya kuteseka. Kwa kumpokea yeye, tunapokea nguvu ya kufanya kama alivyofanya yeye.
Tutafakarishwe na mfano huu: Ndugu wawili – mdogo alikuwa jambazi na kila aina ya maisha ya ubaya na yasiyofaa kwa jamii. Kaka mkubwa daima alikuwa akitumia kila aina ya ushawishi na maonyo ili ndugu yake aondokane na maisha hayo ya ujambazi. Usiku mmoja huyu ndugu mdogo jambazi akarudi nyumbani mbio na nguo zake zimejaa damu. Mara akamwambia kaka yake nimeua mtu. Lakini mimi sitaki kufa. Dakika chache baadaye nyumba ikawa imezingirwa na polisi. Wote wawili wakajua wazi kuwa hakuna namna yo yote ile ya kutoroka katika mikono ya askari. Yule ndugu jambazi akaanza kulia sikunuia kumuua yule. Mimi sitaki kufa. Alimwambia kaka yake. Kaka mtu akapata wazo. Akachukua nguo za yule ndugu yake jambazi na kuzivaa. Polisi walipoingia ndani wakamkamata, wakamshtaki na kumhukumu kufa kwa sababu ya kuua. Akafa yeye na ndugu yake akabaki. Alikufa kwa ajili ya ndugu yake. Hiki ndicho anachofanya Yesu kwa ajili yetu.
Kilichopo katika somo la leo na adhimisho la leo ni swala la mapendo – upendo wa Mungu kwetu. Sisi tutalipaje upendo huo? Yule ndugu mdogo atalipaje upendo kwa kaka yake aliyekufa badala yake? Ndugu mpendwa, ni lazima majibu ya maswali yetu yapatikane katika Maandiko Matakatifu. Jibu la kidunia kuhusu kifo ni huzuni, karaha, wasiwasi, mashaka, kilio n.k.
 Jibu la Mungu ni tofauti. Ni furaha, ni utukufu, ni uzima mpya. Mbegu isipoanguka na kuchipua, haitazaa. Ni ajabu kweli. Nabii Ayubu anatuambia, mateso yanapoteza uzito wake yanapohusishwa na upendo wa fumbo la Mungu. Peke yetu hatutaweza kuelewa fumbo zito la ukombozi wetu. Ni katika imani tu twaweza kupata jibu. Mtazamo wa haya tufanyayo upo mbele, kwake Mungu. Hatuwezi kufanya mambo yamhusuyo Mungu na kutaka kupata majibu hapa hapa au hapo hapo au jinsi tunavyofikiri au kutaka sisi. Sisi kama tunamwamini Mungu, tumempokea Yesu, basi tuenende kadiri ya amri na maagizo yake na tumpe nafasi atende kazi yake ndani yetu.
Pd. Reginald Mrosso, C.PP.S.

Wednesday, March 25, 2015

Jumapili ya Matawi

Katika mwaka wa Kanisa wa madhehebu mbalimbali ya Ukristo, Jumapili ya matawi inaadhimishwa jinsi Yesu Kristo alivyoingia Yerusalemu ili kufa na kufufuka kwa wokovu wa binadamu wote. Siku hiyo alishangiliwa na umati kwa kutumia matawi, ndiyo asili ya jina.
Ndiyo mwanzo wa Juma kuu linaloadhimisha matukio makuu ya historia ya wokovu kadiri ya imani ya Wakristo.
Tangu mwaka 1985 siku hiyo Kanisa Katoliki linaadhimisha pia "Siku ya kimataifa ya vijana"

Kulikuwa Jumapili ya Matawi hasubihi, na kijana wa familia moja alikuwa amepatwa na mafua, na hivyo hakuweza kwenda Kanisani pamoja na wana familia wengine. Aliachwa nyumbani. Basi wana familia waliporuri kutoka sherehe za Jumapili walifika nyumbani na matawi yao. Yule kijana akawauliza umaana wa matawi yale. Mama akamjibu, “Umati ulimshangia Yesu akipita kwa kuinua ya matawi juu. Basi yule kijana akajibu kwa mshangao, Jumapili ya pekee ambao sikuweza kwenda Kanisani, na Yesu anakuja binafsi!” Kwa sherehe za Jumapili hii ya Matawi, Kanisa huadhimisha ukubusho wa Bwana Yesu wakati aliingia Yerusalemu mahali atakapokamilisha fumbo la Pasaka, yaani, mateso, kufa na kufufuka kwake. Kwa maandamano ya matawi Jumapili hii, tunaanza rasmi Wiki Takatifu tukielekea Pasaka. Maandamano yenyewe humshangilia Yesu, ambaye hivi punde kwa kifo na ufufuko wake, atarudi kwenye utukufu wa Baba. Jumapili ya Matawi ina pande mbili, yaani pande moja ya furaha na nyingine ya mateso. Tunaona kwanza Yesu akiingia Yerusalemu kwa shangwe na furaha, na pia hivi punde atateswa. Yule anayeingia Yerusalemu kwa shangwe, ndiye pia atayehukumiwa na umati afe msalabani kwa ajili ya dhambi zetu. Hivyo Yesu ndiye mfano maalum wa kutuonyesha jinsi safari yetu ya imani itakapokuwa hapo mwisho, yaani kujinyenyekesha na kuteswa hadi kukubali kufa msalabani, ili Mungu atufufue siku ya mwisho.

