Friday, June 27, 2014

Ibada ya kumwaga Sr. Crescentia Kapuli -Ubungo Riveside

Jumapili tarehe 29 juni 2013 Sherehe za Watakatifu Petro na Paulo miamba wa Imani

Jumapili tarehe 29 Juni 2014 Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Sherehe za Watakatifu Petro na Paulo, miamba wa imani, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Hawa ni “vigogo” wa imani waliojitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa mataifa kwa njia ya mahubiri, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao, wakawa tayari kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.

Hii ni Jumapili ambayo Baba Mtakatifu anatarajiwa kutoa Pallio Takatifu kwa Maaskofu wakuu wa Majimbo makuu walioteuliwa hivi karibuni, kama kielelezo cha umoja na mshikamano kati ya Maaskofu wakuu na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hii pia ni siku ya mshikamano kwa kuonesha upendo kwa Baba Mtakatifu kwa njia ya sala, lakini kwa kuchangia katika Mfuko maalum wa huduma ya mshikamano na upendo unaotekelezwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro, sehemu mbali mbali za dunia.

Mchango huu unaotolewa na waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema unamwezesha Baba Mtakatifu kuwasaidia watu waliokumbwa na majanga asilia kama vile matetemeko ya ardhi, mafuriko, njaa, ukame. Ni msaada unalenga kumsaidia mtu mzima katika mahataji yake: kiroho na kimwili, kwa kuchangia maboresho katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele kwa ajili ya kuwasaidia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kwa kuwajengea uwezo ili kukabiliana na changamoto za maisha kwa ujasiri mkuu.

“Usiwasahau maskini” ni maneno ambayo Kardinali Claudio Hummes alimwambia Baba Mtakatifu Francisko mara tu baada ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki. Maneno haya yakaingia na kunata katika akili na moyo wa Baba Mtakatifu Francisko, ambaye leo hii maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni anawapatia kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wake, si kwa maneno tu bali kwa njia ya ushuhuda wa maisha. Papa akamchagua Mtakatifu Francisko wa Assis mpenda amani, mazingira na mhudumu wa maskini kuwa msimamizi wake, leo hii mjini Vatican wimbo umebadilika, mwenye macho aambiwi tazama!

Siku ya Upendo wa Papa ilianzishwa kunako tarehe 8 Agosti 1871 na Papa Pio IX katika Waraka wake wa kichungaji “Saepe Venerabilis” na tangu wakati huo, kila mwaka ifikapo tarehe 29 Juni, Kanisa linashikamana na Papa kuonesha upendo na ukarimu kwa kuchangia mfuko unaogharimia shughuli mbali mbali za upendo zinazotekelezwa na Baba Mtakatifu sehemu mbali mbali za dunia.

Nawe unaweza kushikamana na Papa kwa kuchangia katika mfuko huu! Kwa njia hii, unashiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya kwani maisha na utume wa Kanisa unaendelea kupanuka siku hadi siku!

Thursday, June 26, 2014

World cup 2014 live here>>>>>>>>>.Angalia mechi zote za kombe la Dunia hapa

click here  Portugal vs Ghana
Bonyeza hapa Portugal vs ghana

Safari ya Mwisho ya Marehemu Sr. Kapuli (wasifu wa Sister aliye uwawa na majambazi)


 Sr. Crescentia Kapuli (52) wa Shirika la Bikira Maria Malkia wa Mitume, Jimbo Katoliki la Mbeya meuwawa kikatili kwa kupigwa risasi kifuani na watu wanaosadikiwa kuwa ni amajambazi, siku ya Jumatatu alasiri, tarehe 23 Juni 2014 wakati akitoka Benki, eneo la Ubungo Riverside, Dar es Salaam. 
Jimbo kuu la Dar es Salaam Alhamisi tarehe 26 Juni 2014, majira ya saa 5:00 asubuhi linatarajia kuadhimisha Ibada ya Misa takatifu kwenye Parokia ya Mtakatifu Gaudencia, Makoka kwa ajili ya kumwombea na hatimaye, kuanza safari kuelekea Jimboni Mbeya, atakapopumzishwa kwenye makao ya milele pamoja na watawa wenzake
 Wasifu wa marehemu
Sr. Crescentia Kapuli wa Shirika la Watawa wa Bikira Maria Malkia wa Mitume Jimbo Katoliki Mbeya. Amezaliwa katika Kijiji cha Mkulwe, Wilaya ya Mbozi, mkoani Mbeya, Agosti, 29, 1962 katika Kijiji cha mkulwe na kupata ubatizo Agosti, 31, 1962 huko Mkulwe na nambari ya cheti cha Ubatizo ni LB 19703, amepata Komunio ya kwanza Oktoba,11, 1972 na kuimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara Oktoba, 12, 1972 huko huko Mkulwe.