Kwenye Injili juu ya Mateso ya Bwana iliyoandikwa na Mtk. Luka tunashirikishwa kwenye mchezo wa kuwiga juu wa ukombozi wetu, lakini mchezo wenyewe ni wa hali ya juu sana. Yesu ndiye anayechukua mahali pa katikati kwenye mchezo huu. Mtk. Luka anatuonyesha kwamba Yesu anateseka na kufa asipokuwa na kosa hata moja (Lk 23:4, 14-15, 22). Yesu anateswa na kuuawa na hadui zake ambao sio Warumi, lakini Mayahudi wenzake (Lk 22: 3,31,53). Maandishi ya Luka juu ya mateso na kufa kwa Yesu umaana wake hasa ni Habari Njema juu ya huruma na usamaho wa Mungu Baba. Hivyo Injili yenyewe ni kama mujiza wa vile Baba huendelea kuonyesha huruma wake kwa wote. Hivyo Yesu anaponya sikio la askari aliyekatwa na Petro; Yesu anamwangalia Petro kwa huruma wakati alimkana mara tatu; na Yesu anamuhurumia mwizi aliyekuwa amehukumiwa kufa msalabani. Kwenye mateso yake huko gethsemani, wakati alikuwa akichekelewa na umati na mateso yake yote msalabani, Yesu ni ishara ya Mungu baina ya watu wake; na pia kama chombo kinachoonyesha upendo na huruma wa Mungu. Kuna ujumbe gani tungepeleka nyumbani Jumapili hii? 1) Tunapotafakari juu ya mateso na kifo cha Bwana, tuyaone pia kwenye maelfu ya watu wetu barani Afrika wanaoteswa na kufa bila kosa lolote. Pia tukumbuke mateso yetu binafsi. 2) Kwenye mateso ya Yesu tunaonyeshwa kwamba Mungu katika upendo na huruma wake hawezi kutuacha peke. Pia tunagundua kwamba hapo mwisho, mateso yatageuzwa kuwa furaha, na kifo kuwa maisha mapya. 3) Tukumbuke kwamba ni kwa ajili ya dhambi zetu Yesu anahukumiwa kufa msalabani, na ni kwa ajili ya upenda na huruma wa Mungu tunapata maondoleo ya dhambi tukitubu na kuungama dhambi zetu.


 ABEL R. REGINALD

Masomo ya Jumapili ya Tano ya Kwaresima Mwaka B wa Kanisa tarehe 22/03/2015

22

 Marchi
 Jumapili ya 5 ya Kwaresima Masomo ya Mwaka "B".
Mwanzo

Ee Bwana Mungu wetu, tunakuomba utusaidie tuwe na mapendo kama ya mwanao, aliyeipenda dunia hata kujitoa auawe. tunaomba hayo kwa njia ya Bwana.........
SOMO  1: Yer. 31:31- 34
Somo katika kitabu cha Nabii Yeremia.
  Angalia siku zinakuja, asema Bwana, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. si kwa mfano wa agano lile nililofanya na Baba zao, katika siku ile nilipowashika mkono, ili kuwatoa katika nchi ya Misri; ambalo agano langu hilo walilivunja, ingawa nalikuwa mume kwao, asema Bwana.
  Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema Bwana; nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.
  Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue Bwana; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema Bwana; ,maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.

WIMBO WA KATIKATI. 
Zab. 19:7-10. 
Kiitikio. Ee Mungu, uniumbie moyo safi..