Sr.Crescentia alikuwa ni mtoto wa mwisho kati ya watoto 12 wa Mzee Peter Kapuli na Mama Maria Nakana. Sr.Cresensia ameingia utawani kama mwomboaji kunako mwaka 1979. Upostulanti mwaka 1980. Unovisi mwaka 1981 hadi mwaka 1983. Akafunga nadhiri za kwanza tarehe 12 Desemba 1983 na baadaye kunako tarehe 12 Desemba 1991 akafunga nadhiri za daima. Tarehe 31 Mei 2009 akaadhimisha Jubilee ya miaka 25 ya maisha yakitawa.

ELIMU
Alipata elimu yake ya msingi katika shule ya msingi Mkulwe mwaka 1972 hadi 1978, elimu ya Sekondari katika Shule ya Sekondari ya Bigwa ( Bigwa SR’s Secondary School) Mwaka 1994 hadi Mwaka 1997, amesoma chuo cha maarifa ya nyumbani homecraft Mwanjelwa mwaka 1991 hadi mwaka 1992, amesoma Chuo cha Uhasibu Mbeya na Dare Es salaam Mwaka 2000 hadi Mwaka 2002.

UTUME

Sr. Crescentia amewahi kufanyakazi katika Convent ya Kyela akifanya Utume Parokiani mwaka 1984 na kusimamia mradi wa mashine ya kusaga katika nyumba ya watawa iliyoko Mlowo mwaka 1985. Msimamizi wa Jiko la Nyumba ya Utawala Jimbo Katoliki la Mbeya mwaka 1986 hadi mwaka 1989. Mlezi msadizi wa Wanafunzi wa Kitawa(Wanovisi) Mlowo mwaka 1993 hadi mwaka 1998. Mlezi Msaidizi wa Wanafunzi wa Kitawa - Kisa Aspiranti Mwaka 1999 hadi mwaka 2000.

Utume katika Convent Parokia ya Mwambani mwaka 2001. Utume Uaskofuni Convent akiwa Mama Mkubwa wa nyumba na Mhasibu Jimboni Mbeya mwaka 2002 hadi 2009. Utume Gua Convent akiwa Mama Mkubwa wa nyumba; Utume Parokiani na Mlezi wa Wawata 2009 – 2011.

Utume Jimbo kuu la Dar es Salaam akiwa Mama Mkubwa katika Convent ya Makoka, Mhasibu Sekondari ya Makoka na Chuo cha Ufundi cha Mwenyeheri Anwarite 2011 – 2014 hadi mauti yalipomfika.

Jimbo kuu la Dar es Salaam, Alhamisi asubuhi tarehe 26 Juni 2014 wanaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumwombea na kumwaga Marehemu Sr. Crescentia Kaupili na baadaye msafara utaondoka kuelekea Jimboni Mbeya. Taarifa za awali zinasema mara baada ya kuwasili kwa mwili wa marehemu Sr.Cresensia utaingizwa katika makao makuu ya Shirika la Bikira Maria Malkia wa Mitume, Jimbo Katoliki la Mbeya.

Baada ya kutoka katika makao makuu ya Shirika safari itaanza kuelekea katika safari yake ya mwisho hapa duniani Sr.Cresensia katika shamba la Mungu la Masista maeneo ya Hasamba, wilayani Mbozi, mkoani Mbeya. Maziko yanatarajiwa kufanyika Jumamosi, tarehe 28 Juni 2014, Mama Kanisa atakapokuwa anaadhimisha Siku kuu ya Moyo Safi wa Bikira Maria.

Raha ya milele umpe ee Bwana na mwanga wa milele umwangazie apumzike kwa amani, Amina.

MASOMO YA 29 JUNI JUMAPILI YA 14 YA MWAKA "A" 2014 (KIJANI)

29
   JUNI 
 JUMAPILI YA 14 YA MWAKA "A"
2014 (KIJANI)


RATIBA ZA IBADA
KIGANGO CHA BOKO.
IBADA YA MISA YA KWANZA 12:15 – 1:45 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 2:00 – 3:50 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA TATU SAA 4:00-5:20 ASUBUHI
KIGANGO CHA MBWENI.
IBADA YA MISA YA KWANZA 1:15 – 2:55 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 3:00 – 4:50 ASUBUHI
KIGANGO CHA MT. RAFAEL.
IBADA YA MISA YA KWANZA 1:00 – 2:55 ASUBUHI
IBADA YA MISA YA PILI 3:00 – 4:50 ASUBUHI
KIGANGO CHA ANTHONY WA PADUA – MBWENI MPIJI.
IBADA YA MISA NI 3:00 – 5:00ASUBUHI

SOMO 1:Zek.9:9-10


Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, mfalme wako anakuja kwako; Ni mwenye haki, naye ana wokuvu; ni mnyenyekevu, amepanda Punda; naam, mwana-punda, mtoto wa Punda. Na gari la vita nitaliondoa liwe mbali na Efraimu, na Farasi awe mbali na Yerusalemu, na upinde wa vita utaondolewa mbali; naye atawahubiri mataifa yote habari za amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka mto hata mwisho wa dunia.



SOMO 2:1Rum. 8:9, 11-13

Roho wa Mungu anakaa ndani yetu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na roho wa Kristo, huyo si wake. Lakini ikiwa roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa roho wake anayekaa ndani yenu. Basi, kama ni hivyo, ndugu, tu wadeni, si wa mwili tuishi kwa kufuata mambo ya mwili; kwa maana kama mkiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa roho, mtaishi.



INJILI: Mt.11:25-30

Wakati ule Yesu alijibu, akasema, Nashukuru, Baba, Bwana wa mbingu na Nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako. Akasema, nimekabidhiwa vyote na Baba yangu; wala hakuna amjuae mwana, ila Baba; wala hakuna amjuae Baba, ila mwana, na ye yote ambaye mwana apenda kumfunulia. Nyoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kuelemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini; na mzigo wangu ni mwepesi.



 MATANGAZO

mara baada ya misa ya pili saa 4:00 asubuhi, Parokiani Boko, mazoezi ya washiriki wa ziara ya taendelea;

Jumanne tarehe 1/7/2014 tunatarajia kuanza safari ya kuelekea Dareda, na tutainjilisha hapo kwa siku nne na tarehe 5/7. tutaelekea parokia ya BM-mpalizwa mbinguni Sanu ....tarehe 6/7 tutaenda parokia ya Daudi na endabashi na tarehe 7/7 tutaenda Mbuga ya Wanyama ya Ngorongoro,,,,,Sisi ni Askari kamili wa Yesu tuzidi kuombeana tuweze kwenda kumtangaza huyu Yesu ambaye ndiye Njia ya Uzima na Ukweli katika Maisha yetu sisi Vijana.......Mapen

Tunawatikia Dominika njema, Amani ya Bwana Iwe nasi.........Mapendo sana,,,,,,,

MAJAMBAZI WALIOMUA MTAWA ( SISTER KAPULI) WA MAKOKA

POLISI Kanda Maalumu ya Dar es Salaam imeanzisha msako mkali, kuwatafuta watu waliohusika na mauaji ya Mhasibu wa Kanisa Katoliki Parokia ya Makoka jijini Dar es Salaam, Sista Cresencia Kapuri (50), ambao utahusisha vikosi vyote vya Polisi. Vikosi hivyo ni Usalama Barabarani, askari wa doria wanaotumia pikipiki na magari, wapelelezi na askari Polisi wa kawaida.
 
Mauaji ya mtawa huyo, yalitokea juzi mchana katika eneo la Ubungo Riverside, jijini humo, ambapo alipigwa risasi na watu wanaodaiwa kuwa ni majambazi na kumpora Sh milioni 20 pamoja na nyaraka mbalimbali za ofisi.
 
Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Mkoa wa Dar es Salaam, Suleiman Kova, aliwaambia waandishi wa habari ofisi kwake jana kuwa Sista Cresencia wakati anapigwa risasi, alikuwa ameongozana na wenzake, ambao ni Sista Brigita Mbaga (32) na dereva wao Mark Mwarabu, aliyekuwa akiendesha gari aina ya Toyota Hilux Pick-Up, yenye namba T213 CJZ.
 
Kova alisema wakati watawa hao, wakitoka katika Benki ya CRDB Tawi la Mlimani City, walipofika Ubungo Riverside kulipa deni la chakula katika duka la Thomas Francis, ndipo walitokea watu hao wawili wanaodaiwa kuwa ni majambazi wakiwa na pikipiki, ambayo haikusomeka namba, huku mmoja akiwa na bunduki aina ya SMG.
kova  
“Yule dereva wa gari la masista walimpiga risasi katika kidole gumba cha mkono wa kulia na kisha kumpiga mtawa huyo risasi ya kifuani na kupora kiasi hicho cha fedha na nyaraka hizo,” alisema Kova. 
 
Alisema kuwa jambo kubwa walilogundua ni kuwa matukio mengi ya ujambazi, hasa unaohusisha wananchi kuporwa kiasi kikubwa cha fedha, yanaanzia katika mabenki, hivyo kuna uwezekano wa watu ambao si waaminifu, wanafanya uhalifu huo.
 
Alisema kuwa katika matukio ya aina hiyo, majambazi huwafuatilia wateja wanapoingia au kutoka katika benki mbalimbali.
 
Alisema imeonekana kwamba mara nyingi benki, zinapohitaji kusafirisha pesa nyingi, hutumia askari au taasisi nyingine za usalama kusafirisha fedha zao.

Tuesday, June 24, 2014

Mtakatifu Gaspar mtume hodari wa Damu Azizi ya Yesu, rafiki na mtetezi wa wanyonge! (precios bloods fathers in Tanzania)



Yafuatayo ni mahubiri yaliyotolewa na Padre Reginald Mrosso, Mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Gaspar del Bufalo, Mwanzilishi wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 21 Oktoba.

Katika Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki tunasoma hivi “Mungu aliye mkamilifu bila mpaka na mwenye heri ndani yake mwenyewe, katika mpango wa wema wake tu, alimwumba mtu kwa hiari yake apate kumshirikisha uzima wake wenye heri. Kwa sababu hiyo, wakati wote, na mahali pote yupo karibu na mwanadamu. Humwita mwanadamu na kumsaidia ili amtafute, amjue, na ampende kwa nguvu zake zote. Anawakusanya watu wote, ambao dhambi iliwatawanya, katika umoja wa familia yake, Kanisa. Ili apate kukamilisha hayo, wakati ulipotimia alimpeleka Mwanawe kama Mwokozi na Mkombozi. Ndani ya Mwanawe na kwa njia yake anawaita watu wafanyike kuwa wana wake katika Roho Mtakatifu, na hivyo wawe warithi wa uzima wake wenye heri”.

Mtume Petro – 1Pet. 1: 13-21 – anatuita tuiishi dhamiri hii. Sisi tunayo matumaini yanayotuhimiza tuwe watakatifu. Sisi tumekombolewa si kwa fedha au dhahabu, bali kwa DAMU YA KRISTO. Hivyo tuishi kama watakatifu kwa mfano wa Mungu aliyetuita katika imani.

Hapa tunatambua kuwa Mungu amekuja kati yetu na amekaa nasi na kila mmoja wetu anaalikwa kuishi na kuutangaza uzima huu mpya. Mtakatifu Gaspari del Bufalo alitambua vizuri kabisa mpango huu wa Mungu kwa ajili ya wokovu wa mwanadamu. Aliweka katika matendo ufahamu huo akitoa ushuhuda na hata kumwaga damu yake kama Kristo kwa ajili ya ndugu zake.

Leo tunakaa hapa pamoja kusali na kutafakari juu ya ukuu huu Mungu na upendo wake kwetu lakini zaidi pia tunatafakarishwa juu ya wajibu wetu mbele ya Mungu na watu wake.

Mtakatifu Gaspari alipoanzisha Shirika alichagua tasaufi ya Damu takatifu iwe karamu yetu ikiongozwa na vipengele vikuu vine – agano, kikombe, msalaba na upatanisho. Katika adhimisho la Jubilee kuu ya Mwaka 2015 Shirika limechagua maandalizi ya adhimisho hilo kuu kwa kufanya tafakari ya kina juu ya uwepo wake na ushuhuda wake hapa duniani. Maadhimisho kuelekea Jubilei hii kuu yalianza rasmi mwaka 2013 kuelekekea 2015 kwenye kilele – mambo ambayo tunayafanya:

Mwaka wa kwanza – 2012-2013 -Kuangalia historia yetu tulikotoka na uaminifu kwa karama yake.

Mwaka wa pili – 2013-2014 - Kuangalia wakati wetu wa sasa – ni kwa jinsi gani tunaishi karama ya upatanisho katika dunia ya leo.

Mwaka wa tatu – 2014-2015 - Kuangalia utume wetu – ni kwa namna gani tunaweza kutoa jibu kwenye kilio cha damu.


Leo tunakutana katika adhimisho la sadaka takatifu ya misa tukiwa pamoja na kama taifa la Mungu linaloamini uwepo wake Mungu Baba mwenyezi. Na dhamira yetu kuu mwaka huu ni upatanisho. Tunajiuliza je upatanisho maana yake nini? Upatanisho ni tendo la uponyaji. Ni tendo linalorudisha mahusiano kati yetu na Mungu na kati yetu.

Uwepo wa Kristo umeleta wokovu wa milele. Neno wokovu linaeleza dhana ya kuwekwa huru. Kwa kutupatanisha naye, tumepewa wajibu mpya kumtumikia Mungu mzima.

Zaburi ya 85 inatukumbusha tena wajibu wetu wa kutafuta upatanisho na Mungu na watu wake. Utuponye tena Ee Mungu, mwokozi wetu…. Wokovu wake ni karibu na wenye kumcha, utukufu wake utakaa katika nchi yetu, wema na uaminifu zitakutana, haki na amani zitabusiana. Uaminifu utachipuka katika nchi, na haki itachungulia kutoka mbinguni. Naye Bwana atatoa yaliyo mema, na nchi yetu itatao mazao, haki itatangulia mbele ya Bwana, wokovu utafuata nyayo zake.

Kama walivyofanya wana wa Israeli katika sala hii, wanamkubusha Mungu fadhila zake kwao na zikijumuisha msamaha wa hatia zao. Wanatambua makosa yao na wanaomba Mungu awajenge upya tena. Hapa baada ya kutoka utumwani wanatambua ubaya wa dhambi na balaa zake na wanataka kujijenga upya na kuanza upya katika yote. Wajibu wetu leo ni kujenga na kuendeleza huo ufalme mpya wa Mungu ulioletwa kwa njia ya Kristo na kanisa lake.


Baba Mtakatifu mwenye heri Yohani Paulo II katika mojawapo ya mafundisho yake anaeleza kuwa - ukombozi wa mwanadamu umefanyika kwa Kristo kumwaga damu yake. Kwake yeye sisi tumefanywa wana – Efe. 1:3…ametuchagua kabla ya kuumbwa ulimwengu ili tuwe wake. Na kwa njia yake tumepokea neema ya kuwa wana na kuwa watakatifu. Hii zawadi ya neema imeletwa kwetu kwa njia ya Kristo.

Na kwa namna hii Mungu Baba amefanya mageuzi makubwa kwetu – ukombozi toka utumwa wa dhambi, ukombozi kwa njia ya damu yake, msamaha wa dhamhi kwa neema yake na kuwa wana katika Mwanaye. Kifo cha Kristo msalabani, tendo kuu kabisa la upendo na umoja, humwaga kwetu mwanga mkuu na kutujalia busara ya kimungu.

Katika lugha ya kibiblia – akili au ufahamu huelezwa au kuonekana katika pendo na kwa maana hiyo pendo hutuingiza katika fumbo la mapenzi yake Mungu ambapo lengo lake ni wokovu – mwisho wake ukiwa ni kuunganisha yote mbinguni na duniani chini ya Kristo. Anahitimisha akisema au tukialikwa au tukimwomba Mungu atujalie neema ya kuona, kutafuta na kutafakari mema ya mbinguni na si ya hapa duniani.

Narudia tena, sisi ambao tumepatanishwa na Damu ya Kristo tumepewa wajibu mpya.

Mtume Paulo katika - 2Kor. 5:17-21 – basi mtu akiwa katika Yesu Kristo ni kiumbe kipya. Ya kale yamepita, mapya yamefika. Hayo yote yanatoka kwa Mungu. Yeye ametupatanisha naye kwa ujumbe wa Kristo, akatukabidhi sisi kazi ya usuluhishaji. Yaani, Mungu ameipatanisha dunia naye katika Kristo, kusudi asiwahesabie watu tena makosa yao. Akaliweka neno la upatanisho ndani yetu. Basi, tumekuwa wajumbe mahali pa Kristo, kwa maana ni Mungu anayeonya kwa huduma yetu. Na ombi tunalotoa kwa jina la Kristo ndilo mpatanishwe na Mungu. Yeye amemfanya yule asiyejua dhambi kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili na sisi tuwe uadilifu wa Mungu katika yeye.

Sisi leo kama Mtakatifu Gaspari tunaalikwa kutafakari vyema nguvu ya upendo wa Kristo aliyemwaga damu yake na akatupatanisha na Mungu. Tendo hili la Mungu ni pendo takatifu na hivyo basi sisi tunaomwamini Mungu tuna lazima ya kuingia katika falsafa hii ya wokovu. Huu ni utume wa Kanisa na kila mkristo. Sisi tumesamehewa makosa yetu kwanza na Mungu. Ni wajibu, ni lazima, si hiari. Je mimi, wewe, sisi ni sababu ya upatanisho?


Ili upatanisho utokee ni lazima mambo manne yawepo; ukweli, huruma, haki na amani. Na tujiulize sote tulioko hapa leo je tunazo sifa hizo katika maisha yetu.

Kristo kwa kumwaga damu yake ametukomboa toka mauti na kutupatanisha tena na Mungu Baba. Mara nyingi tunapofikiria kuhusu sakramenti ya upatanisho tunatingwa. Huwa tunatatizwa zaidi na ubaya au ukubwa dhambi zetu. Kwa hiyo tunakata tamaa, Kwa hakika tafakari yetu ingetakiwa itambue kwanza huruma ya Mungu ambayo ni kuu kuliko dhambi zetu.

Kama tutafikiria zaidi juu ya dhambi zetu na kuogopeshwa sana kama vile hutujapatanishwa naye Kristo, basi hatuna cho chote cha kuadhimisha, au cha kusherehekea au kinachotuwajibisha. Upatanisho hautatafutwa wala kupatikana. Tafakari yetu kuu na ya kwanza ni juu ya huruma ya Mungu isiyo na mwisho, isiyopunguka, na ikiwa hivyo basi tuna kila sababu ya kufurahi na kushangilia. Tufikirie kwa mfano Injili ya Luka sura 15: kondoo aliyepotea, shilingi iliyopotea, mwana mpotevu.

Fundisho hilo ni juu ya huruma kuu ya Mungu. Hata kama tumekata tama, Mungu husamehe, Mungu hufurahi na hukamilika katika kusamehe. Kristo amekufa ili kudhihirisha pendo hilo kuu la Mungu kwetu. Huo ndio upendo kamili.

Sisi tumekombolewa kwa Damu yake Kristo. Sisi tuliokuwa na dhambi tumekombolewa. Sisi ambao hatukustahili tena upendo wake Mungu, tumetakaswa kwa neema yake. Haijalishi wingi na ukubwa wa dhambi zetu, huruma ya Mungu ni kuu zaidi. Mungu ametupatanisha naye. Hiyo ndiyo furaha yetu. Somo la Injili latukumbusha uwepo wa majaribu lakini pia ipo nguvu ya ushindi kama tukibaki pamoja na Kristo. – katika somo la Injili sala ya Yesu kuhusiana na majaribu, wafuasi wanaahidi kushiriki kikombe cha mateso. Lakini baadaye unapatikana wokovu.

NCHI YANGU FAHARI YANGU TOUR