Sunday, March 15, 2015

Download Picture za Hija ya Vijana iliyofanyika Parokiani Boko tarehe 14/03/2015 hapa

Dominika ya 4 ya Kwaresima tarehe 15/03/2013(Masomo ya Jumapili)

15

 Marchi
 Jumapili ya 4 ya Kwaresima Masomo ya Mwaka "B".
Mwanzo

Furahi, Jerusalemu, mshangilie ninyi nyote mmpendao; furahini, ninyi nyote mliao kwa ajili yake, mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa na faraja.
SOMO  1: 2Nya. 36:14- 16, 19-23
Somo katika kitabu cha pili cha Mambo ya Nyakati.
Wakuu wote wa makuhani, na watu,wakakosa mno sawasawa na machukizo yote ya mataifa; wakainajisi nyumba ya Bwana aliyoitakasa katika Yerusalemu. Naye Bwana, Mungu wa baba zao akatuma kwao kwa mikono wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake; lakini walidhiaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake; na kuwacheka manabii wake, hata alipozidi ghadhabu ya Bwana juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.
wakaiteketeza nymba ya Mungu wakaubomoa ukuta wa Yerusalemu, wakayateketeza kwa moto majumba yake yote, wakaviharibu vyombo vyake vyote vya thamani. Na wale waliookoka na upanga akawachukua mpaka Babeli; wakamtumikia yeye na wanawe hata kulipoingia milki ya Uajemi; ili kulitimiza neno la Bwana kwa kinywa cha Yeremia, hata nchi itakapofurahia sabato zake; kwa maana siku zote ilipokaa ikiwa ilishika sabato, kutimiza miaka sabini.
Ikiwa katika mwaka wa kwanza wa Koreshi, mfalme wa Uajemi, ili kwamba neno la Bwana alilolisema kwa kinywa cha Yeremia lipate kutimizwa. Bwana akamwamsha roho yake Koreshi, mfalme wa Uajemi, hata akapiga mbiu katika ufalme wake wote, akaiandika pia akisema. Koreshi, mfalme wa Uajemi asema hivi; Bwana, Mungu wa mbinguni, amenipa falme zote za dunia; naye ameniagiza nimjengee nyumba katika Yerusalemu, ulioko Yuda. Basi kila mtu katika nyinyi nyote mlio watu wake, Bwana, Mungu wake, na awe pamoja naye, na akwee.

WIMBO WA KATIKATI. 
Zab. 19:7-10. 
Kiitikio. Ulimi wangu na ugandamane 
            Na kaakaa la kichwa changu, nisipokumbuka..

Friday, March 6, 2015

Masomo ya Dominika ya 3 ya Kwaresima, Jumapili ya tarehe 08/03/2015

08

 Marchi
 Jumapili ya 3 ya Kwaresima Masomo ya Mwaka "B".
Mwanzo

Macho yangu humwelekea Bwana daima, naye atanitoa miguu yangu katika wafu. uniangalie na kunihifadhi, Maana mimi ni Mkiwa na mteswa.
SOMO  1: Kut. 20:1- 17
Somo katika kitabu cha Kutoka.
Mungu alinena maneno haya yote akasema, mimi ni Bwana, Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa. Usiwe na miungu ila mimi. Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu ya mbinguni, wala kilicho chini duniani. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana Mungu wako, ni Mungu wenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wananichukiao, nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu. usilitaje bure jina la Bwana, Mungu wako, maana Bwana hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure. Ikumbuke siku ya sabato uitakase. Siku sita fanya kazi, utende mambo yako yote; lakini siku ya saba ni sabato ya Bwana, Mungu wako, siku hiyo usifanye kazi yo yote, wewe wala mwanawako, wala binti yako, wala mtumwa wako,  wala mjakazi wako, wala mnyama wako wa kufuga, wala mgeni aliye ndani ya malango yako. Maana, kwa siku sita Bwana alifanya mbingu, na nchi, bahari , na vyote vilivyomo, akastarehe siku ya saba; kwa hiyo Bwana akaibariki siku ya Sabato akaitakasa. Waheshimu baba na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako. Usiue. Usizini. Usiibe. Usimshuhudie jirani yako uongo. Usitamani nyumba ya jirani yako, usitamani mke wa jirani yako; wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng'ombe wake, wala punda wake, wala cho chote alicho nacho jirani yako.

WIMBO WA KATIKATI. 
Zab. 19:7-10. 
Kiitikio. Wewe, Bwana, Ndiwe Mtakatifu wa Mungu..

Wednesday, March 4, 2015

Tafakari ya Masomo ya Dominika ya 3 ya Kwaresima


Ni Dominika nyingine tena katika kumega mkate, Neno la Mungu litupalo furaha na tumaini la kweli. Basi karibuni tuendelee na wajibu wetu wa kutafakari Neno la Mungu ili kwa njia hii tuweze kuliweka Neno la Mungu katika matendo na kisha lizae matunda. Ni Dominika ya tatu ya Kwaresima na Neno linatualika kusafisha kwa ndani Hekalu la Mungu, ndiyo mioyo yetu.  

Mpendwa somo la kwanza linatoka katika kitabu cha kutoka likiweka mbele yetu amri za Mungu na linatupa mwaliko wa kushika amri hizo. Mungu anaweka amri ili ziwe ni dira ya kuongoza maisha ya watu. Mpendwa kabla ya kuwekwa amri hizi Waisraeli kwa sababu ya kutotii mapenzi ya Mungu walienda utumwani na hivi anapowatoa katika utumwa huo hapendi tena shida hii itokee na hivi anaweka dira na mwongozo wa mapendo yake.

Mpendwa, amri za Mungu hazikuwekwa tu kwa ajili ya kuzishika au kuzikariri bali ni namna ya kujibu mapendo kwa Mungu, ni njia ya kuelekea furaha ya kimungu, ni njia ya kukutana na Mungu atupendaye daima. Amri za Mungu ni namna ya kuongoza maisha ya watu yakae katika msimamo thabiti wa kimaadili ambao huruhusu amani na uelewano kati ya watu. Basi mpendwa unayenisikiliza shikeni amri za Mungu si tu kwa woga bali kama nyenzo, taa, na dira ya maisha yako.

Katika somo la pili, Mtume Paulo anawaandikia Wakorinto akiwataka watambue kuwa wale wote walioitwa na Kristu na watakaoitwa naye baadaye, kwao Kristu ni nguvu na hekima ya Mungu. Fundisho hili linalenga kuvunjilia mbali fikira potofu za Kiyahudi na Kiyunani. Fikira ambazo zilmweka Kristu katika nafasi ya waliolaaniwa na kwamba Mungu ni jambo la kutafuta kwa akili, ni jambo la kifalsafa tu na hivi hakuna haja ya imani. 

Basi anakukumbusha wewe pia, kuwa uwe macho na wale wote ambao wanafikiria dini au imani ni jambo la miujiza na maajabu. Anakutahadharisha usije ukaanguka katika falsafa ya ujanjaujanja ambao huiweka imani katika kipimo lelemama yaani kutowajibika kwa sababu hakuna mahakama. Imani yetu, Neno la Mungu ni maisha na hivi yatupasa kuweka chachu ya Injili katika maisha ya kijamii. Dini si njia ya kujipatia kazi bali njia ya kwenda mbinguni.

Katika somo la Injili, Bwana yuko Yerusalemu, na ni muda mfupi umebaki ili pasaka ya Wayahudi iwadie. Anaona jinsi wafanya biashara ambavyo wanahangaikia mambo ya nje yaani biashara na wanasahau hekalu la Baba yake. Wanalifanya hekalu sehemu ya kawaida ambapo mambo ya kidunia yanaweza kusonga mbele! Anawakemea na anasafisha hekalu la Baba yake akisema: “msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara” Bwana anatimiza lile andiko lililonenwa na Nabii Zakaria yakuwa Masiha ajapo hakutakuwa na biashara katika nyumba ya Mungu, Zk 14:21. 

Tunafundisha kuondoa ubaya wote moyoni ili Bwana aiingie na kupata kukaa nasi. Atufundisha kuwa mioyo yetu kwa njia ya ubatizo ni hekalu la Mungu, ni kikao cha hekima ya Mungu yaani Roho Mtakatifu. Bwana anatangaza ufalme wa kimasiha na hivi mchanganyo wa uchumi na dini anautupilia mbali.

Sehemu ya pili ya Injili yatufundisha juu ya NGUVU ya BWANA kujenga hekalu kwa siku tatu!, Umungu wake na Habari ya Ufufuko upeo wa wokovu wetu. Anatangaza mwanzo mpya wa ufalme wa Mungu, na anataka wale wote watakaomfuata watambue kuwa hekalu si jengo bali ni ufufuko wa Mwana wa Mungu. Hekalu ni jumuiya ya watu walio na imani ya kweli na wako chini ya Kristu mwenyewe aliye Masiha.

Kumbe mpendwa, ninakusindikizeni daima katika kukua na kutambua wajibu wako wa kusafisha hekalu kwa njia ya kitubio na Ekaristi na kwa namna hiyo Mwana wa Mungu ataweza kuja kwako nawe utazidi kusonga mbele katika safari ya wokovu ukiwa jiwe hai na hekalu safi lisilo na doa.

Nakutakieni heri na baraka za Mungu katika Dominika hii, tukutane tena siku kama ya leo kwa chakula zaidi cha roho zetu. Tumsifu Yesu Kristo.

Ni Padre Richard Tiganya, C.PP.S.

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR